Breaking News

Your Ad Spot

Feb 27, 2015

ZITTO KABWE KUTANGAZA MAAMUZI MAGUMU YA KUJITOWA CHADEMA MWEZI WA TATU

MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, amesema hatma yake kisiasa ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) itajulikana katika kipindi cha mwezi mmoja kutoka sasa.
Raia Mwema linafahamu kwamba tangazo hilo la kisiasa linahusu mustakabali wake wa kisiasa ndani ya Chadema, chama ambacho amekitumikia katika maisha yake yote ya kisiasa tangu akiwa mtoto wa umri wa miaka 16.
Katika mahojiano aliyofanya kwa njia ya mtandao na gazeti maarufu la Guardian la Uingereza wiki iliyopita, Zitto alisema kuna kitu kikubwa atakifanya mwishoni mwa mwezi Machi huu.
“Sijawahi kufanya kampeni yoyote kubwa ya kisiasa kupitia mtandao wa twitter katika maisha yangu ya kisiasa, lakini nataraji kuwa nitafanya hivyo katika muda wa mwezi mmoja kutoka sasa. Fuatilieni tu twitter na mtaona,” alisema Zitto pasipo kwenda kwa undani.

Gazeti hilo la Uingereza limeanzisha utaratibu mpya wa kuhoji watu maarufu kwa kutumia mtandao wa twitter (twit interview) na Zitto alikuwa mwanasiasa wa kwanza kuhojiwa baada ya kubainika kuwa ndiye anayeongoza kwa kuwa na wafuasi wengi kwenye mtandao huo hapa nchini.
Akizungumza na gazeti hili kuhusu nini hasa anataraji kukifanya mwishoni mwa mwezi Machi kama alivyozungumza na gazeti hilo, Zitto alisema ni mapema kwa sasa kuweka kila kitu hadharani lakini wakati ukifika kila kitu kitakuwa wazi.
“Niseme kwamba kwenye mahojiano yale nilisema hivyo kweli na nakuhakikishia kuwa kuna tukio litatokea mwishoni mwa mwezi Machi. Ni tukio gani na linahusu nini bado mapema kusema.
“Ila naomba kuahidi Watanzania kuwa watafahamu kila kitu kuhusu tukio hilo wakati ukifika. Hiyo kampeni ambayo itaendeshwa kupitia mtandao wa twitter na mingineyo, itakuwa ya kisasa na ya uhakika kuliko yoyote ambayo imewahi kuendeshwa katika historia ya Tanzania, “ alisema.
Zitto alikataa kusema lolote kama tangazo hilo litahusiana moja kwa moja na kuhama kwake kutoka Chadema kwenda ACT au chama chochote kingine cha siasa hapa nchini zaidi ya kusema; “subirini”.
Kwa sasa, Zitto ni Mbunge na mwanachama wa Chadema kwa sababu tu ya zuio ambalo Mahakama Kuu kupitia Jaji John Utamwa liliweka katikati ya mwaka jana la kufukuzwa kwake ndani ya chama hicho kutokana na kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho.
Zitto na wenzake, Profesa Kitila Mkumbo na Samson Mwigamba, walifukuzwa na Chadema kwa madai ya kupanga mapinduzi ya kumng’oa madarakani Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe.
Mwigamba na Kitila wamehamia katika chama kipya cha siasa cha ACT; Mwigamba akiwa Katibu Mkuu wa muda na mwenzake mshauri na Zitto mwenyewe amekuwa akihusishwa na chama hicho.
Akizungumzia mahojiano hayo ya Zitto na Guardian, Dk. Kitila Mkumbo alisema aliyasoma mahojiano hayo lakini akasema anayejua nini kitatokea mwishoni mwa Machi ni Zitto mwenyewe.
“Mimi kama mshauri wa ACT nasema Zitto kama mwanasiasa makini ana mawazo yake na mipango yake. Mimi nasisitiza tu kwamba kama ataamua kuja ACT basi tunamkaribisha kwa mikono yote miwili.
“Tunaamini kwamba yeye ni muumini wa dhana ya Unyerere (Nyerereism) ambayo ndiyo msingi mkuu wa sera za ACT. Kama ataamua vinginevyo, sisi pia tutamuunga mkono kwa sababu tunajua itakuwa kwa nia njema,” alisema.
Katika mahojiano hayo na Guardian, Zitto aliulizwa kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu siasa na Tanzania, ikiwamo changamoto za kisiasa, hifadhi za jamii na nguvu ya mitandao ya kijamii katika siasa za hapa nchini.
Zitto alisema silaha kubwa ya maendeleo ambayo Tanzania inayo kwa sasa ni wingi wa vijana ambao alisema kama watawekewa mipango mizuri na kuwezeshwa kutumika kwa kadri ya uwezo wao, Taifa litapiga hatua kubwa.
Alisema fursa hiyo ina hatari yake nyingine kwamba chini ya asilimia 20 ya Watanzania hawana ulinzi wowote wa Mifuko ya Hifadhi za Jamii, jambo alilosema ni hatari kwa mustakabali wa Taifa.
Alisema pia kwamba kwa sasa Watanzania wengi wana ufahamu wa masuala ya mitandao ya kijamii, lakini akasema idadi ya wanaoitumia ni ndogo; huku akibainisha kuwa baadhi ya viongozi wa juu wa serikali hawako hata kwenye mitandao kama twitter.
Zitto ana wafuasi zaidi ya 200,000 katika mtandao wa twitter akiwa anaongoza kwa wafuasi; huku katika nchi nyingine barani Afrika wanaoongoza wakiwa marais, wanamichezo na wanamuziki maarufu kama Didier Drogba wa Ivory Coast na Wiz Kid wa Nigeria.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages