Breaking News

Your Ad Spot

Mar 27, 2017

WATANZANIA WAASWA KULIPIA KODI YA PANGO LA ARDHI

NA GEORGINA MISAMA – MAELEZO
SERIKALI imewataka wamiliki wa ardhi kuhakikisha wanalipia kodi ya pango la ardhi kwa wakati ili kuepuka kunyang’anywa umiliki wa ardhi zao.
Hayo yamesemwa  na Mkuu wa Kitengo cha Mawasilino kutoka Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bi. Mboza Lwandiko wakati akizungumza na waandishi wa habari, Jijini Dar es Salaa.
Mboza alisema kwamba Wizara inakusudia kufanya mnada wa viwanja takribani 10 kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, Temeke na Kinondoni ambavyo havijalipiwa kodi ya pango la ardhi mpaka Machi 24, 2017.
“Usipolipa Kodi ya Pango la Ardhi kwa wakati, utanyanganywa umiliki wa ardhi yako, kutokana na sheria ya Ardhi, Na. 4 ya mwaka 1999, katika kifungu cha 49 na 51”, alisema Mboza.
Naye Mkuu wa Kitengo cha Kodi kutoka Wizara hiyo Bw. Denis Masami  alitoa ufafanuzi wa utaratibu unaotumika kuwasiliana na  wamiliki wa ardhi walioshindwa kulipa kodi kwa wakati na kusema kwamba wadaiwa wanapewa hati ya madai na kupewa muda wa kukamilisha madeni yao.
Muda wa kukamilisha malipo ukipita, amri ya mahakama ya kukamata mali hufuata, ambapo mmiliki wa ardhi atatakiwa kuikomboa ardhi yake kwa kulipa deni mara moja, akishindwa Mahakama hutoa amri ya kuuza mali.
Mahakama imetoa amri ya kwanza tarehe 27/01/2017 ya kukamata mali kwa wadaiwa sugu na tarehe 24/01/2017 mahakama ilitoa kibali kwa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuuza kwa mnada wa hadhara viwanja ambavyo havijalipiwa kodi ya pango la ardhi.
“Tarehe 20 Machi, 2017 Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi ilitoa tangazo la mnada wa hadhara wa kuuza viwanja ambavyo havijalipiwa kodi ya ardhi unaotarajiwa kufanyika Machi 26, 2017”, alisema Denis.
Denis aliongeza kwamba Wizara imeandaa orodha ya wadaiwa sugu, mpaka sasa katika orodha hiyo baadhi ya viwanja vimelipiwa sehemu ya kodi inayodaiwa baada ya wamiliki kuomba kukamilisha sehemu iliyobaki kabla ya kumalizika kwa muhula huo.
Wizara inatoa rai kwa watanzania  wanaomiliki ardhi kujifunza utamaduni wa kulipia kodi pasipo shurti. Kodi ya ardhi hulipiwa kila ifikapo Julai Mosi ya kila mwaka katika Manispaa au Halmashauri husika na katika Ofisi za Malipo ya Kodi-Dar es salaam.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages