Breaking News

Your Ad Spot

Nov 2, 2011

UMOJA WA MATAIFA WA UTANGAZA MWAKA 2012 KUWA MWAKA WA KIMATAIFA WA VYAMA VYA USHIRIKA

Na Mwandishi Maalum
New York
Imeelezwa kwamba,  Vyama vya Ushirika, kama vikisimamiwa vizuri, vikaandaliwa sera na sheria  stahili , na vikaachwa vifanye kazi zake bila ya kuingiza siasa, ni eneo muhimu sana  linaloweza kutoa ajira kwa mamilioni ya vijana ambao wamepoteza matumaini ya kupata ajira.
Aidha  imebainishwa kwamba, kwa kupitia   Vyama hivyo vya Ushirika  ni rahisi kwa wananchi kujiletea maendeleo yao haraka na kuondokana na umaskini.
Kwa kutambua hayo Umoja wa Mataifa, umeutangaza mwaka 2012 kuwa mwaka wa Kimataifa wa  Vyama vya  Ushirika. Na kuzitaka Serikali za nchi Wanachama wa Umoja wa Mataifa,  kuvijengea vyama vya Ushirika mazingira  mazuri  yatakayoviwezesha  kukua, kustawi na  kutekeleza majukumu yake kikamilifu .
Hayo yamesemwa  na wazungumzaji tofauti akiwamo Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dk. Asha-Rose Migiro wakati wa uzinduzi wa mwaka huo,    uliofanyika   siku ya jumatatu    katika Ukumbi Mkuu wa Mikutano wa Umoja wa Mataifa,  na kuhudhuriwa pia  na watu mashuhuri   akiwamo aliyekuwa Waziri Mkuu wa Uingereza, Bw. Gordon Brown.
 Ujumbe wa mwaka wa Kimataifa wa vyama vya ushirika unasema.“Makampuni ya kibiashara ya Vyama vya Ushirika  hujenga ulimwengu bora zaidi”.
 Akizungumza wakati wa uzinduzi huo  uliotanguliwa na kongamano  lililoyojumisha  nchi wanachama wa UM, Shirika la Kazi Duniani ( ILO) na  wataalamu mbalimbali. Naibu Katibu  MKuu, Dkt.Asha- Rose Migiro amesema “Mwaka wa Kimataifa wa Vyama vya  Ushirika ni fursa ya kuongeza uelewa kwa umma kuhusu vyama hivyo, kuhimiza ukuaji wake na kuzihimiza Serikali kuanzisha sera  nzuri zitakazo weka mazingira mazuri ya ustawi wa vyama vya ushirika”.
Akasema  uzinduzi huo unafanyika katika kipindi ambacho dunia iko katika mtafaruku wa kutengana na kutoridhika kunakotokana na mwendelezo wa mdodoro wa uchumi.
Akaongeza kuwa kupitia Vyama vya Ushirika, dunia inaweza kujifunza namna ya kukabiliana na mdodoro huo kwa kuwa  vyama hivyo vimeweza kuhimili  matatizo ya uchumi kwa kuwa na mitaji na akiba kubwa.
Aidha akasema Vyama hivyo   vimetoa mchango mkubwa si tu kwa wanachama wake lakini pia katika jumuia zao na jamii inayowazunguka.
“ Vyama vya Ushirika vinauwezo mkubwa wa kupunguza umaskini, kukuza na kutoa ajira kwa  vijana, wanawake, wazee, watu wenye ulemavu na watu asilia. Ni vyama vinavyotoa mafunzo na kukuza ujuzi wa wanachama wake,    Na  ni chanzo muhimu cha usalama wa chakula na amani na usalama” akasema Migiro
Akasisitiza kwamba,  umuhimu mwingine wa Vyama vya  Ushirika unatokana na  Mshikamano wake . Kwa maana ya kwamba vyama hivyo ni imara, vinajenga uhusiano miongoni mwa wanachama wake, kuna uwajibikaji kwa wanachama  na wateja wake na vinazingatia ustawi wa wanachama wake na ustawi wa jamii nzima.
Kwa upande wake  Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza, Bw. Gordon Brown  yeye amesema   vyama vya Ushirika vinaajiri zaidi ya watu 100 milioni duniani kote,
Aidha Bw. Brown amesema kuwa taarifa mbalimbali zinaonyesha kuwa  vyama vikubwa  300 vya Ushirika vilivyoko duniani vilifaya mauzo ya dola za kimarekani 1.1 trilioni katika mwaka 2008. Hali inayoonyesha kwamba vyama hivyo vina nguvu kubwa sana kiuchumi ni  kimitaji.
Akasema kama hiyo haitoshi  Vyama hivyo vya  Ushirika ambavyo vimeenea katika nchi  mbalimbali vinahudumia wanachama zaidi ya bilioni Moja. Akasema ni  muhimu kwa jumuia ya kimataifa kuutumia mwaka huu wa kimataifa wa vyama vya Ushirika kujifunza zaidi utendaji wake pamoja na kuvisaidia kwani vina nafasi kubwa ya kukabiliana na changamoto mbalimbalili zinazoendelea  hivi sasa dunia zikiwamo za ajira kwa vijana.
Kilele cha Mwaka wa Kimataifa wa Vyama vya Ushirika  kitakuwa Desemba 31,2012.

 Washiriki wa  Kongamano lililotangulia uzinduzi wa Mwaka wa 2012 kuwa Mwaka wa Kimataifa wa Vyama vya Ushirika. Baadhi ya wazungumzaji katika kongamamo hilo  walizitaka serikali kutoingiza siasa katika utendaji kazi wa vyama vya Ushirika. wakainisha pia mafanikio mbalimbali yaliyotokana na vyama hivyo pamoja na changamoto zinazovikabili vyama hivyo.  Umoja wa Mataifa umeutaganza mwaka 2012 kuwa mwaka wa Vyama vya Ushirika kwa kutambua mchango wake katika  utoaji wa ajira, kukuza uchumi na kuleta maendeleo endelevu, kupiga vita umaskini, kuchangia utekelezaji wa  malengo ya maendeleo ya millenia pamoja na hifadhi salama ya chakula.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages