Mmoja wa Waandishi wa Habari (kulia) akipiga picha ya bakteria wanaoonekana kwa kifaa maalum cha kuangalia bakteria (Microscope) katika Maabara ya kuaandaa bakteria 15 Mei, 2017 Kibaha, Mkoani Pwani. |
Baadhi ya mitambo iliyopo katika Kiwanda cha Kuzalisha
Viuadudu vya Kuua Viluwiluwi vya Mbu wa Malaria kilichopo Kibaha, Mkoani Pwani.
|
(PICHA/HABARI NA BENEDICT LIWENGA-WHUSM)
Halmashauri
nchini zimetakiwa kuitikia wito wa kununua dawa za kuua viluwiluwi vya mbu wa
malaria zilizoanza kuzalishwa hapa nchini ili kukabiliana na ugonjwa wa
malaria.
Kauli
hiyo imetolewa jana na Kaimu Meneja Mkuu wa Kiwanda cha Kuzalisha Viuadudu vya
Kuua Viluwiluwi vya Mbu wa Malaria cha Tanzania Biotech Products Limited
kilichopo Kibaha Mkoani Pwani, Bw. Samwel Mziray wakati alipokutana na
Waandishi wa habari na kufanya nao mazungumzo juu ya shughuli zinazofanywa katika
kiwanda hicho.
Bw.
Mziray amesema kuwa, dawa za kuua viluwiluwi vya mbu wa malaria zinapaswa
kununuliwa na kila Halmashauri nchini kwa maagizo yaliyotolewa na Serikali kupitia
waraka wake kwa kuwa kiwanda hicho kinachomilikiwa na serikali kwa asilimia 100
kilijengwa ikiwa ni sehemu ya mkakati wa serikali katika kupambana na malaria
nchini. Hata hivyo amebainisha kwamba mpaka sasa mwitikio wa halmashauri umekua
mdogo kwani ni halmashauri mbili tu za Geita pamoja na Mbogwe ndizo
zimeshanunua dawa hizo.
“Lengo
la Serikali kuja na mpango huu ni kupunguza vifo vitokanavyo na malaria nchini
na kupunguza gharama kubwa ya kununua dawa na vifaa tiba vya kupambana na
malaria”, alisema Mziray.
Amesema
kwamba iwapo kama halmashauri zitanunua dawa hizo na kuzitumia, ugonjwa huo
utapungua kwa kiasi kikubwa nchini na hivyo serikali kuelekeza fedha zake
katika shughuli za maendeleo.
Amesema
kwamba, kwa Afrika kiwanda hicho ni moja ya kiwanda kilichobahatika kujengwa
Tanzania ambapo nia ya Serikali ni kutokomeza ugonjwa wa malaria kwa kuharibu
mazalia ya mbu.
Ameongeza
kuwa, kiwanda hiki kitazalisha mbolea ya kibaiolojia (Bio fertilizer) siku za
usoni, lakini kwa sasa kiwanda kinazalisha dawa za aina mbili ambazo ni
Bactivec na Griselesf ambazo hutumika kwa kunyunyuzia katika mazalia ya mbu.
Amefafanua
kwamba, kwa sasa kiwanda hicho kinaweza kuzalisha kwa wingi dawa hizo ambapo
ametaja moja ya nchi iliyonunua dawa hizo ni Niger ambayo tayari imenunua lita
91,000 na nchi nyingine za Serbia na Srilanka ziko katika mazungumzo ya kununua
dawa hizo.
“Niiombe
Serikali iweze kutoa msukumo zaidi kwa halmashauri ambazo bado hazijanunua dawa
hizi kukitumia kiwanda hiki kufikia malengo kwani jamii inapoteza wapendwa wao
kutokana na ugonjwa wa malaria”, alisema Mziray.
Amefafanua
kuwa, dawa hizo zinaweza kutumika katika kipimo cha mililita moja kwa lita 50
za maji na bei ya lita moja ni shilingi 13,000/= na zina uwezo mkubwa wa
kuangamiza viluwiluwi vya mbu wa malaria.
Kuhusu
agizo la Serikali la kuzitaka halmashauri nchini kununua dawa hizo amesisitiza
kwamba utekelezaji wa halmashauri hizo kuja kiwandani unapaswa kuwekewa
kipaumbele na Serikali na halmashauri hazinabudi kuitikia wito huo.
“Serikali
imeshatoa waraka kwa halmashauri zote nchini kuweza kutumia kiwanda hiki
kununua dawa, kwahiyo sasa kilichobaki ni utekelezajina suala la bei sio
kisingizio, suala kubwa ni utayari na kuona umuhimu wa kufikia malengo ya
kutokomeza malaria kwa jamii”, alisema Mziray.
Aidha,
amebainisha kuwa, jukumu la kununua dawa hizo liko chini ya halmashauri husika
na inatakiwa kupanga bajeti yake ya kununua dawa hizo.
Kuhusu
suala la usalama wa dawa hizo amesema kwamba, dawa hizo ni salama kwa binadamu
na Kiwanda kinafanya mawasiliano na vyombo vya habari ili kutoa elimu na mkazo
mkubwa wa kununua dawa hizo.
Kwa
upande wake Kaimu Meneja Masoko na Mauzo wa Kiwanda hicho, Bw. Frank Mzindakaya
amesema kwamba, Serikali hainabudi kutenga bajeti ya kutosha ili kuziwezesha
halmashauri kununua dawa hizo.
Ameongeza
kuwa, dawa za kiwanda hicho wanaziweka katika vipimo mbalimbali ikiwemo vya
lita 20 na ujazo wa miligramu 30 na katika matumizi makubwa mteja mkubwa ni
Serikali yenyewe kwakuwa ndiyo inayonunua kupitia Halmashauri na kwenda kuzinyunyuzia
katika madimbwi. Kwa mwananchi wa kawaida anaweza kununua miligramu 30 ili
aweze kutumia kwa matumizi ya kifamilia ya kujikinga yeye na familia yake.
“Serikali
haijamtwisha mzigo mwananchi yeyote wa kununua dawa hizi ndiyo maana
tunazisisitiza kuwa halmashauri zije kununua dawa hizi ili ziende kuwasaidia
wananchi kwa kuziweka katika madimbwi makubwa na hatimaye kuwalinda wananchi
dhidi ya malaria”, alisema Mzindakaya.
Tanzania
Biotech Products Limited (TBPL) ni
Kampuni tanzu ya Shirika la Maendeleo (NDC) iliyopewa dhamana ya kusimamia na
kuendesha kiwanda cha kuzalisha bidhaa za kibaiolojia zikiwemo viuadudu vya
kuua viluwiluwi wa mbu waenezao malaria (Biolarvicides). Kiwanda hiki kipo eneo
la TAMCO Kibaha, Mkoa wa Pwani.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269