Breaking News

Your Ad Spot

Jun 5, 2011

NAPE AWASHUKIA WATENDAJI NA VIONGOZI WANAOGEUZA MATUKIO YA UJAMBAZI NA MIGOGORO YA WAKULIMA NA WAFUGAJI KUWA VITEGAUCHUMI VYAO

NA MWANDISHI WETU,RUKWA
KATIBU wa NEC, Itikadi na Uenezi CCM, Nape Nnauye amewakata viongozi na watendaji wanaogeuza matukio ya ujambazi na migogoro ya wafugaji na wakulima kuwa vitegauchumi vyao kuacha tabia hiyo mara moja kabla kushukiwa na rungu kali la CCM mpya.
Amesema kuna kila dalili kwamba matukio hayo, yanaendelea kujitokeza na kusabaisha waanchi kuichukua CCM, kutokana na baadhi ya watendaji kuwakumbatia wanaousika na matukio hayo ya uhalifu kwa sababu ya kuhongwa fedha chafu.
Nape alisema  hayo kwa nyakati tofauti wakati akihutubia mikutano ya hadhara iliyofanyika katika kata ya Kabwe wilayani Nkasi na Usevya wilayani Mpanda, akiwa katika ziara na ujumbe wake mkoani hapa.
"Vongozi hawa ndio wanaokitukanisha Chama chetu na kutugombanisha na wananchi kwa sababu ya tamaa zao, sasa naagiza waache vitendo vyao mara moja vinginevyo tutawashukia kwa sababu CCM imeshaamua kupambana  kwa nguvu zake zotena wale wote wanaokichafua Chama kwa matendo yao binafsi." Alisema Nape.
Mapema katika ziara hiyo, viongozi wa  CCM mkoa walimwambia Nape kwamba katika maeneo yaliyopo mwabao wa Ziwa Tanganyika na maeneo waliyowahi kuwa kambi za wakimbizi, kumekwa kukitokea matukio ya ujambazi unaogharimu maisha na mali za wananchi.
Viongozi hao walisema, matukio hayo ya ujambazi yanadaiwa kufanywa na baadhi ya waliokuwa wakimbizi kutoka nchi jirani ambao sasa wameomba uraia, na kwamba kuna kila dalili kwamba baadhi ya viongozi katika maeneo husika wanawafahamu lakini hawatoi taarifa ili wakamatwe kwa kuwa wamewageuza mradi wao wa kuchuma fedha kila wanapofanya uhalifu.
Walisema kutokana na wimbi la ujambazi, hivi karibuni wafanyabiashara wawili katika mji mdogo wa Maji Moto, wilayani Mpanda wameuawa kwa kupigwa risasi na majambazi ambayo hadi sasa hayajakamatwa.
Kuhusu migogoro ya wakulima na wafugaji, viongozi hao walisema, uroho wa fedha wa baadhi ya viongozi na watendaji umesababisha wafugaji kuwa na kiburi kwa kuwa mifugo yao inapolisha kwenye mashamba ya wakulima huwaziba midomo viongozi hao kwa kuwapa fedha.
Akiwa katika mikutano hiyo, Nape aliwaomba wananchi kuwataja viongozi na watendaji wanaoshirikiana na wahalifu hao kwa kuwa wanawafahamu.
"Ninyi mnaoishi katika maeneo haya, bila shaka mtakuwa mnawajua viongozi hawa wanaotuchafulia Chama, nawaomba watajeni hata kwa njia ya siri, nasi tutawashughulikia bila kuwaonea aibu hata kama mhusika atakuwa ni kiongozi mwezetu wa CCM", alisema Nape.
Katika ziara hiyo, Nape ambaye amefuataja na Mjumbe wa NEC, Uchumi na Fedha, Nchemba, mbali na kuhutubia mikutano ya hadhara isiyopungua tisa katika wilaya za Nkasi, Sumbawanga mjini, Mpanda na wilaya mpya ya Mlele, pia alikagua ujenzi wa miradi ya maendeleo.
Miongoni mwa miradi aliyotembelea ni ujenzi wa zahanati katika Kata ya Maji Moto wilayani Mpanda ambayo ujenzi wake unatarajiwa kugharimu sh. milioni 60 utakapokamilika na ghala la kuhifadhi mazao ya wakulima katika kata hiyo.
Pia alikagua ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami ya kutoka Tunduma-Ikana, Ikana-Laela, Laela hadi Sumbawanga mjini na ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Mpanda ambao utakuwa wa kisasa kiasi cha kuwezesha kutua hadi ndege za Kimataifa.
Wakati Nape alipongeza hatua zinazoendelea katika utekelezwaji wa miradi hiyo, lakini alikerwa na ule wa ujenzi wa Zahanati ambao alikuta unafanyika nje ya kijiji ambako ni mbali na makazi ya wananchi wa Kata ya Maji Moto na pia kujengwa eneo yoevu.
Kufuatia kero hiyo, Nape aliagiza kusimama mara moja ujenzi huo na kuhamishiwa eneo lililopo karibu na wananchi na pia kumtaka mhandisi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda kuwajibika kusimamia ujenzi huo badala ya kukaa ofisini. Ziara hiyo ilimalizika jana

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages