Ndugu zangu,
Ikafika siku ile Julius Nyerere
akaenda mwenyewe pale Mlimani kuongea na wanafunzi. Julius alikuwa
makini sana.
Aliposikia juu ya tuhuma zile kutoka kwa Vijana wa TANU dhidi ya akina Museveni na USARF yao, kwamba wanapiga kampeni dhidi ya sera za TANU, alielewa, kuwa huenda kuna ' Majungu Yanapikwa' dhidi ya USARF.
Neno USARF kirefu chake ni ' University Students Africa Revolutionary Front.
Aliposikia juu ya tuhuma zile kutoka kwa Vijana wa TANU dhidi ya akina Museveni na USARF yao, kwamba wanapiga kampeni dhidi ya sera za TANU, alielewa, kuwa huenda kuna ' Majungu Yanapikwa' dhidi ya USARF.
Neno USARF kirefu chake ni ' University Students Africa Revolutionary Front.
Nyerere hakutaka kukimbilia kuwahukumu
USARF, bali, kwenda Mlimani, na kupitia staili yake ya kuongea na
kuruhusu maswali, angepima mwenyewe.
Na ndivyo ilivyokuwa, huku USARF nao
walijipanga chini ya Museveni kupanga mikakati ya siku hiyo Nyerere
atakapokuja kuongea na wanafunzi.
Kuna miongoni mwa wanachama wa USARF
waliofikiri, kuwa strategia nzuri ni kutouliza maswali siku hiyo Nyerere
atakapokuja. Lakini, Museveni akawaambia wenzake kwenye USARF, kuwa
hilo litakuwa kosa kubwa kimkakati, maana, Nyerere ataamini katika
majungu aliyopelekewa na Vijana wa TANU. Tutaonekana wanafiki. Museveni
akawaambia wenzake, kuwa ni lazima waandae maswali.
Kulikuwa na utaratibu wa maswali
kupelekwa kwa Makamu Mkuu wa Chuo kabla siku ya tukio. Museveni akawa na
swali lake pia. Akalipeleka.
Jambo lingine, ni kuwa, kutokana na
USARF kuonekana ni wenye kuwakosoa sana wahadhiri pale Mlimani. Baadhi
ya wahadhiri wenye kuchukizwa na tabia hiyo ya akina Museveni, waliona
ni fursa ya kumtumia Nyerere kuwaumbua USARF hadharani kwa sababu za
kupishana mitazamo kiitikadi.
Ukumbi wa Nkrumah ulijaa, Nyerere
alipomaliza kutoa hotuba tangulizi, Museveni mwenyewe alishangazwa
kusikia ikitamkwa na Makamu Mkuu wa Chuo: " The first questioner is
Yoweri Museveni..." ( Sowing The Mustard Seed, pg, 27)
Museveni analikumbuka swali lake,
lilihusu Ujamaa. Kwamba Nyerere alikuwa na maana gani katika Ujamaa
anaouzungumzia. Museveni alianza kwa kumshambulia Nyerere juu ya dhana
ya Ujamaa kwa kadiri anavyoiwasilisha yeye Nyerere.
Kwa Museveni, alisema ina sura ya
ujima na haiwezi kukidhi matakwa ya itikadi ya kiuongozi wa kisasa.
Kwamba Nyerere anatolea mfano kabila lake ( Wazanaki) kama mfano kwa
Watanzania wengine kuwa ni mfano wa jamii ya kijamaa wakati Wazanaki
walikuwa chini sana kimaendeleo na hawakuwa na matabaka ya kijamii.
Kwa Museveni, hali halisi haikuwa
hivyo sehemu nyingine katika Afrika. Museveni alitoa mifano ya kwao
Uganda, ambako hata kabla ya ukoloni kulikuwa na tawala za Kifalme zenye
matabaka, kama Buganda. Hivyo, akamwambia Nyerere, kuwa huwezi kusema
kuwa Afrika kumekuwa na ujamaa wa watu kuishi kindugu wakati wote.
Kwamba ni wakoloni ndio waliokuja kuharibu mfumo huo.
Baada ya Museveni kushusha kigongo
hicho, Nyerere alitumia nusu saa kujibu swali la Museveni, lakini,
kimsingi, alilizunguka swali la Museveni. Hakulijibu. Mara kadhaa ukumbi
ulikuwa ukilipuka kwa vicheko. Nyerere alikuwa mahiri kwenye rhetoric,
uwezo wa kuongea hadharani.
Lakini, muda wote, Nyerere hata mara
moja hakumponda Museveni wala USARF kama ilivyotarajiwa na Vijana wa
TANU na baadhi ya wahadhiri wa Mlimani.
Nyerere akarudi tena Mlimani mara
nyingine kuongea na wanafunzi. Siku hiyo vijana wa USARF hawakuingia
ukumbini. Nyerere alipomaliza maongezi yake, na wakati akiondoka,
alisikika akiwauliza waandaaji:
" Wale jamaa ' USARF' leo sikuwaona!"
Ndio, moyoni, Nyerere aliwaheshimu na aliwapenda USARF. Nyerere alimheshimu na alimpenda Museveni, kwa misimamo yake.
Maggid Mjengwa,
Ndio, moyoni, Nyerere aliwaheshimu na aliwapenda USARF. Nyerere alimheshimu na alimpenda Museveni, kwa misimamo yake.
Maggid Mjengwa,
0688 37 36 52 ( Whatsapp)
0754 678 252
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269