Breaking News

Your Ad Spot

Nov 24, 2016

SUDAN YAWATIA NGUVUNI VIONGOZI WANNE WAKUU WA UPINZANI

Serikali ya Sudan imewakamata viongozi wanne mashuhuri wa upinzani nchini humo akiwemo mwanasiasa mkongwe Sadiq Youssef.
Muungano wa upinzani unaoongozwa na Youssef umesema viongozi hao wa upinzani wamekamatwa ikiwa ni katika mwendelezo wa vyombo vya usalama kukandamiza wapinzani na wakosoaji wa serikali ya Rais Omar al-Bashir.
Mbali na Sadiq Youssef, wanasiasa wengine wa upinzani waliotiwa mbaroni na vyombo vya usalama ni Mohammed Dia al-Din, msemaji wa chama cha National Consensus Forces na makada wawili wa chama hicho cha upinzani, Manzar Abu al-Maali na Tareq Abdul Majid.
Maandamano ya madaktari Sudan
Haya yanajiri muda mfupi baada ya mgomo wa nchi nzima wa madaktari nchini humo kusitishwa kwa muda baada ya vyombo vya dola kuwaachilia huru madaktari wawili waliokuwa wametiwa mbaroni kwa tuhuma za kushiriki katika mgomo wa kuipinga serikali ulioanza tarehe 6 Oktoba mwaka huu.
Mbali na mgomo huo wa madaktari, wananchi wa Sudan wanaendelea na malalamiko yao dhidi ya kupandishwa gharama za nishati pamoja na hali ya kisiasa na kijamii nchini mwao.
Migomo na maandamano nchini Sudan yanafuatia machafuko na maandamano yanayoendelea katika pembe mbalimbali za nchi hiyo kupinga hali mbaya ya kijamii na kiuchumi na sera za serikali ya Rais Omar al Bashir. Maandamano hayo yameshika kasi zaidi baada ya serikali ya Khartoum kufuta ruzuku ya wananchi katika sekta ya nishati, suala ambalo limesababisha kupanda kwa bei ya bidhaa muhimu na ughali mkubwa wa maisha.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages