Breaking News

Your Ad Spot

May 11, 2017

MAFURIKO ZANZIBAR KUSABABISHA SHULE ZOTE KUFUNGWA

Mafuriko makubwa yaliyosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha katika visiwa vya Zanzibar ambayo ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yamesababisha shule zote visiwani humo kufungwa kwa muda.
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar amesema kuwa mvua hiyo ambayo pia imekuwa ikinyesha katika kisiwa cha Unguja na Pemba kwa kipindi cha wiki tatu zilizopita pia imeharibu barabara na mali ya watu.
Riziki Pembe Juma amesema kuwa baadhi ya shule zimejaa maji na hivyo kuwa vigumu kwa walimu kufunza mbali na kuwa wanafunzi wanashindwa kufika shuleni kutokana na mafuriko. Waziri huyo ameongeza kuwa, uamuzi huo umefikiwa kufuatia pendekezo kutoka kwa kamati ya kukabiliana na majanga ya Zanzibar ambayo iliishauri serikali kufunga shule hizo kwa usalama wa wanafunzi.
Sehemu ya mbele ya jengo la Uwanja wa Ndege Zanzibar ikiwa imejaa maji
Hata hivyo amesema kuwa wanafunzi wa kidato cha sita waliokuwa wakifanya mitihani yao ya mwisho wataendelea kufanya hivyo.
Taarifa zaidi zinasema kuwa, watu kadhaa wanadaiwa kupoteza maisha kutokana na mafuriko hayo. Nyumba nyingi zimejaa maji yaliyosababisha hasara kubwa. 
Aidha makumi ya familia zimebakia bila makazi baada ya nyumba zao kuathiriwa vibaya na mafuriko hayo. Afisa mmoja wa masuala ya misaada ya kibinamu kwa waathirika visiwani Zanzibar amesema watu wengi wanahitaji misaada mbalimbali kutokana na kuathiriwa mno na mafuriko hayo. Mavazi, misaada ya vyakula, vifaa vya afya na madawa inasemekana kuwa ndio vitu vinavyohitajika zaidi kwa sasa kwa ajili ya waathiriwa wa mafuruki hayo.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages