Breaking News

Your Ad Spot

Feb 18, 2010

WATANO MBARONI KWA MAUAJI MUSOMA

WATU watano wamekamatwa na polisi mjini mkoani Mara, kwa tuhuma za kuhusika na  mauaji ya watu watu 17 wa familia tatu za ukoo mmoja kwa kuchinjwa na kukatwa mapanga, mjini Muosma, jumatatu wiki hii.
   Katika mauaji hayo, yalitokea, saa sita usiku, mtaa wa Bugharanjabho, kata ya Buhare, Manispaa ya Musoma, mkoani Mara, ambapo yanadaiwa kufanywa na watu wasiofahamika waliwaua watu hao wakiwemo watoto wenye umri wa miezi mitatu na minne..
    Akizungumza na gazeti hili jana Kamanda wa Polisi, mkoani Mara Robert Boaz, alisema watu watano wanashikiliwa kuhusiana na mauaji hayo.
     Familia zilizokubwa na mkasa huo ni ya Kawawa Kinguye ambapo yeye na watoto watano walichinjwa na ya mdogo wake, Moris Mgaya, ambayo watu sita waliuawa kabla ya kuvamiwa nyumba ya binamu yake Mgaya Nyarukende na kumuua.
      Hata hivyo, Boaz alisema hawezi kutaja majina ya watuhumiwa hao ambao walikamatwa juzi kwa sasa kwa sababu za kiupelelezi.
     “Tunawashikilia watu watano, lakini kwa sababu za kiupelelezi hatuwezi kuwataja majina yao,” alisema Kamanda Boaz na kuongeza kuwa watuhumiwa hao wote ni wanaume.
     Kamanda Boaz aliwataja waliouawa katika familia ya Kawawa (48), kuwa ni yeye mwenyewe, mkewe Buki Kawawa (43) na watoto wao Kiguye (15), Magdalena (13), Nyarukembe (9), Juliana (13), Mary (4) na Nyanyama (11).
     Familia ya Moris waliouawa ni mkewe Nyasimo Kitego (65), Mgaya (miezi mitatu), Irene (minne na nusu), Maheri (9). Waliouawa familia ya Nyarukende ni mkewe Umbele Mgaya (32), Joseph Asoseleti (17) na mama mwenye nyumba Dorica Mgaya (60), ambaye alifariki akiwa hospitalini.
    Alisema taratibu za kiuchunguzi za miili ya marehemu zilikamilika juzi na kwamba hali ya usalama imeimarishwa.
    Aliwataja majeruhi ambao wamelazwa hospitali ya mkoa wa Mara kwa matibabu ni Moris (65), ambaye mkewe na watoto wake wanne waliuawa, Maria Kawawa (17) na Maxmilian Robert (18). Alisema hali za majeruhi hao zinaendelea vizuri.
    Maelfu ya wananchi walifurika jana katika mazishi ya watu hao 17, yaliyofanyika kwenye shamba la familia lililopo kijijini hapo.
   Viongozi wa Dini waliotoa ibada ya mazishi walilaani vitendo hivyo na kutaka wahusika wasakwe na kufikishwa katika vyombo vya sheria.
   Tukio hilo la kusikitisha lilitokea juzi, ambapo Mkuu wa Mkoa wa Mara, Enos Mafuru, alimwagiza Kamanda huyo, kufunga baadhi ya vituo na askari kuanza msako dhidi ya wauaji hao.
    Pia aliwataka wananchi kutoa ushirikiano wa hali na mali utakaofanikisha wahusika kutiwa mbaroni na kufikishwa katika vyombo vya sheria.
   Katika hatua nyingine Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), imelaani vikali mauaji hayo na kuliomba jeshi la polisi kwa kushirikiana na jamii kuwafichua wote waliohusika waweze kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria ili sheria ichukue mkondo wake.
    Taarifa ya kulaani maauji hayo, ilitolewa jana na Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Kiongozi mstaafu Amiri Manento.
    “Mauaji hayo ni uvunjwaji wa haki za binadamu ambao unakiuka Haki ya msingi ya kuishi ambayo
imeainishwa katika ibara ya 14 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977,” alisema Jaji Manento.
  Alinukuu ibara hiyo, ‘kila mtu anayo haki ya kuishi na kupata kutoka katika jamii hifadhi ya maisha yake kwa mujibu wa sheria’.
   Pia, tume hiyo imekemea na kulaani vikali vitendo vya watu kujichukulia sheria mikoni mwao.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages