Breaking News

Your Ad Spot

Oct 8, 2016

KIMBUNGA MATTHEW CHAUWA TAKRIBAN WATU 900 HAITI

Haiti nach Hurrikan Matthew (Reuters/A.M. Casares)
Kimbunga kijulikanacho Matthew kimewaua takriban watu 900 nchini Haiti na kusababisha maelfu ya wengine kupoteza makazi kabla ya kuvuma kuelekea katika jimbo la Florida nchini Marekani siku ya Ijumma (07.10.2016).
Idadi ya vifo nchini Haiti, taifa masikini zaidi katika bara la Amerika iliongezeka hadi 887 huku taarifa zikianza kupokelewa kutoka vijiji na maeneo ya mbali yasiyofikika kwa urahisi nchini humo ambayo yaliathirika vibaya na kimbunga hicho.
Huku mawasiliano ya simu yakiwa yamekatika, umeme kutokuwepo, barabara kujaa maji, nyumba kuporomoka na madaraja kusombwa na mafuriko, msaada umechukua muda kuwafikia walioathirika zaidi na kimbunga hicho kusini magharibi mwa Haiti.
Chakula kinaripotiwa kuwa haba katika taifa hilo ambalo bado linajaribu kujikwamua kutokana na athari za tetemeko kubwa la ardhi lililoikumba mwaka 2010. Takriban watu saba wanaripotiwa kufariki kutokana na maradhi ya kipindupindu, maambukizi yanayohofiwa yamesababishwa na maji ya mvua kubwa kuchanganyika na maji taka.
Kimbunga Matthew chaitikisa Haiti
Vituo vya afya vya vijijini vimefurukia wagonjwa miongoni mwao waliovunjika mifupa na hawajapokea matibabu tangu siku ya Jumanne. Meli iliyobeba makontena tisa ya chakula na dawa imeelekea katika eneo la Dame Marie.
Misaada inayosafirishwa kwa njia ya barabara, majini na angani inapelekwa pia katika maeneo mengine yaliyoathirika. Helikopta mbili za jeshi la Marekani zimepeleka tani 50 ya maji, chakula na dawa katika eneo la Grand'Anse. Ufaransa pia imetangaza inapeleka misaada Haiti.
Mashirika ya kutoa misaada yamesema takriban watu milioni moja wanahitaji misaada ya dharura nchini humo. Kulingana na Umoja wa Mataifa, katika baadhi ya maeneo, asilimia 80 ya mimea imeharibiwa na kimbunga hicho.
Mamia ya watu hawajulikani waliko na inahofiwa kuwa idadi ya waathiriwa huenda ikaendelea kuongezeka huku shughuli za uokozi zikianza katika baadhi ya maeneo ya pwani, siku nne baada ya kimbunga Matthew kuikumba nchi hiyo ambayo imelazimika kuahirisha uchaguzi mkuu uliokuwa ufanyike siku ya Jumapili.
Kimbunga Matthew kinatajwa kuwa kibaya zaidi kuwahi kuikumba Haiti, nchi nyingine za Carribean na Marekani katika kipindi kirefu.
Marekani katika hali ya tahadhari
Kimbunga Matthew pia kilisababisha maelfu ya watu kuhamishwa makwao katika majimbo ya Florida, Georgia, South Carolina na North Carolina nchini Marekani ili kupeusha vifo na maafa. Rais wa Marekani Barack Obama amewaomba watu wa majimbo hayo kuitikia wito wa kuhamia maeneo salama na kuzingatia maagizo ya kiusalama. Obama aliwaambia wanahabari kuwa uwezekano wa mafuriko, vifo na uharibifu mkubwa wa mali upo.
Kituo cha Marekani kinachofuatilia vimbunga NHC, kimeshusha nguvu za kimbunga hicho kilichaonza kuvuma siku ya Jummanne katika kiwango cha nne katika vipimo vya Saffir Simpson ambapo kilivuma kwa kilomita 230 kwa saa, hadi kiwango cha pili kufikia jana Ijumma kikivuma kwa kasi ya kilomita 195 kwa saa.
Kumeripotiwa vifo vya watu wanne katika jimbo la Florida vinavyohusishwa na kimbunga hicho lakini mpaka sasa hakujaripotiwa maafa makubwa katika miji ambayo mafuriko yaliiangusha miti na kusababisha kiasi ya watu milioni moja kukosa umeme.
Gavana wa Florida, Rick Scott amewatayarisha wanajeshi wa ulinzi wa taifa 3,500 ili kusaidia hali kwenye jimbo hilo. Wataalam wanasema maeneo ya jimbo hilo yatakuwa kwenye hali ya kudhibitiwa kwa wiki kadhaa baada ya kimbunga hicho kupiga.DW

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages