Breaking News

Your Ad Spot

Jul 21, 2011

NCHI WANACHAMA WA UMOJA WA MATAIFA WAPINGA BARAZA KUU LA USALAMA KUPEWA DHAMANA YA KURATIBU NA ATHARI ZA MABADILIKO YA TABIA NCHI (1)

Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa,lilipokutana
kujadili athari za mabadiliko ya tabia nchi na
tishio lake kwa  amani na usalama wa kimataifa
Na Mwandishi Maalum, New York
Wakati tishio la mabadiliko ya tabia nchi likiwa Dhahiri kwa hatima ya  mataifa mbalimbali  yakiwamo  yale ambayo ni visiwa. Nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa wamepinga kwa mara nyingine, juhudi za  Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa za  kushinikiza  kupewa dhamana ya  kuratibu  athari za mabadiliko ya tabia nchi.

Kwa  siku nzima ya jumanne, Baraza hilo ambalo liko chini ya Uraisi wa Ujerumani kwa mwezi huu wa Saba,   lilikuwa na mjadala wa wazi  kuhusu   Udumishaji wa amani na usalama wa kimataifa; madhara ya  mabadiliko ya tabia nchi.

Lengo la  majadiliano   hayo  pamoja na mambo mengine,yalikuwa ni kwa Baraza  hilo kushinikiza  liwe na  uwezo wa kuratibu na  kushughulikia uwezekano wa ukosefu wa amani na usalama utakaosababishwa na madhara ya  yatokanayo na mabadiliko ya tabia nchi.

Karibu kila Balozi anayeiwakilisha nchi yake katika UM ,wakiwamo baadhi ambao nchi zao ni wajumbe wa kudumu wa Baraza la Usalama maarufu kama P5, waliochangia   majadialiano hayo, walisema  ingawa  wana kubali  ukweli kwamba madhara ya mabadiliko ya tabia nchi, yanatishia usalama na amani ya jumuia ya kimataifa, bado Baraza hilo haliwezi kuwa na  dhamana ya kulijadili , kulitolea maamuzi au maelekezo suala hilo.

Baadhi ya  hoja zilizotolewa na wazungumzaji hao ni kwamba,  ikiwa  Baraza Kuu la Usalama  litapewa dhamana hiyo.  Siyo tu  kwamba ,halina wataalam  katika eneo hilo, lakini litakuwa linaingilia majukumu, dhamana na wajibu wa vyombo  vingine vya UM  ambavyo hasa ndivyo vilivyokasimiwa  kulishughulikia  tatizo hilo. Na kusisitiza  kuwa viachwe vyombo hivyo vifanye kazi yake

Majadiliano hayo yalifunguliwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, ambaye pamoja na kuwasilisha taarifa yake  kuhusu mabadiliko ya tabia nchi, lakini pia alisema, athari za mabadiliko hayo zipo wazi kabisa na wala hazina mjadala.

Hata hivyo akasema,  yeye anadhani  kutokana na tishio la kiusalama,  na ustawi wa maendeleo  na uhai wa mataifa mbalimbali na watu wake. Baraza  Kuu la Usalama,  linapashwa pia kupewa dhamana ya  kuratibu  athari za mabadiliko ya tabia nchi.

Akichangia majadiliano hayo, mwakilishi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika UM, Balozi Ombeni Sefue, alisema , Serikali ya  Tanzania  inatambua kwamba kuna  kipengele  cha usalama katika mabadiliko ya tabia nchi,  kipengele ambacho  pia kiko   karibu katika kila  jambo   katika dunia hii.

  Hata hivyo hatujayaleta hayo mengine   kujadiliwa katika Baraza Kuu la Usalama la UM kama tunavyotaka kufanya kwa hili. Ujumbe wangu unaamini kwamba,  mabadiliko ya tabia nchi yanashughulikiwa kwa ukamilifu na vyombo vya msingi vya   UM. Vyombo ambayo  vimepewa dhamana  ya kushughulikia  suala la Maendeleo Endelevu ” akasema Balozi  Sefue.

Na kuongeza. “Mwaka 2007 tulikuwa na majadiliano kama haya, na  maoni ya wajumbe wengi waliochangia majadiliano yale yalikuwa,  Baraza  la Usalama lijiepushe kuingilia dhamana za taasisi nyingine za UM kama vile  Mfumo wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu mabadiliko ya tabia nchi (UNFCCC ) na  Baraza la Uchumi na Mandeleo ya Jamii  ( ECOSOC).

Aidha Balozi Sefue amasema,  Tanzania kama ilivyo kwa mataifa mengine inatambua ukubwa wa athari za mabadiliko ya tabia  nchi kwa   visiwa  vilivyoko katika  bahari ya Pasifiki.

Lakini akasema ,  tishio la kutoweka  kwa nchi hizo, tishio ambalo pia linaweza kuzalisha wakimbizi ,haliko kwa visiwa hivyo tu. Bali ni tishio hata kwa Tanzania n ambayo nayo ina visiwa   ambavyo  vimo hatarini  kutoweka.

Kwa hiyo akasema , ndiyo maana Tanzania imekuwa ikisisitiza na kusimamia kwamba  majadiliano kuhusu tatizo la mabadiliko ya tabia nchi na athari zake lijadiliwe zaidi katika ngazi ya  kimataifa kupitia  Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa  ili kupata  ufumbuzi wa kudumu.

Akasisitiza kuwa, kwa kutenga tatizo la mabadiliko ya tabia nchi na kuliingiza katika Baraza Kuu la Usalama, kunaweza kufifisha jitihada zote  ambazo zimekwisha kufanyika na hivyo kutokamilisha majadiliano  yanayo simamiwa na  UNFCCC.

Halikadhalika , mwakilishi huyo wa Tanzania  amerejea wito uliotolewa na wajumbe wengine wa kutaka nchi maskini kama Tanzania  na zile ambazo zimo katika hatari kubwa ya kutoweka, na  zile ambazo zimeonyesha nia thabiti ya  kudhibiti hewa ukaa na uhifadhi wa  mazingira kwa kupanda miti ya ziada. Zisaidiwe kwa hali na mali na mataifa  yaliyoendelea ambayo hasa ndiyo  chanzo kikubwa cha mabadiliko ya tabia nchi.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages