Breaking News

Your Ad Spot

Nov 28, 2011

KATIBA MPYA : RAIS KIKWETE AKUTANA NA VIONGOZI WA CHADEMA

THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

Telephone: 255-22-2114512, 2116539

Fax: 255-22-2113425



PRESIDENT’S OFFICE,
      THE STATE HOUSE,
       P.O. BOX 9120,  
DAR ES SALAAM.
Tanzania.
 
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na ujumbe wa Serikali yake, Jumapili, Novemba 27, 2011, amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam, yamefanyika katika mazingira ya urafiki na ujumbe wa CHADEMA umewasilisha mapendekezo yake kuhusu mchakato wa kuandika Katiba Mpya ya Tanzania.  Serikali imepokea mapendekezo hayo.

Hata hivyo, pande zote mbili zimekubaliana kukutana tena asubuhi ya kesho, Jumatatu, Novemba 28, 2011, ili kuipa nafasi Serikali iweze kutafakari mapendekezo hayo.

Lakini pande hizo mbili zimekubaliana kuwa Katiba ya sasa ni Katiba nzuri iliyolilea Taifa kwa miaka 50 iliyopita kwa sababu ni Katiba ya sasa iliyoliwezesha Taifa la Tanzania kuwa na amani,  utulivu na kupata maendeleo makubwa ambayo nchi yetu imepata mpaka sasa.

Pia pande zote mbili zimekubaliana kuhusu umuhimu wa kutunga Katiba Mpya kama Mheshimiwa Rais Kikwete alivyoliahidi taifa wakati wa salamu zake za mwaka mpya Desemba 31, mwaka jana, 2010, Katiba ambayo italiongoza Taifa la Tanzania kwa miaka mingine 50 ijayo.

Katika mazungumzo hayo, Mheshimiwa Rais aliwahakikishia wajumbe hao wa CHADEMA wakiongozwa na Mwenyekiti wa chama hicho, Mheshimiwa Freeman Mbowe kuwa ni dhamira yake na ya Serikali yake kuhakikisha kuwa Tanzania inapata Katiba mpya.

Katika mkutano huo, pande zote mbili zimekubaliana kuwa ni jambo muhimu sana kwa mchakato mzima wa kutungwa kwa Katiba Mpya kuendeshwa kwa namna ya kulinda na kudumisha tunu za taifa za amani, utulivu na umoja wa kitaifa.

Aidha, pande zote mbili zimekubaliana kuwa mchakato huo uendeshwe kwa kuzingatia misingi ya mambo mengine muhimu kwa taifa la Tanzania kama vile kujiepusha na vitendo vya uvunjifu wa amani, kuligawa Taifa kwa misingi ya udini na ukabila ama kutugawa kwa misingi ya maeneo.  

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.

27 Novemba, 2011


No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages