Breaking News

Your Ad Spot

Feb 8, 2017

SPIKA UK APINGA TRUMP KUHUTUBIA BUNGE


Spika wa Bunge la Uingereza John Bercow, amesema rais wa Marekani Donald Trump hafai kualikwa kulihutubia bunge hilo wakati atakapofanya ziara rasmi nchini humo.

Matamshi hayo ya Spika John Bercow (pichani) yanaondoa uwezekano kwa Trump kupewa heshima hiyo wakati wa ziara yake baadae mwaka huu. Bercow aliwambia wabunge kwamba angepinga mwaliko huo hata kabla ya marufuku  ya Trump inayowazuwia raia kutoka mataifa saba yenye Waislamu wengi kuingia nchini Marekani.

"Kabla ya kuwekwa marufuku ya uhamiaji, binafsi ningepinga vikali kuruhusiwa rais Trump kutoa hotuba katika ukumbi wa Westminster. Baada ya kuwekwa kwa marufuku ya uhamiaji na rais Trump, ninapinga hata vikali zaidi hotuba ya rais Trump katika ukumbi wa Westminster," alisema Bercow bungeni siku ya Jumatatu.

Matamshi ya Bercow hayakuwa ya kawaida kwa sababu maspika wa bunge la Uingereza wanatarajiwa kutoegemea upande wowote wa kisiasa. Ni mmoja wa maafisa wa bunge ambao wangekubali kumualika mgeni wa nje kuwahutubia wabunge.

Viongozi wa dunia waliowahi kupewa heshima ya kutoa hotuba kwa mabaraza yote ya bunge ni pamoja na Nelson Mandela, na mtangulizi wa Trump Barack Obama.

Bercow alishangiliwa na wabunge pale aliposema kwamba, inagwa Uingereza inathamini uhusiano wake na Marekani, "upinzani wetu dhidi ya ubaguzi wa rangi na kijinsia, na uungwaji wetu wa usawa mbele ya sheria na mahakama huru, ni mambo yenye umuhimu mkubwa zaidi.

Trump atazuru Uingereza kama mgeni wa Malkia, ziara iliotangazwa na waziri mkuu Theresa may alipomtembelea Trump mjini Washington mwezi uliopita.

Lakini baadhi ya raia wameonyesha mashaka na uharaka wa serikali kuwa karibu na rais huyo mwenye kuchochea mgawanyiko. waraka wa mtandaoni unaopinga ziara ya Trump umesainiwa na zaidi ya watu milioni 1.8, na utajadiliwa bungeni Februari 20.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages