Breaking News

Your Ad Spot

Nov 30, 2011

MAANDAMANO, FUJO NA VURUGU HAVIWEZI KUZALISHA AJIRA-CHEYO

                                                                                       Na Mwandishi Maalum, New York
Maandamano  yasiyokuwa na ukomo na yasiyozingatia utawala wa sheria, vurugu na fujo  zinazofanywa na vijana kwa kisingizo cha kutaka fursa sawa na uwajibikaji, hayawezi kujenga  mazingira ya uzalishaji wa ajira.

Kauli hiyo imetolewa na Mhe. John M. Cheyo  mbunge wa Bariadi Mashariki na mwenyekiti wa  UDP,  wakati alipokuwa akichangia majadiliano kuhusu    fursa na changamoto   za ushiriki wa vijana katika  demokrasia.

Mhe. Cheyo ni kati ya wabunge wawili wanaouhudhuria mkutano wa siku mbili unaoshirikisha  wabunge kutoka mabunge mbalimbali duniani, mkutano huo unafanyika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, ukiwa umeandaliwa na UN kwa kushirikiana na Chama cha Mabunge ( IPU). Mbunge mwingine kutoka Tanzania anayeshiriki mkutano huo ni Mhe. Betty Machunge

 Akafafanua zaidi  kwa kusema ingawa vijana  wanadai  uwajibikaji zaidi kutoka serikali zao pamoja na fursa za ajira, lakini ajira na fursa hizo haziwezi kupatikana katika mazingira ambayo yametawaliwa na vurugu na maandamano yasiyokuwa na kikomo.

“ Ni kweli wanayo haki ya kudai fursa sawa za kushiriki katika demokrasia na kupata ajira, lakini pia wanatakiwa kukumbuka kwamba wanaowajibu pia wa  kufuata utawala wa sheria na taratibu zilizopo katika kuwasilisha madai yao, kinyume na hapo wanachokifanya si demokrasia” akasititiza  Cheyo.

 Akizungumzia  ushiriki wa vijana katika siasa, Bw. Cheyo amesema bila ya kubadili mifumo ya uchaguzi   ikiwa ni pamoja na kuweka mikakati ya makusudi  itakayoongeza idadi ya vijana mabungeni. Vijana wengi hususani  Barani Afrika watabaki kuwa wasindikizaji badala ya kuwa washiriki .

Akasema kuwa vurugu nyingi na maandamano yasiyokwisha na  yanayoendelea sehemu mbalimbali duniani na yakiwahusisha zaidi vijana,  yanatokana na sababu nyingi lakini kubwa ni kunyimwa kwao fursa za kushiriki siasa.

“ Vijana wengi hivi sasa wamekata tamaa na wamechoka kuendelea kuwa vipandio vya watu wengine kujipatia nafasi za uongozi wa kisiasa. Kama kweli tunataka na wao washiriki kikamilifu katika siasa  basi tunatakiwa kubadili mifumo yetu ya uchanguzi na hasa zile chaguzi ambazo zinatanguliza mbele fedha” akasisitiza  Bw. Cheyo.

Akaongeza kuwa  kila nchi inatakiwa kuweka mikakati ya makusudi itakayohakikisha  kunakuwapo na ongezeko la wabunge vijana katika mabunge yao.

 “ sisi katika  Tanzania   tumeweza kuongeza idadi ya wanawake bungeni maradufu kwa sababu tulijiweka malengo na mikakati ya kuhakikisha kwamba idadi ya wanawake inaongezeka. Kwa utaratibu huu ambao Tanzania imeutumia tunaweza pia kuutumia kwa vijana”. Akasema Cheyo.

Akizungumzia suala zima la vijana  na changamoto zinazowakabili. Mhe. Cheyo ametahadharisha kwamba, vijana wasipopatiwa  matumaini ni sawa na  silaha ya maangamizi inayosubiri kulipuka.

Akasema wanachokifanya  vijana hivi sasa katika maeneo mbalimbali duniani kama hakitaangaliwa katika umakini wake. Kuna hatari  kubwa ya kujirudia kwa tabia  ya kuwaondoa viongozi walioko madarakani kwa njia zisizo halali. Pamoja kurejea kwa matukio kama vile  mapinduzi ya kijeshi  yaliyotawala sana katika miaka ya 70 na 80.

Wachangiaji wengine waliochangia ajenda hiyo, walisema kwamba pengine vijana si  wakulaumiwa sana bali wakulaumiwa ni  wale wanaowatumia vijana  kwa manufaa  na malengo yao.

Aidha baadhi ya wachangiaji, walitaka kuwepo na tafsiri sahihi ya nani ni kijana. Kutokana na kile kilichoelezwa kwamba kumekuwa na  tafrisi zinazochanganya ni umri gani unaoweza kutajwa kwamba ni umri halali wa kijana kushiriki siasa na hata uchaguzi.

“ tumezungumza  sana kuhusu haki na fursa za vijana, wote tunakubaliana kwamba vijana wanahasira  na wanataka mgawanyo sawa wa  raslimali. Lakini hebu tuanzie humu humu  katika ukumbi tuliomo, je kati yetu ni nani mbunge kijana? Hakuna. Nadhani tuna mengi ya kufanya”. Akasema mbunge mmoja kutoka Bunge la  Uingereza na kuwafanya washiriki wengine kuangua kicheko.

Ajenda  hiyo ambayo ilikuwa kivutio kwa wachangiaji wengi lakini pia kila mmoja akitoa maoni  tofauti, na hisia tofauti katika matumizi ya vyombo vya habari vya kijamii kama vile face book na tweeter kama eneo mbadala la mawasiliano kwa vijana.

Lakini kauli za wazungumzaji wengi  ilijidhirisha wazi kwamba kila aliyeichangia  hakusita kusema vijana wengi si katika nchi zinazoendelea  bali hata zile zilizoendelea wamechoka, wamekata tamaa  na  hawana matumaini ya  maisha yao ya baadaye.

Naye Mhe. Betty Machunge akichangia majadiliano kuhusu dhana  ya uwajibikaji, uhusiano kati ya UM na Mabunge na ushiriki wa wanawake katika siasa na demokrasia kwa ujumla. Yeye alitaka kuimarishwa  na kuwepo kwa ushirikiano wa karibu kati ya Umoja wa Mataifa na  Mabunge.

Akasema kuwa maamuzi mengi yanayofanywa na Umoja wa Mataifa  hayawafiki wabunge na kama yanawafikia basi yanachelewa mno.

Akapendekeza kuwapo na mfumo au utaratibu utakao wawezesha wabunge kupitia mabunge yao kutoa taarifa za utekelezaji wa maazimio mbalimbali ya Umoja wa Mataifa hasa yale ambayo yanatakiwa kufanyiwa kazi na wabunge.

Aisha akasema kuwa kama ushirikiano kati ya UM na wabunge utaratibiwa vizuri, utasaidia pia katika kubadilishana mawazo na mbinu mbadala za kuongeza idadi ya wanawake wabunge.

John Cheyo akibadilishana mawazo na  Bw. Oscar Fernandez-Taranco aliyewahi kuwa Mwakilishi  Mkazi wa Shirika la  Maendeleo la Umoja wa Mataifa UNDP) nchini Tanzania. muda mfupi kabla ya ufunguzi wa mkutano wa siku mbili wa wabunge kutoka mabunge mbalimbali. Bw. Taranco ambaye kwa sasa ni Msadizi wa Katibu  Mkuu wa Umoja wa Mataifa, akisimamia  Idara ya masuala ya Siasa alikuwa miongoni mwa watoa mada.Mhe. Cheyo anahudhuria mkutano huo akiliwakilisha  Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages