Breaking News

Your Ad Spot

Mar 27, 2012

BARAZA KUU LA USALAMA LA LAANI MAPINDUZI YA KIJESHI NCHI MALI


Na Mwandishi Maalum
New York
Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa  Mataifa, limelaani vikali mapinduzi ya kijeshi yaliyofanywa na askari wa chache dhidi ya serikali ya kidemokrasia nchini Mali. Na limewataka wanajeshi hao kuachana na vitendo vya kihalifu na fujo na kurejea katika makambi yao.

 Taarifa  iliyotolewa na  Rais wa Baraza hilo kwa mwezi huu wa Marchi  Balozi wa  Uingereza Bw. Mark Lyall Grant (pichani) amesema. “  Baraza la Usalama linalaani mapinduzi hayo na linawataka wanajeshi kurudi katika makambi yao na  linatoa wito  wa kurejeshwa kwa  utaratibu wa Katiba  na kufanyika kwa uchaguzi kama  ilivyokuwa imepangwa.

Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa lilikutana siku ya jumatatu ambapo lilijadili kuhusu kuzorota kwa hali ya kibinadamu katika Kanda ya Afrika ya Sahel, ambapo lilisema kwamba kuongezeka kwa makundi  yenye silaha na magaidi pamoja na kuzagaa kwa silaha kumeongeza hali ya wasiwasi katika kanda hiyo.

 Wiki iliyopita baadhi ya wanajeshi wa nchi  Mali  wakiongozwa  Kapteni Amadou Haya Sanogo walitangaza kuipindua serikali ya Rais Amadou Toumani Toure ambaye mpaka sasa hajulikano aliko.

Katika mkutano huo ambao uliwahusisha wajumbe 15 wanaounda Baraza   Kuu la Usalama,  Baraza hilo pia limelaani vitendo vinavyofanywa na baadhi ya makundi ya waasi ya kuvivamia vikosi vya serikali na kuwataka waasi hao kusitisha  aina zote za vurugu na kutafuta  ufumbuzi wa amani kwa njia ya mazungumzo ya kisiasa. Aidha   Baraza hilo  limesisitiza haja ya  kuzingatia na kuheshimu uhuru, umoja na mipaka ya nchi.

Tayari Umoja wa Afrika ( AU) umekwisha kutanga kutoyatambua mapinduzi hayo, huku  baadhi ya nchi  ikiwamo  Marekani  ikitangaza  kusudio la kusitisha misaada   kw anchi hiyo , nchi  ambayo uchumi wake kwa asilimia kubwa  unategemea sana misaada kutoka nchi wahisani.

Kuhusu hali tete ya kanda ya Sahel, Baraza limebainisha kuwa hali ya ukame , uhaba wa chakula na kurudi kwa  maelfu ya watu kutoka Libya kumeongeza hali ugumu wa maisha kwa watu wa eneo hilo. Hali ambayo imesababisha  maelfu ya   wananchi wa eneo hilo kukimbilia  katika nchi za jirani kutafuta hali bora ya maisha.

Kutokana na hali hiyo, Baraza  Kuu la  Usalama la Umoja wa Mataifa,  limetoa wito kwa  mamlaka za kitaifa na kimataifa, kikanda na masharika ya  misaada ya  kibinadamu  kuchukua hatua za haraka kuimarisha juhudi za kuwasaidia wananchi wa eneo hilo.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages