Breaking News

Your Ad Spot

Feb 16, 2013

MAZUNGUMZO NJIA SAHIHI YA KUMALIZA MIGOGORO YA KIDINI- UMOJA WA MATAIFA

NAIBU KATIBU MKUU WA UN
Na Mwandishi Maalum, NEW YORK
Wakati viongozi wakuu  mbalimbali nchini Tanzania  wakisisitiza haja na umuhimu wa viongozi wa madhebu ya dini kuwa na utaratibu wa kukutana mara kwa mara. Umoja wa Mataifa nao kwa upande wake  unaeleza kwamba ni kwa  njia ya  mazungumzo  migogoro ya dini inaweza kuepukika.
 Kauli hiyo ya Umoja wa Mataifa,  umetolewa na  Jan Eliasson,Nabu Katibu Mkuu wa  chombo hicho ya Kimataifa ,  wakati wa  tukio maalum  la Muungano  kwaajili ya utamaduni wa Amani kwa njia ya  maelewano ya  madhehebu ya dini. Tukio ambalo limefanyika mwishoni mwa wiki hapa umoja wa mataifa likiwahusisha  wawakilishi kutoka  dini mbalimbali, vyama visivyo vya kiserikali na mabalozi.
“Migogoro mingi inayoendelea  hivi sasa duniani,  ni migogoro ya kidini. Mazungumzo baina ya imani mbalimbali yanaweza kusaidia kusuluhisha migogoro hii.  Tunaweza kupambana na chuki kwa njia ya mazungumzo   ili kujenga maelewano   na kujenga daraja la maisha bora kwa jamii zetu”.Akasema  Naibu Katibu Mkuu
Na kuongeza kuwa, dini zote zimekuwa  mstari wa mbele katika juhudi si tu za kuhimiza amani na upendo, bali hata katika miradi ya  kuwasaidia watu maskini kwa kutoa huduma  kama vile za afya, na kuwasaidia vijana.
 Hata hivyo akaonya kwamba, siasa kali za  kidini zimekuwa chimbuko la uharibifu wa kudumu na  mateso  katika jamii.
Na kwa sababu hiyo akasisitiza kutoachiwa kwa vikundi vya dini vyenye misimamo mikali  kuharibu na kuvuruga amani  na maendeleo na kazi nzuri inayofanywa na madhehebu ya dini .
“Hatuwezi kuruhusu kundi dogo la watu wenye misimamo mikali  kuharibu kazi nzuri zinazofanywa na  jumuia za kidini kwa waumini wao duniani kote” akahimiza Bw. Eliasson
Akaelezea  wasi wasi wake kuhusu vijana kutumiwa  na vikundi vyenye misimamo mikali kueneza  kampeni za chuki na  vurugu kwa ahadi za kupata dhawabu au wokovu ili wao watimize malengo yao.
“Kwa kawaida  vijana wana nguvu.  Tunapashwa  kutafuta   njia nzuri na sahihi za kuwafanya wazitumie nvugu  zao kuboresha maisha yao” akasisitiza Naibu Katibu Mkuu.
Naye  Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Bw. Vuk Jeremic kwa  upande wake alisema  Umoja wa Mataifa unaweza  kufaidika sana  kama viongozi wote wa dini watajihusisha na kufanya kazi kwa moja ili kuleta amani. Huku akiutaka  Umoja huo kuogeza kasi ya kushirikiana na madhehebu ya dini.
“ Hebu basi  na turejee na kukumbatia wito unaotolewa na imani zetu, wito wa kuwasaidia watu wengine wenye matatizo, wito wa kuheshimiana wenyewe kwa  wenyewe,ikiwa  ni pamoja na  uhuru wa kuabudu wakati wowote na mahali popote bila ya kujali tofauti zetu za imani”.
Rais huyo wa Baraza Kuu akasema kila mtu anawajibu wa kuwasiliana na mwenzake na kusahau yaliyopitia na kuonya kwamba kama vyanzo vilivyopita  vya migogoro ya kidini vitaendelea kukumbushiwa mara kwa mara, kuna hatari kubwa ya kuitumbukiza dunia katika  machafuko ya kutisha

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages