Breaking News

Your Ad Spot

Nov 24, 2016

UN YAPASISHA MPANGO WA KUUNDWA KAMATI YA KUCHUNGUZA UKIUKWAJI WA HAKI ZA BINADAMU BURUNDI

Nchi wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa zimepasisha mpango wa kuundwa kamati ya uchunguzi kuhusiana na vitendo vya ukiukaji wa haki za binadamu nchini Burundi.
Mpango huo umepasishwa katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa huku serikali ya Burundi ikiendelea kupinga madai ya kuweko ukiukaji wa haki za binadamu nchini humo. Miezi miwili iliyopita, wataalamu wa kujitegemea wa Umoja wa Mataifa waliwasilisha ripoti katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ikielezea kuweko vitendo vya ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu nchini Burundi. 
Ripoti hiyo iliyowasilishwa katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa baada ya wataalamu hao kuitembelea Burundi, ililaani vikali kile ilichokieleza kuwa, ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu katika nchi hiyo ya Kiafrika unaofanywa na vyombo vya usalama.
Rais Pierre Nkurunziza ambaye serikali yake inatuhumiwa kukiuka haki za binadamu
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa kamati hiyo itakuwa na muhula wa mwaka mmoja kufanya kazi yake ya kuchunguza ukiukaji wa haki za binadamu nchini Burundi.
Burundi imekuwa ikishuhudia hali ya mchafukoge tangu mwezi Aprili mwaka jana, baada ya chama tawala cha CNDD-FDD kumuidhinisha Rais Pierre Nkurunziza wa nchi hiyo kugombea kwa muhula wa tatu katika uchaguzi wa rais uliopita.
Kwa mujibu wa asasi za kutetea haki za binaadamu nchini Burundi, hadi sasa kwa akali watu 450 wamekwishapoteza maisha kufuatia machafuko hayo, huku maelfu ya wengine wakilazimika kuwa wakimbizi.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages