Breaking News

Your Ad Spot

Oct 6, 2011

TANZANIA NA PHILIPPINES KUANDAA MKUTANO WA KILELE KUHUSU WATU WENYE ULEMAVU

Na Mwandishi Maalum
New York
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya  Jamhuri ya Philippines zitaanda mkutano wa kilele wa wakuu wa nchi na serikali  utakaojadili  haki na fursa za watu wenye ulemavu .
Hayo yameelezwa na Balozi wa  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa mataifa, Ombeni Sefue, wakati alipokuwa  akizungumza  katika  mkutano wa   Kamati ya Tatu ya Baraza Kuu la 66 la Umoja wa Mataifa.
Kamati ya Tatu ni kati ya Kamati Sita za Baraza  Kuu la Umoja wa Mataifa. Na ni kamati inayohusika  pamoja na mambo mengine masuala yote  yanayohusu  maendeleo na ustawi wa jamii,  misaada ya kibinadamu, wakimbizi, haki za binadamu, haki za makundi mbalimbali wakiwamo wanawake, watoto, na wazee.
Balozi Ombeni Sefue, Tanzania inaamini kwamba kuna uhusiano mkubwa kati ya  umaskini na ulemavu na ndiyo maana imekubali kuandaa mkutano kwa kushirikiana na Philippines. Mkutano huo unatarajiwa kufanyika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, mwezi Septemba  2012.
Amefafanua kwa  kueleza kwamba, ili watu wenye ulemavu waweze kuondokana na umaskini kama ilivyo kwa makundi mengine ya jamii. Jumuia ya kimataifa inatakiwa kuweka mikakati ya makusudi ya kulisaidia kundi hilo.
“Nchi yangu kwa kushirikiana na Philippines  tutaanda mkutano wakilele wa wakuu wa nchi na serikali kuhusu watu wenye ulemavu, naomba kutumia fursa hii kuwaomba mtuunge mkono kwa kuridhia azimio tunalolianda kuhusu walemavu na mkutano tutakouandaa.  akasema Balozi.
Tayari nchi hizo mbili zimeanza maandalizi ya rasimu ya azimio la   watu wenye ulemavu.
Mwaka jana (2010)  Tanzania na Philippines  zilishirikiana kuanda azimio kuhusu watu wenye ulemavu. Ni kutokana na azimio hilo,  masuala ya watu wenye ulemavu yameeingizwa katika  taarifa ya mkutano wa kilele uliofanyika mwaka huo kuhusu  utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia ( MDGs).
Akizungumzia juhudi na mikakati ya Tanzania katika kuwasaidia watu wenye ulemavu pamoja na wale wanaoishi katika mazingira magumu. Balozi amesema serikali imeandaa na inatekeleza sera mbalimbali zinazolenga kupunguza makali ya maisha  kwa  makundi hayo.
Amezitaja  sera hizo kuwa ni pamoja na sera ya  hifadhi ya jamii, sera ya wazee  na mkakati wa  kukuza uchumi na kupunguza umaskini wa mwaka 2010.
Wakati huo huo, Tanzania imesisitiza kwamba kilimo kinabaki kama chanzo muhumu  cha ajira na hasa kwa nchi kama Tanzania  ambayo watu wengi wanaishi vijijini na kutegemea kilimo.
Na kutokana ukweli huo, Balozi Sefue amesema maendeleo ya  vijijini na uzalishaji wa kilimo ni muhimu sana katika kuleta maendeleo ya jamii na kupunguza umaskini pamoja na kuchagiza utekelezaji wa malengo ya maendeleo ya millennia.
“Maendeleo ya  sekta ya kilimo ni muhimu mno kwa Tanzania katika kutoa ajira na kukabiliana na umaskini”. Amesisitiza.
Akasema katika kutilia mkazo kilimo, serikali  imeandaa  mpango unaojulikana kama kilimo kwanza, ukiwa na lengo la, pamoja na mambo mengine,  kukifanya kilimo kiwe cha  kisasa , kuboresha uzalishaji, utafutaji wa masoko na kushughulikia kwa kina matatizo yanayokwamisha kilimo.
Aidha akasema kuwa  mpango huo unawashirikisha wadau mbalimbali katika ngizi zote za serikali,mashirika ya kiraia,mashirika ya kilimo na sekta binafsi.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages