Breaking News

Your Ad Spot

Jun 15, 2015

SERA YA MAENDELEO YA VIJANA NA HARAKATI YA KUWAKOMBOA VIJANA NCHINI

imagesNa: Genofeva Matemu, na Benjamini Sawe
……………………………………………….. Serikali iliandaa Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana mnamo mwaka 1996; Utekelezaji wa Sera hii umekabiliwa na changamoto mbalimbali za kitaifa na za kidunia. Katika milenia hii ya Sayansi na teknolojia, vijana wa kiume na kike ni rasilimali kubwa zaidi kwa sasa na siku za baadaye; wanatoa msukumo wa kuleta mageuzi ya kijamii, kiuchumi na kisiasa katika sayari hii yenye mabadiliko ya haraka duniani. Mazingira ya dunia, kijamii, kiuchumi na kisiasa yameathiri hali ya vijana nchini Tanzania, Uhamiaji wa vijana kutoka maeneo ya vijijini kwenda mijini umeongeza mzigo wa huduma za Umma mijini na miundombinu ya kijamii hivyo kuleta ukuaji wa haraka wa sekta isiyo rasmi na ongezeko la matukio ya ajira mbaya kwa vijana. Vijana wengi nchini wanafanya kazi kwenye sekta za kilimo, uvuvi, madini, ufugaji wa wanyama na viwanda vidogovidogo kama vya useremala, sonara, biashara ndogondogo za kuuza nguo za mitumba, matunda na vyakula vya aina mbalimbali. Pamoja na ukweli kwamba vijana hawa wamejiajiri lakini bado wanakumbana na matatizo mengi katika kutekeleza shughuli zao; matatizo hayo ni pamoja na ukosefu wa mtaji wa kufanyia kazi, vifaa na ujuzi wa kiufundi au stadi muhimu za maisha. Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 1996 imewezesha utekelezaji wa program mbalimbali za maendeleo ya vijana ambazo ni pamoja na stadi za kujenga uzoefu kwa ajili ya uwezeshaji wa kiuchumi, maadili mema, mwenendo na utendaji bora, ushiriki wa vijana na utoaji wa huduma rafiki kwa vijana. Hata hivyo Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 2007 inalenga masuala ya maendeleo ya vijana katika uwezeshaji wa kiuchumi, mazingira, ukuzaji wa ajira, ushiriki wa vijana katika masuala mbalimbali kwenye jamii, VVU na UKIMWI, jinsia, Sanaa na utamaduni, michezo, afya ya uzazi kwa vijana na masuala ya maisha ya familia. Katika kutekeleza Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 2007 Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo imejizatiti kutoa elimu ya uhamasishaji, Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, ujuzi, na stadi za maisha kwa vijana wote nchini kwa kukutana na vijana katika kila Halmashauri na kutoa elimu inayowasaidia vijana kujitambua hivyo kutumia fursa mbalimbali walizonazo kujiendeleza. Kwa kuanzia Vijana kutoka Halmashauri za Mkoa wa Mbeya, Dodoma,Kilimanjaro, Singida, Kigoma, Manyara, Arusha na Mara wamefikiwa na Wizara ya habari, Vijana, Utamaduni na Michezo katika harakati za kuwakomboa vijana kifikra na kiuchumi ili kuondokana na kundi la vijana lisilokuwa na mwelekeo katika jamii. Wizara inaendelea kuhamasisha vijana kujiunga katika vikundi vya uzalishajimali, kusajili vikundi hivyo na hatimaye vikundi hivyo kujiunga katika SACCOS za vijana zilizoanzishwa, ikizingatiwa kuwa hii ni mojawapo ya kigezo muhimu cha kikundi kuweza kupewa Mkopo kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana. Mfuko wa Maendeleo ya vijana una changamoto mbalimbali zikiwemo: Fedha zinazotengwa kwa ajili ya Mfuko kuwa kidogo ukilinganisha na mahitaji ya Vijana, Vijana wengi kutokuwa na mwamko wa kurejesha fedha kwa wakati, Maandiko ya Miradi mingi inayowasilishwa kutokidhi vigezo ili kuweza kukopesheka. Fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ni kwa ajili ya Vijana wote nchini, kila kijana anayo haki ya kunufaika na Mkopo kutoka katika Mfuko huu. Vijana wanatakiwa kukopa na kurejesha na siyo kama wengine wanavyohusisha fedha hizi na masuala ya kisiasa wakidhani ni takrima. Pia, wanatakiwa kuzingatia masharti/ vigezo vilivyopo katika mwongozo wa Mfuko pindi wanapoandaa Maandiko ya Miradi yao. Serikali imelenga kuendelea kuboresha Mfuko huu ili kuwa na fedha za kutosha na kuweza kuwafikia vijana wengi nchini, hii itasaidia vijana wengi kujiajiri wao wenyewe na kutengeneza ajira kwa vijana wengine. Katika kutekeleza azma ya kusaidia Vijana, jumla ya shilingi Bilioni 6 zimetengwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2014/2015 kwa ajili ya kusaidia mfuko wa Maendeleo ya Vijana, ambapo Vijana kutoka Halmashauri mbalimbali nchini wamepatiwa mikopo yenye unafuu, riba kidogo na upatikanaji wake ukiwa ni wa urahisi.
Mfuko huu ulianzishwa mwaka 1993, chini ya kifungu namba 17(1) cha The Exchequer and Audit Ordinance (Cap 439) No 21 of 1961, lengo likiwa ni kuwasaidia vijana ili wapate mikopo yenye masharti nafuu.
Katika ziara yake ya kukagua miradi ya vikundi vya Vijana wa Wilaya ya Kilwa mkoani Lindi hivi karibuni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari Vijana, Utamaduni na Michezo Bi. Sihaba Nkinga amewashauri vijana kuchangamkia fursa hiyo ambayo haimuhitaji mkopaji kuwa na dhamana isiyo hamishika bali kuwa na uaminifu wa kurejesha mkopo huo utakaotolewa kupitia vyama vya kuweka na kukopa SACCOS.
“Vijana wanatakiwa kuhamasishwa kuunda na kujiunga katika vikundi vya uzalishaji mali na kuunda SACCOS za vijana ili waweze kupatiwa mikopo kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana kwa ajili ya kuongeza mitaji na kupanua uzalishaji”. Anasema Bi. Nkinga.
Afisa Maendeleo ya Vijana Halmashauri ya Wilaya ya Mwanga Bibi. Subira Mfanga anabainisha kuwa vijana nchini wanahitaji elimu ya ziada kubadilisha fikra zao kwani kwa kufanya hivyo itawasaidia vijana kutambua kuwa fursa za ajira zinasababishwa na wao wenyewe kwa kuwa waaminifu, kuchukua mkopo unaotolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana na kurudisha mkopo huo kwa wakati ili kuweza kutoa fursa kwa vijana wengine kufikiwa na mkopo huo.
Bibi Mfanga anaongezea kuwa zoezi lililofanywa na Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kuwafikia vijana wa Halmashauri ya Mwanga ni lulu kwa vijana wa Wilaya hiyo kwani limewasaidia vijana kujielewa hivyo kuacha kutumika vibaya katika makundi yanayoleta uhasama ndani ya jamii bali wajikite zaidi katika uwekezaji kwa kuanzisha miradi endelevu, yauhakika na inayotekelezeka. Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma Bw. Deogratius Yenza amesema kuwa viongozi wa Mkoa wa Dodoma wako bega kwa bega na Vijana wa Mkoa huo kwani vijana ndio sehemu kubwa ya nguvu kazi ya Taifa wanahitaji kujengewa ujuzi, kushauriwa, na kufanyiwa tathmini ya miradi wanayoombea mikopo ili iweze kuleta tija na hamasa kwa vijana wengine kuiga mfano wa vijana wa Dodoma. Aidha Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Maendeleo Vijana Bi. Venerose Mtenga amesema kuwa walengwa wa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ni vijana wenye umri kati ya miaka 15 hadi 35 watakaoruhusiwa kuomba mkopo na kurejesha mikopo hiyo kwa kipindi cha miaka miwili ambapo muda wa maandalizi utakuwa wa miezi mitatu tu na riba yake itakua asilimia kumi (10%) kwa mwaka ambapo kikundi kitalazimika kulipa tozo ya asilimia 15 iwapo kitashindwa kurejesha mkopo katika muda uliopangwa. Akifafanua jambo wakati wa semina ya kuhamasisha vijana wa Mkoa wa Mbeya Afisa Maendeleo ya Vijana Mkoa wa Mbeya Bw. George Mbijima amewataka vijana kutambua yakua miradi itakayopewa mikopo kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Vijana itaibuliwa na vikundi vya vijana wenyewe na andiko la miradi litawasilishwa kwa Afisa Maendeleo ya vijana wa Halmashauri husika ambapo ataitembelea miradi hiyo iliyowasilishwa kwake ili kuthibitisha uhai wake na uwezo wa miradi kurejesha mkopo na kuwasilisha miradi hiyo kwa Afisa wa Mkoa ambaye baada ya kuipitia ataituma Wizarani kwa hatua zaidi.
Hata hivyo, vijana waliopata nafasi kushiriki semina mbalimbali zilizotolewa na Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo wameiomba Serikali kupitia Idara ya Maendeleo ya Vijana kuhakikisha kuwa mafunzo hayo yanakuwa endelevu na yanawafikia vijana nchini kote ili kuwawezesha vijana kufahamu umuhimu wa Mfuko huo, upatikanaji wa fedha, pamoja na sifa za upatikanaji wa fedha kutoka mfuko wa Maendeleo ya Vijana.
Jitihada zote hizo zinalenga katika kufikia malengo na mikakati mbalimbali ya kukuza ajira kwa Vijana nchini kama zilivyoainishwa kwenye Sera ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 2007, Sera ya Ajira ya mwaka 2008, Mpango Kazi wa Taifa wa Ajira kwa Vijana wa mwaka 2007, MKUKUTA II na Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2025.
Tanzania kama sehemu ya dunia inatambua changamoto mbalimbali zinazowakabili vijana walioko katika mazingira hatarishi pamoja na umuhimu wa kuhakikisha kuwa vijana wanahusishwa kikamilifu katika malengo ya maendeleo kama Taifa la kesho.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages