Breaking News

Your Ad Spot

May 17, 2016

MKUTANO WA KIUSALAMA WAFANYIKA KATIKA MSIKITI MMOJA NCHINI RWANDA

Wakuu wa vyombo vya usalama na viongozi wa Kiislamu wa Rwanda wamefanya mkutano katika msikiti mmoja nchini humo kujadili mustakabali wa kiusalama.
Viongozi wa Kiislamu waliohudhuria mkutano huo uliofanyika katika msikiti mmoja wa wilaya ya Ruhango wameelezea juu ya utayarifu wao wa kushirikiana na vyombo vya usalama nchini humo, kwa lengo la kuboresha usalama wa eneo hilo na nchi nzima kwa ujumla. Sheikh Ismail Ntawukuriryayo, Imamu wa Msikiti wa Ruhango amesema jamii ya Waislamu nchini humo inathamini usalama na amani ya nchi na kwamba daima imekuwa ikionyesha utayarifu wake wa kuzidi kushirikiana na vyombo vya usalama juu ya suala hilo.
Ameongeza kuwa, na hapa tunamnukuu: "Yale yote tuliyojifunza kwenye mkutano huu wa pamoja na vyombo vya usalama, tutayapeleka katika misikiti mingine kote nchini ili kuhakikisha kuwa jamii ya Waislamu wa Rwanda inafahamu kuwa jukumu la usalama sio tu la vyombo vya usalama, bali linahusu kila mmoja." Mwisho wa kunukuu.
Kwa upande wake, Francis Nkwaya, Naibu Kamishna wa Polisi katika Mkoa wa Kusini amepongeza Waislamu wa wilaya ya Ruhango kwa kuwa wenyeji wa mkutano huo na kuwataka viongozi wa dini hiyo waendelee na moyo huohuo. Amewataka wazidi kuwahamasisha wafuasi wa dini hiyo tukufu juu ya umuhimu wa usalama akisisitiza kuwa, wafuasi wa kila dini nchini humo wamekuwa wakitekeleza wajibu wao wa kufanya ibada kwa miaka 22 bila tashuwishi kutokana na usalama huo.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages