Breaking News

Your Ad Spot

Oct 10, 2012

KUNA UHUSIANO WA KARIBU KATI YA UMASKINI NA ULEMAVU

Balozi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika  Umoja wa Mataifa, Tuvako  Manongi akichangia majadiliano ya  ajenda namba 27 kuhusu Maendeleo ya Jamii,  Kamati ya Tatu ambayo ni Moja ya  Kamati sita zinazounda Baraza Kuu la 67 la Umoja wa  Mataifa na kama ilivyo kwa kamati nyingine imeanza majadiliano ya kubadilishana mawazo kuhusu suala zima la maendeleo ya jamii, ambapo  taarifa mbalimbali zimekuwa zikipokelewa na kujadiliwa. Kila nchi mwanachama wa Umoja wa  Mataifa inapata fursa ya kuelezea mafanikio na changamoto  inayokabiliana nazo katika utekelezaji wa jukumu la kuwaletea maendeleo wananchi wake. Aidha wajumbe wamekuwa pia wakitoa mapendekezo na ushauri wa nini kifanyike  ili kusukuma mbele ajenga ya  maendeleo endelevu na kuupiga vita umaskini kwa njia ya ubia kati ya  nchi hizo, Umoja wa Mataifa na wadau wengine wa maendeleo. Katika Mkutano huo Tanzania kwa upande wake imesisitiza haja na  umuhimu wa  watu wenye ulemavu  kupewa kipaumbele katika mipango ya maendeleo kwa  kile inachosema kwamba kuna uhusiano wa karibu kati ya umaskini na ulemavu na kwamba kundi hilo la jamii ni muhimu sana katika utekelezaji wa  Malengo ya Maendeleo ya Millenia ( MDGs)
HABARI KAMILI
NA MWANDISHI MAALUM, NEW YORK
Wakati  Umoja wa Mataifa((UM) ukieleza kwamba, kumekuwa na ongezeko kubwa la kati ya walionacho  na wasionacho, Tanzania kwa upande wake inasema inaamini kwamba kuna uhusiano   mkubwa kati ya umaskini na ulemavu.
Na kwa sababu hiyo, Tanzania , imependekeza kuwapo kwa juhudi  za makusudi za kuwasidia watu wenye ulemavu  na kutambua mchango wao ili waweze siyo tu  kuondokana na  umaskini na  bali pia kujiletea maendeleo endelevu.
Kauli hiyo imetolewa na Balozi wa  Kudumu  wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika  Umoja wa Mataifa, Tuvako Manongi, wakati alipokuwa akichangia majadiliano  ya Kamati ya Tatu ya Baraza Kuu la 67 la Umoja wa Mataifa. Kamati hiyo ambayo ni kati ya Kamati Sita zilizo chini ya Baraza Kuu, inahusika  pamoja na mambo mengine na  masuala ya Maendeleo, Haki za Binadamu  na Utamaduni.
Kuanzia   mwanzoni mwa wiki hii, wajumbe wa Kamati hiyo wamekuwa wakijadiliana na kubasilishana mawazo kuhusu Ajenda namba 27, ajenda    hiyo inahusu suala zima la   Maendeleo ya Jamii katika nyanja zote muhimu.
Katika mchango wake, Balozi Manongi  anasema,  kwa kutambua nafasi ya walemavu katika  kusukuma mbele ajenda ya maendeleo na kuupiga vita umaskini, ndiyo maana  ujumbe wa Tanzania  kwa kushirikiana na  ujumbe wa  Ufilipino waliandaa  Azimio kuhusu walemavu. Azimio ambalo hatimaye lilipelekea kuingizwa  kwa suala la walemavu katika  ajenda za Malengo ya Maendeleo ya Millenia ( MDGs).
Aidha kupitia juhudi hizo za Tanzania na  Ufilipino,   Umoja wa Mataifa umekubali kufanyika kwa   mkutano wa kilele katika ngazi ya Viongozi Wakuu wa Nchi na Serikali  hapo mwakani.
Ajenda  kuu ya  mkutano  huo itakuwa ni  kujadili masuala ya watu wenye ulemavu na nafasi yao katika utekelezaji wa  MDGs,   na kuupiga vita umaskini, Malengo ambayo yanafikia kilele chake  mwaka 2015.
Kupitia mkutano huo Tanzania inaamini kwamba viongozi wakuu wa nchi na serikali watatarajiwa kutoka na mkakati ambao utahakikisha kwamba watu wenye ulemavu na vipaumbele vyao vinazigatiwa katika maeneo yote ya maendeleo.
Kwa upande mwingine mwakilishi huyo wa Tanzania katika  UM anasema , ingawa Tanzania imefanikiwa katika kuandaa mipango na sera za kumwondolea  mwananchi  umaskini kupitia MKUKUTA na MKUZA , kupunguza ukali wa maisha, na kuboresha huduma mbalimbali za kijamii zikiwamo za afya. Bado inakabiliwa na changamoto mbalimbli zikiwamo  vifo vya wanawake wajawazito na watoto wachanga  chini ya miaka mitano. 
Aidha  akasema changamoto nyingine ni ile ya idadi kubwa ya wanawake kuendelea kukabiliwa na unyanyasaji na ubaguzi kama ilivyo duniani kote. Hata hivyo amesema kwa upande wa Tanzania, serikali za pande zote mbili zimejitahidi katika kuhakikisha kwamba wanawake wanakuwa na fursa sawa ikiwa ni pamoja na kuwa na haki ya kumiliki ardhi.
Awali akifungua mkutano huo,  Katibu Mkuu Msaidizi anayesimamia Idara ya  Uchumi na  Masuala ya Jamii ( ECOSOC) Bw. Wu-Hongbo, yeye aliwaeleza wajumbe wa mkutano huo kwamba, ingawa kumekuwa na mafaniko kadha wa kadha katika utekelezaji wa  MDGs  kuelekea mwaka 2015  lakini bado kuna changamoto nyingi.
Akazitaja baadhi ya changamoto hizo kuna ni kuongezeka kwa pengo ya kati ya walionacho  na wasionacho na tatizo kubwa la  ukosefu wa ajira hususani kwa vijana.
 Akabainisha kwamba kuanzia mwaka 1990 nchi  62 kati ya 116 na ambazo taarifa zao  zimeweza kupatikana , zimeonyesha kwamba kumekuwapo na ongezo kubwa la kati ya wasionacho na walionacho hali ambayo  imechangia katika kuzorotesha kasi ya kupunguza umaskini na matumaini ya kuwa na maendeleo endelevu.
Kama hiyo haitoshi, Bw. Wu- Hongbo anasema tatizo la ukosefu wa ajira nalo ni kubwa sana  hususani wa vijana ambao ndio wamekuwa waathirika wakubwa.
“ Vijana, wanawake na wanaume wanawakilisha karibu asilimia 40 ya watu milioni 200 ambao hawana ajira duniani kote” anabainisha  Bw. Wu- Hongbo
Nini  basi kifanyike katika kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa ajira na  changomoto nyinginezo zinazohusu maendeleo ya mwanadamu. 
 Katibu Mkuu Msaidizi anapendekeza kwa Jumuia ya Kimataifa kuhakikisha kwamba sera na mipango yao ya kiuchumi inazingatia haki za wanawake pamoja na mambo mengine, kwa kile alichosema  hakuna jamii inayoweza kustawi  pasipo  kuwawezesha wanawake.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages