Breaking News

Your Ad Spot

Nov 24, 2011

VIJANA WA KIUME SEMENI HAPANA DHIDI YA UKATILI WA WANAWAKE-BAN KI MOON

Balozi Sefue kaimpongeza Kihongosi
Na Mwandishi Maalum
New York
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki  Moon  amewataka vijana wa kiume kushiriki kikamilifu katika kupinga  na kutokomeza  ukatili dhidi ya wanawake.
Ban Ki  Moon ametoa wito huo wakati wa maadhimisho ya   siku ya  Kimataifa ya kukomesha ukatili  dhidi ya wanawake, maadhimisho ambayo hufanyika kila  Novemba 23.
Katika maadhimisho hayo yaliyofanyika   siku ya jumatano, hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa,  Katibu Mkuu, licha ya kusisitiza haja na umuhimu wa vijana wa kiume  kuwa mstari wa mbele kupinga ukatili dhidi ya wanawake.Lakini pia alitoa tuzo kwa vijana  sita  kutoka mabara sita  walioshinda ubunifu wa   fulana( T- Shirts)   zenye nembo maalum  ya kampeni dhidi ya unyanyasaji wa wanawake.
Miongoni mwa washindi hao, yuko kijana wa Kitanzania,  Mwasapi Kihongosi ambaye  pia ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam aliyekuwa mshindi wa kwanza  Barani  Afrika . maadhimisho hayo  yalihudhuliwa na Mkurugenzi Mkuu wa  chombo maalum cha Umoja wa Mataifa kinachoshughulikia masuala ya wanawake- UN WOMEN Michelle Bachelet na viongozi mbalimbali wakiwamo mabalozi.
“ Ninapenda kuwapongeza sana vijana   hawa sita ,ambao wameshinda tuzo ya ubunifu wa fulana   zenye nembo na ujumbe maalum.  Wito wangu kwenu na kwa vijana wote wa kiume ni  huu,  unganeni kukomesha unyanyasaji dhidi ya wanawake. Na nimefurahi kuona wengi wenu ( wageni waalikwa) mmevaa  fulana walizobuni vijana hawa ” akasema Ban Ki Moon.
Akasema kuwa kauli mbiu ya mwaka huu  ya siku ya kimataifa ya kukomesha ukatili  dhidi ya wanawake ni “ Uongozi wa vijana”. 
Akaongeza kuwa yeye binafsi  kila  anaposafiri   hujaribu kukutana na kuwasilikiza vijana, kwa sababu vijana  kwa kupitia hisia  na nguvu zao  wanaouwezo mkubwa wa kuifanya dunia yetu  kuwa mahali pazuri.
Ban ki Moon amesisitiza kwamba kwa kupitia vijana hao sita waliobuni na kushinda mpango wa kimataifa wa  kutengeneza nembo na fulana kwaajili ya kampeni  ya  ukatili dhidi ya wanawake , kila mtu na hasa vijana anatakiwa kusema “ Hapana” kwa  unyanyasaji dhidi ya wanawake na wasichana.
Akizungumzia zaidi kuhusu ukatili dhidi ya wanawake, Katibu Mkuu wa UM  amesema . “ wote tunaelewa kwamba  unyanyasaji dhidi ya wanawake na wasichana  uko wa  aina nyingi, unyanyasaji huu ambao uko katika nchi zilizoendelea na zinazoendelea ni pamoja na  ubakaji, tohara,  ukatili wa majumbani, ubaguzi katika mashule,  unyanyasaji wa wanawake katika maeneo ya kazi na ukatili wa kijinsia katika maeneo yenye vita”.
Akaongeza kwamba kundelea kuwapo kwa vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake siyo tu   kwamba ni jambo lisilokubalika lakini pia  ni kikwazo kikubwa katika kufikia  usawa kamili wa kijinsia.
Akazitaka serikali na washirika wote duniani, na uongozi wa vijana  kuunganisha nvugu zao na mawazo  yao  kukomesha gonjwa hilo la ukatili dhidi ya wanawake. Na kwa kufanya hivyo ulimwengu utakuwa  mahali  pa haki, amani na usawa.
Kwa Upande wake Mkurugenzi Mkuu wa UN-Women  Michelle Bachelet amesema ingawa nchi nyingi zimetunga sheria dhidi ya  vitendo vya ukatili kwa wanawake, bado kunahitaji uwajibikaji na utashi wa kisiasa kutoka kwa viongozi na wananchi kwa ujumula katika kulikabili tatioz hilo
Akaainisha masuala  kumi na sita  ambayo anadhani kama yakitekelezwa yanaweza kusaidi  kama si kupunguza  basi kumaliza kabisa ukatili huo. Akayataja mambo  hayo  kuwa  ni pamoja na  kuwa na sera madhubuti za kumaliza  ukatili dhidi ya wanawake,  utoaji wa huduma za dharura kwa waathirika,  kuwashirikisha wanaume na vijana wa kiume na kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria watuhumiwa wa ukatili dhidi ya wanawake.
Vijana hao sita kila mmoja wao sasa anakuwa Balozi maalum katika  kampeni zitakazozinduliwa mwakani  kuhusu ukatili dhidi ya wanawake. Kwa  upande wa  Afrika kampeni hizo zinatarajiwa  kuzinduliwa   mapema mwakani   kwa washiriki    kupanda mlima Kilimanjaro kupinga ukatili dhidi ya wanawake na wasichana.
mwisho


No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages