Breaking News

Your Ad Spot

Apr 28, 2012

TANZANIA YAOMBWA KUCHANGIA WAANGALIZI WA AMANI SYRIA


Baadhi ya walinzi wa amani wa UN walioko Syria wakizungukwa na wananchi 
Na Mwandishi Maalum,
New York
Mkuu Idara ya   Operesheni za Ulinzi wa Amani za Umoja wa Mataifa (DPKO) , Balozi Herve Ladsous, ameziomba nchi ambazo zimepelekewa maombi ya kutoa waangalizi wa amani  kwenda kuhudumu nchini Syria, kutoa waangalizi hao haraka na mapema iwezekanavyo.
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni  kati ya mataifa  ambayo yameombwa kutoa wanajeshi wake.
 Balozi Ladsous ametoa wito huo   siku ya ijumaa wiki hii, wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na wawakilishi  wa nchi ambazo zinashiriki katika Operesheni za ulinzi wa   kulinda amani za UN  maarufu kama TCC.
Ombi la  Balozi Ladsous kwa nchi hizo  linakuja ikiwa ni takribani wiki moja tangu Baraza Kuu la Usalama kupitisha Azimio namba 2043 ( 2012)  linalotakamka pamoja na mambo mengine,  kuanzishwa kwa Misheni  ya Umoja wa Mataifa ya kusimamia amani Syria ( UNSMIS) itakayokuwa na waangalizi 300 wanaotakiwa kupelekwa nchi humo ndani ya kipindi cha siku 90 tangu kupitishwa kwa Azimio hilo.
 “ Ninawaomba sana  sana, tafadhali fanyeni hima, kutupatia waangalizi wa amani, wasilianeni na  Makao  Makuu ya Nchi zenu. Hatuna  muda na dunia inatuangalia”. Akasisitiza na kusihi   ombai alilokuwa akirudia mara kwa mara ,Mkuu huyo wa DPKO  aliyekuwa ameandama na maafisa waandamizi kutoka  Idara hiyo.
Kwa mujibu wa  Bw.  Herve Ladsous   ili   Azimio hilo liweze kutekelezwa kikamilifu,  waangalizi   wa amani 100 wanatakiwa  wawe wamewasili nchini Syria ndani ya siku 30 na idadi    itakayobakia  ya  waangalizi 200 iwe imekamilika  ndani ya siku 60.
Akasema kwamba ili malengo hayo yaweze kufikiwa  kama ilivyopangwa, ni vema na muhimu nchi zilizoombwa  zikawasilisha majina ya wanajeshi wanaowapendekeza  haraka na mapema iwezekanavyo ili taratibu za maandalizi ya kuwapeleka Syria  yaweze kutekelezwa.
Akifafanua zaidi kuhusu majukumu ya  waangalizi hao, ambao hawatakuwa na silaha  za aina yoyote ile ,  kuwa jukumu  lao kuu la  msingi litakuwa ni   kufuatilia na  kusimamia  kwa ukamilifu utekelezaji wa  ajenda Sita za mpango wa amani kama zilivyoainishwa      na  Mjumbe Maalum wa Umoja wa Mataifa na Muungano wa  Nchi za Kiarabu, Bw. Kofi Annan.
Mapendekezo  hayo yanataka pande zote husika nchini humo kusitisha mapigano na vitendo vyovyote  vya uvunjifu wa amani,  kuondoa wanajeshi na  silaha katika makazi ya watu, kuruhusu mashirika ya misaada ya kibinadamu na hatimaye kuruhusu   kuanza  mchakato wa mazungumzo ya amani yatakayozingatia matakwa ya  watu wa Syria.
            Akabainisha kwamba waangalizi hao wa amani  300 watasambazwa katika maeneo 25 ambayo yameainishwa kama  maeneo tete  yanayohitaji uwepo wa maafisa hao.
            Hadi kufikia siku ya  ijumaa  wiki hii kulikuwa na waangalizi wa amani wapatao 14  ambao wapo  tayari  nchini Syria  kwa lengo la kusimamia mchakato huo wa  usitishswaji wa mapigano  na uondoaji wa silaha katika  makazi ya watu na pia kutoa taarifa ya kile kinachoendelea.
Hata hivyo idadi hiyo ya waangalizi hao imekuwa ikilalamikiwa na wananchi wa Syria kwamba haitoshi ikilinganishwa na ukubwa wat atizo.
Wakati huo huo katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, ametangaza uteuzi wa Meja Jenerali  Robert Mood raia  wa  Norway kuwa Mkuu wa  Misheni   ya Usimamizi  ya Umoja wa Mataifa nchini Syria (UNSMIS)

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages