Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Progesa Joyce Ndalichako
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI
KATAZO LA KUONGEZA ADA KWA SHULE ZISIZO ZA SERIKALI KWA MWAKA WA MASOMO 2016
Waraka
wa Elimu Na. 4 wa Mwaka 2008 uliweka viwango vya ada vinavyotozwa
katika shule za Msingi na Sekondari za Serikali na zile zisizo za
serikali. Ada iliyowekwa kwa shule za kutwa zisizo za serikali ni Tsh.
150,000/= na shule za bweni Tsh. 380,000/= kwa mwaka kwa kila
mwanafunzi. Aidha waraka huo ulielekeza kwamba ongezeko lolote la ada
lazima lipate kibali cha Kamishna wa Elimu kabla ya kuanza kutumika.
Hata
hivyo imegundulika kuna baadhi ya shule zisizo za serikali zimekuwa
zikiongeza ada kila mwaka pasipo kupata kibali cha Kamishna wa Elimu.
Utamaduni huu wa kuongeza ada kila ifikapo mwishoni mwa mwaka umekuwa
ukisababisha usumbufu mkubwa kwa wazazi/walezi na hata baadhi yao
kushindwa kuendelea kusomesha vijana wao katika baadhi ya shule.
Kwa tangazo hili wamiliki wote wa shule zisizo za serikali wanaagizwa kufanya yafuatayo:
1. Kutokuongeza
gharama za uendeshaji wa shule zikiwemo ada kwa mwaka wa masomo
unaoanzia mwezi Januari mwaka 2016 mpaka watakapopata maelekezo kutoka
kwa Kamishna wa Elimu; wale ambao tayari wameongeza gharama na ada kwa
mwaka wa masomo wa 2016 bila kibali cha Kamishna wa Elimu, Wizara
haitambui ongezeko hilo kwa kuwa ni batili na hivyo zimefutwa.
2. Ada zote kwa shule zisizo za serikali zitabaki kama zilivyokuwa zimeidhinishwa na Kamishna wa Elimu.
3. Kuwasilisha taarifa kwa Msajili wa Shule aliyepo Idara ya Ithibati ya Shule inayoeleza kiasi cha ada na gharama kinachotozwa
kwa sasa (kabla ya mwaka wa masomo 2016) na tarehe shule ilipopata
kibali kutoka kwa Kamishna wa Elimu kutoza kiwango hicho cha ada. Taarifa hiyo ifike ndani ya wiki mbili kuanzia tarehe ya tangazo hili.
Wathibiti
ubora wa shule waliopo sehemu mbalimbali nchini wanaagizwa kulifuatilia
suala hili kwa karibu ili kila shule itekeleze agizo hili na kutoa
taarifa zilizoelekezwa katika tangazo hili. Hatua za kinidhamu
zitachukuliwa kwa wamiliki ambao hawatatekeleza maagizo haya.
Aidha
Wizara iko katika hatua za mwisho za utafiti na kuandaa mfumo wa
kielektroniki wa kutambua gharama za kumsomesha mwanafunzi katika
elimumsingi (elimu ya awali, msingi na sekondari) na hivyo wadau
mbalimbali watoe ushirikiano kwa timu za wataalamu wanaofanya kazi hii
ili kusaidia katika kuukamilisha mfumo na hatimaye kuwa na ada elekezi
katika maeneo mbalimbali.
IMETOLEWA NA KATIBU MKUU
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269