Zaidi ya wahajiri 240 wamefariki dunia au
kutoweka katika bahari ya Mediterenia huku wengine 580 wakiokolewa
kutoka kwenye boti zilizofurika wahajiri hao haramu.
Msemaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi
(UNHCR) Iosta Ibba amewanukuu watu wapatao 15 walionusurika na
kufanikiwa kufika salama Catania katika pwani ya mashariki ya Sicily
nchini Italia wakieleza kwamba boti waliyosafiria ilipinduka siku ya
Jumatatu ikiwa na watu 150 ndani yake.
Ibba ameeleza kuwa wahajiri hao walinusurika kwa kushikilia vipande
vya mabaki ya boti hiyo ya plastiki vilivyokuwa vikielea majini.
Manusura hao walibaki majini kwa saa kadhaa, baadhi yao wakisema ni muda
wa saa 10 kabla ya kuokolewa na meli moja ya mafuta.
Watu wengine 23 pia waliokolewa na meli nyingine ya mafuta siku ya
Jumanne baada ya boti waliyokuwa wakisafiria ikiwa na watu wapatao 122
kupinduka.
Eneo la bahari lililoko baina ya Libya na Italia limekuwa kivuko
hatari zaidi kwa wahajiri, ambapo kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa la
Uhajiri idadi ya watu waliofariki katika safari hizo hatari za baharini
mwaka huu imepindukia 4,270 kulinganisha na 3,777 katika mwaka uliopita
wa 2015.
Shirika la Kuwahudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR limeripoti
kuwa, aghalabu ya wahajiri wanaopoteza maisha katika ajali hizo za
boti za kuelekea barani Ulaya ni raia wa nchi za Kiafrika kama Somalia,
Sudan, Ethiopia na Misri.../
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269