Breaking News

Your Ad Spot

Jan 10, 2014

IDADI YA TEMBO YAPUNGUA KWA ASILIMIA 66

DAR ES SALAAM, Tanzania
Wizara ya Maliasili na Utalii, imetangaza matokeo ya sensa ya Tembo, yakionyesha kuwa idadi ya Tembo imepungua kwa asilimia 66 hasa katika ukanda wa Selous-Mikumi ikilinganishwa na sensa iliyofanyika mwaka 2009.


Matokeo ya Sensa hiyo iliyofanywa Oktoba na Novemba mwaka jana, yameonyesha kuwa Ukanda wa Selous-Mikumi kwa sasa una Tembo 13,084 huku ukanda wa Ruaha-Rungwa ukiwa na Tembo 20,090.


Akitangaza matokeo hayo leo jijini Dar es salaam, Kaimu Waziri wa Wizara hiyo, LAZARO NYALANDU, amesema idadi hiyo ya Tembo kwa ukanda wa Selous-Mikumi imepungua kwa asilimia 66 ikilinganishwa na idadi ya mwaka 2009 ambapo kulikuwa na Tembo 38,975.

Kwa upande wa Ukanda wa Ruaha-Rungwa, idadi ya Tembo imepungua kwa asilimia 36.5 ikilinganishwa na idadi ya mwaka 2009 ambapo kulikuwa na Tembo 31, 625.

Kufuatia kupungua kwa Tembo hao, serikali imechukua jitihada mbalimbali ikiwa pamoja na kuendesha Operesheni Tokomeza Ujangili ambayo itaingia awamu ya pili ili kulinusuru taifa na wimbi la ujangili dhidi ya Tembo.

Hata hivyo, NYALANDU, amewataka Askari wa Wanyamapori kufanya kazi kwa uadilifu na kutojiingiza katika vitendo vya Ujangili, kwani wakibainika kufanya hivyo hatua za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yao.  SORCE:UHURU FM

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages