Upinzani nchini Burundi unamlaumu Rais Jacob Zuma wa Afrika ya Kusini
ambaye, akiwa kiongozi wa ujumbe wa marais watano wa Afrika, ametaka
suala la muhula wa tatu wa Rais Pierre Nkuruniziza madarakani
lisijadiliwe.
Rais Jacob Zuma wa Afrika ya Kusini anayeongoza ujumbe wa marais
watano wa Afrika nchini Burundi akiwa na Rais Pierre Nkurunziza (kulia).
Mkutano kati ya marais hao na viongozi wa chama tawala na wa upinzani
mjini Bujumbura hapo jioni ya (Februari 25, (Februari 25, 2016)) unaonekana kuwa
ulimalizika pasi na makubaliano ya kimsingi. Tayari mmoja wa marais hao
wa Afrika, Ali Bongo wa Gabon, ameshaondoka nchini Burundi.
Mkutano huo uliokusudia kuweka msukumo kwenye jitihada za kumaliza mzozo
unaoikabili Burundi uliwajumuisha pia wajumbe wa mashirika yasiyokuwa
ya kiserikali na viongozi wa dini.
Licha ya kuwa upande wa chama tawala (CNDD-FDD) haukutowa taarifa yoyote
juu ya matokeo ya mazungumzo yao, wafuasi wa vyama vya upinzani
vinasema vimevunjwa moyo. Kiongozi wa chama cha UPRONA, ambacho
hakikubaliani na serikali ya Rais Nkurunziza, anasema ujumbe wa marais
hao watano wa Afrika haukufanya chochote cha maana.
"Tumevunjika moyo. Hakuna hatua yoyote iliyopigwa kuhusiana na nia ya
Umoja wa Afrika ya kumaliza mgogoro unaoikabili nchi. Rais Zuma anasema
swala la muhula wa tatu si la kujadiliwa kwani ni korti ya kikatiba
iliruhusu muhula huo wa tatu, wakati sote tunaelewa ni katika mazingira
gani korti ya kikatiba iliupitisha uamuzi huo," alisema mwanasiasa huyo,
huku akiutuhumu ujumbe huo kwa kuja kumuunga mkono tu Rais Nkurunziza
na muhula wake wa tatu.
Kwa upande wake, mkuu wa chama FRODEBU, Leonce Ngendakumana, ambaye pia
anaongoza muungano wa vyama vya upinzani, anasema waliwataka marais hao
wauone umuhimu wa mazungumzo yanayoshirikisha pande zote.
"Tunashuhudia silaha zilivyotapakaa nchini na pia uundwaji wa makundi ya
kijeshi. Walituuliza endapo kuna njia nyingine ya kuimaliza hali hiyo,
nasi tuliwahakikishia kuwa hakuna isipokuwa majadiliano. Kwa hiyo,
lazima majadiliano yafanyika na hayo wanaotajwa kuwa waliendesha
mapinduzi."
Nkurunziza hataki kuzungumza na 'magaidi'
Awali Rais Nkurunziza alishasema wazi kuwa hayuko tayari kuzungumza na
wale aliowaita "magaidi" wanaouhujumu usalama wa Burundi, akimaanisha
muungano wa wapinzani wake wanaoishi nje ya nchi hiyo na ambao wanatajwa
kuhusika na jaribio la mapinduzi lililoshindwa mwezi Mei 2015.
Hata hivyo, kabla ya kuondoka mjini Bujumbura , Rais Bongo wa
Gabon alisema kuwa wameafikiana majadiliano yataendelea kufanyika na
kuwashirikisha wote.
"Kilichoafikiwa baada ya kuzisikiliza pande zote ni kuwa lazima kuwepo
na mazungumzo. Ni kupitia njia hiyo tu, ndipo utulivu unapoweza kurudi
katika nchi hii", alisema Rais Bongo.
Mbali na Rais Bongo, ujumbe huo uliotumwa na Umoja wa Afrika na
unaongozwa na Rais Zuma wa Afrika Kusini, unawajumuisha pia Waziri Mkuu
wa Ethiopia, Haile Mariam Deseleyn, Rais Mohamed Ould Abdelaziz wa
Mauritania na Macky Sall wa Senegal.
Kauli ya mwisho juu ya matokeo ya mazungumzo hayo inatarajiwa
kutolewa na Rais Zuma, ambaye mchana huo anafanya mazungumzo na Rais
Nkurunziza.
Mwandishi: Hamida Issa/DW Bujumbura
Mhariri: Mohammed Khelef
Mhariri: Mohammed Khelef
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269