Breaking News

Your Ad Spot

Jul 12, 2012

TANZANIA YATOA MAONI YAKE MKATABA WA BIASHARA YA SILAHA


Na Mwandishi Maalum, New York
Wakati majadiliano  kuhusu uanzishwaji wa mkataba wa kisheria  utakaoratibu na kudhibiti biashara ya silaha duniani yakiendelea, Tanzania  imesema, inashiriki majadiliano hayo si kwa sababu inazalisha au kusambaza silaha bali ni mazingira  inayozungukwa nayo.
“Tunashiriki madiliano haya muhimu si kwa sababu tunazalisha silaha au kusambaza silaha, tunashiriki kwa sababu tumezungukwa na majirani ambao ama wamo katika migogoro ya wenyewe kwa wenyewe au migogoro kati ya nchi moja na nyingine”.
Msimamo huo umetolewa siku ya jumanne na  Kaimu Balozi wa Ubalozi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Dkt. Justin Seruhere wakati alipokuwa  akichangia majadiliano ya jumla kuhusu uanzishwaji wa mkataba wa kisheria wa biashara ya silaha duniani.
Kaimu Balozi  Seruhere  anaongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo akishirikiana na  Brigedia Jenerali Dkt. Charles Muzanila kutoka  Jeshi la Wananchi wa Tanzania ( JWTZ)
Mkutano huu unaohusu majadiliano kuhusu mkataba wa biashara ya silaha duniani,  ni   mkutano muhimu na nyeti kwa mustakabali suala zima la ulinzi na usalama na hususani katika eneo la    uagizaji, usambazaji,  na matumizi ya silaha ndogo ndogo na nyepesi.
Ni  majadiliano yanayovuta hisia  na kugusa maslahi ya watu wengi, na  ni mkataba ambao  vilivile  kama hautajadaliwa vema na kuzingatia maslahi na matakwa ya nchi nyingi hasa zinazoendelea  unaweza kwa namna moja ama nyingine kuingilia  uwezo na uhuru wa mataifa kujilinda na kulinda mipaka   yake.
“ Kwa muda mrefu Tanzania imekuwa mwenyeji wa kuhifadhi wakimbizi wanaokimbia machafuko katika nchi zao. Lakini pia tumekuwa tukishuhudia usafirishaji wa silaha haramu kupitia mipaka yetu.  Hali hii inatishia  misingi  ambayo tumejiweka , misingi  ambayo ni amani , ulinzi na usalama” akasisitiza Dkt. Seruhere.
Na kwa sababu hiyo, Tanzania inasisitiza kwamba  kuanzishwa kwa mkataba huo kutasaidia sana katika kuthibiti usambazaji na matumizi haramu ya silaha  hizo , silaha ambazo zimekuwa zikipoteza maisha ya mamilioni ya  watu  wasio na hatia.
Hata hiyo, Tanzania  imebainisha na kueleza wazi kwamba ingawa inaamini katika kuwapo kwa mkataba huo, lakini kamwe mkataba  huo  usiingilie haki ya  mataifa kujilinda na kulinda mipaka yake.
“ Tunaposhiriki majadiliano haya,   lengo letu ni moja  tu kwamba tutatoka na mkataba  wa kisheria ambao utazingatia  viwango vya kimataifa katika kuagiza, kusafirisha au  kuhamisha  silaha ndogo ndogo na nyepesi. Lakini  tunaamini kwamba haki ya nchi kujilinda itabaki kuwa msingi mkuu wa mkataba huu. Kwa maneno mengine mkataba usiingilie na kuzuia  bali kudhibiti”.  Akasisitiza
Aidha Tanzania imesisitiza kwamba utengenezaji  wa silaha kwa madhumuni ya kujilinda isiwe sehemu ya mkataba huo.
Karibu  kila nchi ambayo imezungumza katika mkutano huu zimejaribu kutoa mwelekeo wa nini  inataka kiingizwe au kisiingizwe katika mkataba huo.
Baadhi zimeeleza umuhimu wa kuzingatia uwazi na ukweli  wakati wa majadiliano haya, huku wakibainisha kwamba kwa namna yoyote ile mkataba huo  usilenge katika kuzipendelea nchi chache.
Wengine wanataka mkataba uandikiwe katika lugha nyepesi na inayoeleweka na ufafanue na kuweka wazi madhumuni na malengo halisi ya mkataba huo.
Wazungumzaji wengine wamesisitiza umuhimu wa kuhakikisha kwamba mkataba unakuwa   katika hali itakayopelekea nchi nyingi kuuridhia mara utakapoandaliwa. Na kuongeza kwamba  litakuwa kama jambo jema  kama mkataba huo utapitishwa  na nchi zote bila ya kupigiwa kura.
 Mkutano huu wa mwezi mmoja unafanyika hapa  Makao makuu ya Umoja wa Mataifa, na mchakato wa majadiliano ya kuanzishwa kwa mkataba huu umeanza miaka sita iliyopita.                              

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages