Breaking News

Your Ad Spot

Nov 30, 2011

MIGIRO ATAKA WABUNGE WAWAJIBIKE KWA WANANCHI

Na Mwandishi Maalum, New York
Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Asha-Rose Migiro amewahimiza wabunge  kuweka mbele maslahi ya wananchi wanaowawakilisha.

 Ameyasema  hayo jana Jumatatu, wakati alipokuwa akifungua mkutano wa siku mbili unaowakutanisha  wabunge  kutoka mabunge mbalimbali duniani, ufunguzi uliomshirikisha pia Rais wa Baraza Kuu la 66 la Umoja wa Mataifa, Nassir Abdulaziz Al-Nasser.

Katika mkutano huo ambao umeandaliwa na Umoja wa Mataifa na  Muungano wa Mabunge ( IPU),Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linawakilishwa   na wabunge wawili, Mhe. John M. Cheyo na Mhe. Betty Machangu.

“ Mkiwa ni  wabunge  kazi yenu si kupitisha sheria tu na kusimamia utendaji wa serikali. Bali mnatakiwa kuwajibika kisiasa kwa kuwasikiliza wananchi na kuelezea matakwa yao”, Akasisitiza Migiro.

Naibu Katibu Mkuu amewaambia wabunge hao, wakiwamo pia baadhi ya maspika , kwamba, uwajibikaji wa kisiasa na utawala wa kidemokrasia haviwezi kutengenishwa kwa kuwa vyote ni muhimu katika kuchagiza  maendeleo ya binadamu,  haki na amani.

“ uwajibikaji wa kisiasa ni muhimu sana katika kukabiliana na changamoto zinazoikabili dunia hivi sasa.  Baadhi ya Changamato  hizo ni  pamoja na   umaskini,  vurugu, na uhalifu wa kupangwa mambo ambayo yanashamiri  katika nchi ambazo hakuna uwajibikaji” akabainisha Migiro.

Akasema kuwa  taarifa ya Bank ya  Dunia imeonesha kuwa  vita vya wenyewe kwa wenyewe,  makosa ya jinai, vurugu na hata ugaidi na  uhalifu wa kupangwa ni mambo yanayoota mizizi na kukua   katika nchi ambazo ama utawala wa sheria ni dhaifu au taasisi zake zimeghubikwa na  ufisadi.

Hata hivyo Migiro amewaeleza wabunge hao kwamba hakuhitajiki   utafiti  kama huo ulioofanywa na  Bank ya Dunia,kufahamu kwamba  kuongezeka   kwa vitendo vya halifu kunasababishwa na  serikali kandamizi.

Akatoa mfano kwa kutaja vunguvungu la kisiasa linaloendelea  hivi sasa  Mashariki ya Kati maarufu kama Arab Spring, ambako anasema vuguvugu hilo limeamsha hamasa  hususani kwa vijana, hamasa ya kutaka kuwepo na serikali za kidemokrasia, zinazowajibika na zenye kuheshimu misingi ya haki za  binadamu.

Akasema anafahamu vema changamoto wanazokabiliana nazo wabunge kwa sababu hata yeye aliwahi kuwa mbunge.

Hata hivyo akasema  yapo mambo kadhaa ambayo wabunge kwa kushirikiana na serikali zao yanaweza  saidia kuzuia au kupunguza mitafaruku ya kisiasa na  vitendo vya  uhalifu. 

Ameyataja mambo hayo kuwa ni pamoja na kujenga mazoea ya uwajibikaji, kufanya uchanguzi wa mara kwa mara na unaozingatia utawala wa sheria, uhuru wa vyombo vya habari na uhuru wa kukusanyika na kutoa mawazo na kuongeza idadi ya wanawake mabungeni.

“ Lakini uwajibikaji unakwenda mbali zaidi ya hapo” anasema Migiro. “ Ni kwa kuhakikisha  ushiriki wa  wananchi  na hasa vijana katika mambo ya  siku hadi siku, kwa kutimiza hayo na mambo  mengine wabunge mnaweza kujenga daraja imara kati ya wananchi na serikali zao” akasisitiza Migiro.

Aidha  Migiro ameyataka mabunge yote   duniani yawajibike katika kuzuia vitendo  vya rushwa.

Ajenda  muhimu zinazojadiliwa  na wabunge hao  katika  mkutano huo wa siku mbili ni    pamoja na, uhusiano kati  ya Umoja wa Mataifa na Mabunge , nafasi ya Umoja wa Mataifa katika kusimamia na kuimarisha dhana  ya uwajibikaji, na     fursa na changamoto  zinazowakabili vijana katika ushiriki wao katika demokrasia.

Nyingine ni  uwajibikaji katika usimamizi wa fedha za umma na uimarishaji wa  uhusiano kati ya taasisi za kitaifa na asasi zisizo za kuserikali  ili kujenga jamii yenye uwazi.

Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Asha-Rose Migiro akifungua siku ya jumatatu mkutano wa siku mbili wa wabunge kutoka mabunge mbalimbali duniani mkutano huo unafanyika makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York, kushoto kwake ni Rais wa Baraza Kuu la 66 la Umoja wa Mataifa, Bw. Nassir Abdulazizi Al-Nasser na kulia ni Katibu Mkuu wa IPU Bw. Anders B. Johson.

 
Naibu Katibu Mkuu Asha-Rose Migiro akibadilishana mawazo na  Waheshimiwa  Wabunge John M. Cheyo na Betty Machunge wakati alipowakaribisha Ofisini kwake Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa.Wabunge hao wapo hapa wakihudhuria mkutano wa wabunge  ambao Naibu Katibu Mkuu aliufungua. Wabunge hao wanaliwakilisha Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mkutano huo .

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages