Breaking News

Your Ad Spot

Jan 30, 2017

MAKAMU WA RAIS MHE. SAMIA AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA BALOZI WA UFARANSA NCHINI NA MWENYEKITI WA CHAMA CHA CUF PROFESA LIPUMBA KWA NYAKATI TOFAUTI JIJINI DAR ES SALAAM

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akimsikiliza kwa makini Balozi wa Ufaransa nchini Mhe. Malika Berak wakati wa mazungumzo yao yaliofanyika ofisini kwake, Ikulu Jijini Dar es Salaam. 
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na Balozi wa Ufaransa nchini Mhe. Malika Berak (kushoto) mara baada ya kumaliza mazungumzo ofisini kwake, Ikulu Jijini Dar es Salaam.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Mwenyekiti wa CUF Profesa Ibrahim Lipumba alipomtembelea ofisini kwake, Ikulu Jijini Dar es Salaam jana.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha ya pamoja na Mwenyekiti wa CUF Profesa Ibrahim Lipumba mara baada ya kumaliza mazungumzo ofisini kwake, Ikulu Jijini Dar es Salaam jana.

...............................................................



Serikali ya Ufaransa kupitia Benki ya Maendeleo ya Nchi hiyo (AFD) imeahidi kuwa inampango wa kuipatia Tanzania mkopo wenye masharti nafuu kutoka wastani wa euro milioni 50 hadi euro milioni 100 kwa mwaka katika miaka ijayo kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo nchini.

Balozi wa Ufaransa hapa Nchini Malika Berak ametoa kauli hiyo Ikulu Jijini Dar es Salaam alipokutana na Kufanya mazunguzo na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kuhusu hatua zilizofikiwa katika uandaaji wa kongamano la uwekezaji litakalofanyika Jijini Dar es Salaam kuanzia mwanzoni mwa mwezi Aprili mwaka huu.

Balozi huyo amesema mkopo huo itaiweza na kuisaidia Tanzania kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ya wananchi hasa katika sekta za maji na usafi wa mazingira na miradi ya umeme. 

Kuhusu uandaaji wa kongamano la uwekezaji nchini, Balozi Malika Berak amemweleza Makamu wa Rais kuwa maandalizi ya kongamano hilo kubwa la Kibiashara linalolenga kujenga na Kuimarisha ushirikiano wa kibiashara kati ya Tanzania na Ufaransa yanakwenda vizuri. 

Balozi huyo amesema kuwa kongamano hilo ambalo litakuwa la Kikanda litajadili kwa kina fursa za uwekezaji hapa nchini hasa kwenye maeneo ya nishati, usafirishaji, teknolojia ya habari na Mawasiliano na miradi ya maendeleo.

Balozi Malika Berak amemhakikishia Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan kuwa kongamano hilo la kibiashara litawakutanisha pamoja wafanyabiashara Watanzania na wenzao wa Ufaransa katika kujadili na kubadilisha uzoefu katika masuala mbalimbali yakiwemo ya kibiashara kama hatua ya kuimarisha shughuli zao za kiuchumi.


Kwa upande wake, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan ameipongeza Serikali ya Ufaransa kupitia kwa balozi wake hapa nchi kwa ufadhili wa miradi mbalimbali ya maendeleo hasa katika sekta ya maji na usafi wa mazingira, nishati na mapambano dhidi ya umaskini nchini.

Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu Hassan amemhakikishia Balozi wa Ufaransa hapa nchini Malika Berat kuwa Tanzania itaendelea kudumisha na kuendeleza mahusiano yaliyopo kwa ajili ya manufaa ya wananchi wa pande Mbili yaani Tanzania na Ufaransa.

Makamu wa Rais pia amepongeza jitihada za Serikali kupitia Ubalozi wake hapa nchini za kuona umuhimu wa kuandaa Kongamano la kibiashara hapa nchini ambalo litatoa fursa kubwa kwa watalaamu wa sekta mbalimbali nchini kukutana na kujadiliana mambo kadhaa ikiwemo fursa za uwekezaji nchini.

Amesisitiza kuwa Serikali ya awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dakt John Magufuli inaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini kwa kupambana na vitendo vya rushwa kama hatua ya kuhamasisha wawekezaji wengi kuja kuwekeza hapa nchini.Makamu wa Rais amemweleza Balozi wa Ufarana hapa nchini kuwa milango ya ofisi yake ipo wazi muda wote hivyo kama watakwama sehemu yeyote katika kuandaa kongamano hilo amfahamishe haraka ili aweze kuchukua hatua haraka kusaidia mchakato huo kutokana na muhimu wa kongamano hilo hasa wakati huu ambapo Tanzania inataka kujenga uchumi wa viwanda nchini.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages