Meneja
wa Shamba la Chuo cha Kilimo Kizimbani liliopo Makurunge Bagamoyo Nd.
Abdulrahman Mahmoud Hamid akimpatia maelezo Makamu wa Pili wa Rais wa
Zanzibar Balozi Seif wakati wa ziara yake ya kulikagua shamba la SMZ
waliokabidhiwa chuo hicho. Nyuma
ya Balozi Seif ni Waziri wa Ardhi Zanzib ar Mh.Abdulla Shaaban, Waziri
wa Kilimo Zanzibar Dr. Sira Ubwa Mwamboyta na Katibu Mkuu wa Wizara ya
Ardhi Nd. Ali Khalil Mirza.
Balozi
Seif akitafakar na Mwanasheria wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa SMZ
Bwana Saleh Said Mbarouk akiwa pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo
kulia yake Nd. Hemed Mwanga mwenye miwani, Waziri wa Kilimo Bara Mh.
Steven Wasira na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo.
Baadhi
ya sehemu ya shamba la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar liliopo
Makurunge Bagamoyo ambalo limekabidhiwa Chuo cha Kilimo Kizimbani ili
kuliendeleza.
Ujumbe wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar uliotembelea shamba la Mifugo la SMZ la Makurunge waliangalia fukwe ya Bagamoyo iliyomo pembezoni mwa shamba hilo.
Makamu
wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif aliyepo kati kati na ujumbne
wake wakifurahia fukwe safi iliyomo ndani ya shamba la Serikaliu ya
Mapinduzi ya Zanzibar liliopo Makurunge. Kushoto
kwa Balozi Seif ni Meneja wa Shamba hilo, Abdulrahman Hamid Mahmoud,
wakati kulia ya Balozi Seif ni Katibvu Mkuu Wizara ya Kilimo na Mali
Asili Zanzibar Nd. Afan Othman Maalim, Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi
Evarist Ndikilo, Waziri wa Kilimo Zanzibar Dk. Sira Ubwa Mwambioya na
Naibu Waziri wa ARDHI Bara Mh. Angela Kairuki.
Naibu
Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi Tanzania Bara Mh. Angela
Kairuki akimuhakikishia Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif
kwamba Wizara hiyo itasimamia kukamilisha taratibu zote
zitakazothibitisha uhalali wa umiliki wa SMZ katika shamba la mifugo la
Makurunge Bagamoyo Mkoa wa Pwani. Kulia ya Naibu Waziri wa Ardhi Mh. Angela Kairuki ni Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo (Picha zote na Hassan Issa – OMPR – ZNZ)
Na Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
26/2/2015.
Makamu
wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba msimamo
wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Baraza lake la Mapinduzi
wa kulitumia shamba lake la Kilimo liliopo Makurunge Bagamoyo Mkoa wa
Pwani ni ule ule wa kuendeleza Mifugo na Kilimo.
Alisema
uamuzi huo umezingatiwa kwa makusudi kuheshimu wazo la pamoja
lililoibuliwa kati ya Rais wa Kwanza wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania
Marehemu Mwalimu Julius K. Nyerere na Rais wa Awamu ya Pili ya Zanzibar
Mh. Aboud Jumbe Mwinyi la kuipatiwa Zanzibar eneo la Mifugo na Kilimo
Tanzania Bara ili kuimarisha Sekta hizo.
Balozi
Seif Ali Iddi alisema hayo wakati alipofanya ziara maalum ya kulikagua
shamba la Mkurunge akiambatana na Waziri wa Kilimo, Ushirika na Chula
wa Bara Mh. Steven Wasira, Naibu Waziri wa Ardhi Bara Mh. Angeja
Kairuki, Waziri wa Ardhi Zanzibar Mh. Ramadhan Abdulla Shaaban, Waziri
wa Kilimo Zanzibar Dr. Sira Ubwa Mwamboya, Makatibu Wakuu wa Wizara hizo
pamoja na watendaji waandamizi wa Serikali zote mbili.
Alisema
Shamba la Makurunge Bagamoyo lina Historia ndefu iliyoasisiwa na Marais
waliopita ikilenga kuimarisha Muungano uliopo kati ya Tanganyika na
Zanzibar sambamba na kuipa nguvu Zanzibar kwa shughuli zake za kuongeza
uzalishaji katika Sekta ya Mifugo.
Balozi
Seif alifahamisha kwamba Zanzibar imekuwa na eneo dogo la ardhi kwa
kuendeleza sekta ya Kilimo na Mifugo huku idadi ya wakaazi wake
ikiendelea kuongezeka kiwango ambacho kinastahiki kujengewa mindo mbinu
ya maisha katika uzalishaji Kiuchumi.
Makamu
wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisisitiza umuhimu wa
ushirikiano kati ya Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Mkoa wa
Pwani pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya
Kilimo na Mali Asili Zanzibar Chini ya Chuo cha Kilimo
Kizimbani kilichokabidhiwa shamba hilo.
Alisema
ushirikiano huo muhimu kwa kiasi kikubwa ndio utakaowezesha kusadia
sana hatma ya shamba hilo ambalo limekuwa na changamoto ya kuvamiwa na
baadhi ya Watu kwa shughuli za Kilimo pamoja na ujenzi wa Makazi.
Alisema
lile lengo la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuomba kupatiwa
shamba hilo kutoka Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ni
vyema ukazingatiwa na kuheshimiwa na watu wanaolizunguuka eneo hilo.
Akitoa
Taarifa ya Historia ya Shamba la Makurugne hapo Ofisi za Halmashauri ya
Wilaya ya Bagamoyo Mkuu wa Wilaya ya Magamoyo Nd.Majid Hemed Mwanga
alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iliomba eneo la ufugaji
wanyama kwa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania mapema mwaka
1977.
Nd.
Mwanga alisema Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia
Wizara ya Mali Asili ilitoa Barua rasmi Mwezi Febuari mwaka huo huo wa
1977 wa kuipatia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar eneo la Shamba hapo
Makurunge Bagamoyo lenye ukubwa wa Hekta 28,099.
Alisema
kazi hiyo ilikwenda sambamba na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
kuwalipa fidia wananchi 64 waliokuwa na mali na vipando vyao kwenye eneo
hilo ambapo watu 16 waliohusika na zoezi hilo walikataa kulipwa fidia
hizo.
Mkuu
huyo wa Wilaya ya Bagamoyo alieleza kwamba kufifia kwa shughuli za
uzalishaji wa Mifugo katika shamba hilo zilizokuwa zikifanywa
na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kulitoa fursa kwa wawekezaji
kujitokeza kuomba eneo hilo kwa shughuli za uwekezaji.
Alifafanua
kwamba mazungumzo ya pamoja kati ya Rais wa Zanzibar na Rais wa
Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania yalifanyika na ukapatikana uamuzi wa
kuipatia Kampuni ya Miwa ya Bagamoyo Eco Energ eneo la Hekta 22,000
kulima miwa kwa ajili ya uzalishaji wa Sukari.
Hata
hivyo Nd. Mwanga alieleza kwamba zipo changamoto kadhaa
zilizojitokeza kwenye shamba hilo ukiwemo uvamizi wa ujenzi na kilimo
uliofanywa na watu wapatao 400 ndani ya shamba hilo.
Akizungumza
katika kikao cha kutathmini ziara hiyo kwenye Hoteli ya Bagamoyo
Oceanic Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo alisema kwamba
Wilaya ya Bagamoyo imo ndani ya mpango wa Serikali wa kulifanya eneo
hilo kuwa ukanda wa Uwekezaji Kiuchumi (EPZ).
Mhandisi
Ndikilo alisema ipo haja ya makusudi ya kuwepo kwa vikao vya mara kwa
mara vya pamoja kati ya Viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
kupitia Mamlaka ya Uwekezaji vitega uchumi { ZIPA } na Halmashauri ya
Wilaya ya Bagamoyo ili kuwa na mtazamo wa pamoja utakaokwenda sambamba
na mpango huo.
Alisema
mtazamo huo utajenga hatma njema ya matumizi sahihi ya Ukanda huo wa
Bagamoyo likiwemo eneo la shamba hilo la Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar liliopo Makurunge.
Mapema
asubuhi katika Kikao cha Maandalizi ya ziara hiyo kiliochofanyika
katika Makazi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar yaliyopo Bara bara
ya Haile Sellassie Jijini Dar es salaam Kamishna wa Ardhi wa Tanzania
Bara Nd. Moses Msilika alisema kwamba mabadiliko ya kiuchumi katika
mipango miji ya Serikali yameifanya Wilaya ya Bagamoyo kuingia katika
ramani ya uwekezaji.
Nd.
Moses alisema shamba la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar liliopo
Makurunge limeshapimwa rasmi na kueleweka vyema mipaka yake na
limeshindwa kutumiwa kwa mujibu wa mipango miji kutokana na kuwa liko
chini ya mamlaka ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269