Breaking News

Your Ad Spot

Sep 11, 2013

WANANCHI WAZUIA MSAFARA WA KINANA KUDAI HUDUMA ZA MAJI NA UMEME

*KINANA AWASIKILIZA KWA MOYO MKUNJUFU
*AWATAKA KUWA WATULIVU WAKATI SERIKALI IKIFANYA JITIHADA KUTATUA KERO ZAO 
NDUGU KINANA
SHINYANGA, Tanzania.
MSAFARA wa Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana leo umelazimika kusimama kwa muda baada ya wakazi wa kijiji cha Mwabenda kata ya Solwa wilayani Shinyanga kuuzuia wakiwa na mabango wakiomba kupatiwa huduma ya maji na umeme.

Hali hiyo ilijitokeza wakazi msafara huo ukielekea katika kijiji cha Salawe ambako kulipangwa kufanyika kwa mkutano wa hadhara ambapo mara baada ya magari kufika katika kijiji hicho umati mkubwa wa wananchi ulisimama barabarani ukiwa na mabango yenye ujumbe wa “Tunataka Maji” na “Tunataka umeme.”

Kutokana na hali hiyo msafara huo ulilazimika kusimama huku mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Annarose Nyamamubi, mbunge wa Jimbo la Solwa, Ahmed Salum na baadhi ya askari polisi wakihaha kuwazuia wananchi hao na kuwasihi waondoke barabarani ili msafara uweze kuendelea na safari yake.


Hata hivyo juhudi hizo hazikufua dafu mbele ya wananchi hao ambao mbali ya kubeba mabango baadhi ya akina mama walikuja na ndoo za maji wakionyesha maji wanayotumia ambayo yalikuwa yamechanganyikana na tope huku wakihoji kuwa hayo maji ndiyo na hao viongozi wanatumia kwao?

Hali hiyo ilisababisha katibu mkuu na viongozi wengine wa kitaifa aliokuwa ameongozana nao pamoja na mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Ally Rufunga kufika katika eneo ambalo wananchi hao walikuwa wamesimama na kuwasikiliza malalamiko yao ambapo waliomba kushusha mabango chini ili wajibiwe hoja zao.

Walipopewa nafasi ya kueleza tatizo lao walisema pamoja na bomba kubwa la maji kutoka Ziwa Victoria kwenda katika miji ya Shinyanga na Kahama kupita katika kijiji chao lakini wao hawana huduma hiyo huku wakilazimika kutumia maji yaliyochanganyikana na tope ambayo siyo salama kwa matumizi ya binadamu.

Kutokana na hali hiyo mbunge wa Jimbo la Solwa alilazimika kutoa maelezo ya kina kwa wananchi hao ambapo alisema tayari mipango ilikuwa mbioni kuhakikisha kijiji hicho cha Mwabenda na vijiji vingine 44 vinapatiwa huduma ya maji kutoka Ziwa Victoria pamoja na umeme.

“Ndugu zangu naomba mtusamehe kwa kutowapatia taarifa juu ya miradi hii ya maji na umeme inavyoendelea kutekelezwa katika maeneo yetu, hivi ninavyozungumza tayari mipango ya kukipatia kijiji chenu maji kwa kuunganisha mtandao kutoka katika bomba kuu na vijiji vingine 44 imekamilika na kazi hiyo itaanza hivi karibuni,”

“Kiasi cha shilingi bilioni 3.6 zimeishapatikana na kazi hii itaanza hivi karibuni niwaeleze wazi kuwa kufikia mwanzoni mwa mwezi Novemba mwaka huu kazi itakuwa imekamilika na tatizo la maji litamalizika, kuweni na subira,” alisema Salumu.

Hata hivyo katibu mkuu pia alimuomba mkuu wa mkoa naye azungumze na wananchi ili awathibitishie juu ya maombi yao, ambapo mkuu huyo aliposimama aliwatoa hofu wananchi hao kutokana na uamuzi waliouchukua wa kuzuia msafara wa kiongozi mkuu ndani ya chama na kwamba kilichochangia hali hiyo ni kutokuwepo kwa mawasiliano ya karibu.

“Ndugu zangu tunakuombeni radhi sana kwa kucheleweshewa kupatiwa taarifa juu ya suala hili, ukweli ni kwamba tayari kazi ya kuwapatia maji katika kijiji chenu iko mbioni kuanza, lakini pia suala la umeme mkandarasi kwa ajili ya kusambaza umeme katika vijiji 10 amepatikana, hivyo kuweni na subira,” alisema Rufunga.
  
Kinana aliwataka wananchi kuwa na subira wakati serikali ya CCM ikishughulikia kero zao mbalimbali zilizokuwa zikiwakabili na kwamba Chama cha Mapinduzi kitahakikisha ahadi ilizozitoa kwa wananchi mwaka 2010 zinatekelezwa na pale itakaposhindikana kitaeleza sababu za kukwama. IMEANDIKWA NA CHIBURA MAKORONGO, SHINYAGA

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages