Breaking News

Your Ad Spot

Jun 23, 2016

MUHIMBILI YATENGUA NAFASI YA MKURUGENZI WA HUDUMA ZA TIBA SHIRIKISHI NA MKUU WA KITENGO CHA KUHIFADHI MAITI


TAARIFA KWA UMMA KUHUSU KUTENGUA NAFASI YA MKURUGENZI WA HUDUMA ZA TIBA SHIRIKISHI NA MKUU WA KITENGO CHA KUHIFADHI MAITI



Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Prof. Lawrence Museru ametengua uteuzi wa Mkurugenzi wa Huduma za Tiba Shirikishi Dkt. Praxeda Ogweyo kuanzia leo Juni 23, 2016 ili kupisha uchunguzi kutokana na kushindwa kusimamia vizuri wafanyakazi walioko chini yake na kusababisha Kitengo cha Kuhifadhi Maiti kuchanganya maiti wakati wa kuzitoa kwa ndugu mara mbili katika kipindi kisichozidi miezi mitatu na kusababisha usumbufu mkubwa kwa wafiwa na Hospitali kwa ujumla. Ikumbukwe kuwa tarehe 9, Aprili 2016 tukio kama hili lilitokea na kusababisha usumbufu mkubwa kwa ndugu, jamii na Hospitali kwa ujumla. Aidha tukio hili tena limejitokeza tarehe 20 Juni, 2016.



Prof. Museru amemteua Dkt. Flora Lwakatare Mkuu wa Idara ya Radiolojia kukaimu nafasi hiyo. Kurugenzi ya Tiba Shirikishi inasimamia Idara ya Mionzi na Idara ya Maabara ambapo Kitengo cha Kuhifadhi Maiti kipo chini ya maabara. Vilevile Prof. Museru ametengua uteuzi wa Mkuu wa Kitengo cha Kuhifadhi Maiti Hospitali ya Taifa Muhimbili Dkt. Innocent Mosha na kumteua Dkt Herbert Nguvumali kukaimu nafasi hiyo.



Aidha, wahudumu waliohusika katika matukio haya wameondolewa katika chumba cha kuhifadhi maiti kuanzia leo tarehe 23 Juni, 2016 ili kupisha uchunguzi. Katika uchunguzi huu, kamati maalumu imeundwa kuchunguza kwa kina utendaji wa Kitengo cha Kuhifadhi Maiti ili kutoa mapendekezo ya jinsi ya kurekebisha utendaji wa kitengo hicho ili matukio kama haya yasitokeze tena.





Imetolewa na;





Aminiel Buberwa Aligaesha,

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano,

Hospitali ya Taifa Muhimbili,

JUNI 23, 2016.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages