Breaking News

Your Ad Spot

Dec 23, 2013

VIJANA WAMPONGEZA JK KUWAWAJIBISHA MAWAZIRI WANNE

MWENYEKITI WA CCM, RAIS KIKWETE
NA BASHIR NKOROMO
UMOJA wa Vijana wa CCM, Kata ya Mabibo, Kinondoni jijini Dar es Salaam, umempongeza Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete kwa kuwavua uongozi mawaziri wanne mwishoni mwa wiki.

Mawaziri waliovuliwa uongozi kufuatia Rais Kikwete kutengua teuzi wao ni, Dk. Emmanuel Nchimbi (Waziri wa Mambo ya Ndani), Shamsi Vuai (Waziri wa Ulinzi), Mathayo David Mathayo ( Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi) na Khams Kagasheki (Maliasili na Utalii) ambaye ndiye pekee pamoja na uteuzi wake kutenguliwa na Rais lakini alitangaza kujiuzulu akiwa Bungeni.

Kutenguliwa kwa uteuzi wa mawaziri hao kulitangazwa rasmi Bungeni na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, hatua iyotokana na mapendekezo ya bunge, baada ya Kamati yake ya kudumu ya  Ardhi, Maliasili na Mazingira kubaini 'uozo' katika operesheni iliyofanyika hivi karibuni ya tokomeza ujangili.

Pongezi hizo ya UVCCM Mabobibo, ni miongozi mwa mazimio waliyofikia wajumbe wa Baraza Kuu la UVCCM kata hiyo, baada ya semina yao iliyomalizika jana kwa kufunguwa na Katibu wa Jumuia ya Wazazi mkoa wa Dar es Salaam, Mohamed Cholage.


Katika maazimio hayo, Vijana hao, Wamepongeza ziara za Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana ambazo amefanya hivi karibuni na sekretarieti yake, na kumuomba Kinana kuendeleza ziara hizo, kwa maelezo kwamba zimeonyesha manufaa makubwa kwa Chama.

Katika ziara iliyomalizika hivi karibuni Kinana alifanya ziara katika mikoa ya Mtwara, Ruvuma, Mbeya na Njombe akiambatana na Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye na Katibu wa NEC, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, Dk. Asha-Rose Migiro ambaye sasa pia ni Mbunge kufuatia kuteuliwa na Rais Kikwete.

Pamaoja na kupongeza ziara hizo, UVCCM Mabibo pia wameazimia kuhakikisha mitaa mitatu iliyopo chini ya chama cha CUF, kati ya sita ya kata hiyo ya Mabibo inarejeshwa kwenye himaya ya CCM baada ya uchaguzi wa serikali za mitaa uliopangwa kufanyika mwakani.

Akizungumza wakati wa kufunga semina hiyo, Cholage aliunga mkono maazimio hayo, akiyaeleza kwamba ni ya msingi.

"Kwa kweli naunga mkono maazimio. Siyo kwamba tunafurahi mawaziri hawa kukosa kazi, la hasha, lazikini kinachotufurahisha zaidi ni kuona kwamba Mwenyekiti wa Chama Rais Kikwete amesimamia inavyostahili misingi ya uwajibikaji", alisema Cholage na kuongeza;

"Pia hii kazi inayofanywa na Mzee wetu Kinana na kina Nape, ni ya kupigiwa mfano ambayo sisi kama vijana, lazima kuiunga mkono kwa dhati ya mioyo yetu yote, lakini si kwa maneno tu bali kwa vitendo".

Cholage aliwahimiza vijana, kuwania nafasi za uongozi wa mitaa, uchaguzi utakapowadia, lakini akawataka kufanya hivyo kwa kujipima kwanza kama anatosha kila atakayekuwa anadhamira ya kugombea.

Aliwataka UVCCM kuwa imara katika kukilinda Chama akiwakumbusha kuwa wao ndiyo askari wa mstari wa mbele katika kazi hiyo.

Cholage aliwataka vijana wa CCM na vijana wote kwa jumla, kujiepusha na tabia ya kulalamika waliyonayo baadhi yao, badala yake wawe mstari wa mbele kukosoa katika njia zinazostahili na kisha kuonyesha njia wanazoona zinafaa kutumika katika utatuzi wa changamoto wanazoziona.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages