Breaking News

Your Ad Spot

Mar 20, 2017

RAIS DK. MAGUFULI AWEKA JIWE LA MSINGI LA UJENZI WA BARABARA ZA JUU (INTERCHANGE) KWENYE MAKUTANO YA UBUNGO LEO JIJINI DAR ES SALAAM

Dar es Salaam
Rais Dk. John Magufuli, leo Machi 20, 2017 ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa barabara za juu kwenye makutano ya Barabara za Morogoro, Mandela na Sam Nujoma eneo la Ubungo Jijini Dar es Salaam, huku akitoa mwito kwa  Watanzaia kuunga mkono juhudi nzuri na muhimu kwa maendeleo, na kuachana na ushabiki usio na manufaa unaochochewa na baadhi ya watu kupitia mitandao ya kijamii na baadhi ya vyombo vya habari.

Sherehe za kuweka jiwe la msingi katika mradi huo zimefanyika kando ya makutano ya barabara hizo na kuhudhuriwa na Rais wa Benki ya Dunia Dk. Jim Yong Kim, Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli, Mawaziri wa Tanzania, Balozi wa China hapa nchini Dk. Lu Youqing, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu Prof. Norman Sigala King na viongozi wengine wa Wizara na Mkoa wa Dar es Salaam wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa huo Paul Makonda.

Ujenzi wa barabara hizo utagharimu Sh. Bilioni 188.71 ambapo kati yake Sh. Bilioni 186.725 ni mkopo wenye masharti nafuu kutoka Benki ya Dunia na Sh. Bilioni 1.985 zitatolewa na Serikali ya Tanzania, na mradi huo utakaochukua muda wa miezi 30 unatekelezwa kwa lengo la kupunguza msongamano wa magari katika jiji la Dar es Salaam.

Akizungumza katika sherehe hizo, Rais wa Benki ya Dunia Dk. Jim Yong Kim amempongeza Rais Magufuli kwa kazi nzuri anayofanya katika uongozi wake iliyomjengea sifa nzuri duniani kote.

“Nilivutiwa na hotuba za Mwalimu Julius Nyerere hasa aliposema bila uhuru hakuna maendeleo na bila maendeleo utapoteza uhuru wako, kwa maana hiyo Nyerere aliona kuwa maendeleo ndio njia pekee ya kulifanya Taifa kuwa imara na kujitawala na kuwawezesha watu kujua mwelekeo wa maisha yao.

“Nipo hapa kwa sababu viongozi wengi wa Afrika na wengine wengi duniani, wameniambia unatakiwa kwenda Tanzania, kuona kile anachofanya Rais Magufuli, ikiwemo kuzuia rushwa na kujenga uchumi wa nchi ambayo ni huru” amesema Dk. Jim Yong Kim.

Kwa upande wake Rais Magufuli ameishukuru Benki ya Dunia kwa kuunga mkono juhudi za maendeleo za Tanzania na ameahidi kuwa Tanzania itaendelea kushirikiana na benki hiyo kwa kuendelea kukopa na kulipa madeni yake.

Dk. Magufuli amesema ataendelea kutekeleza ahadi yake ya kukabiliana na msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam ambapo pamoja na kujengwa kwa barabara za juu katika makutano ya Ubungo, maandalizi yanaendelea kujenga njia ya barabara 6 za kuanzia Dar es Salaam hadi Chalinze Mkoani Pwani, kujenga kilometa 305 za reli ya kati kwa kiwango cha kisasa (Standard Gauge) kuanzia Dar es Salaam hadi Morogoro, kujenga bandari kavu katika eneo la Ruvu Mkoani Pwani na kujenga daraja la Salenda litakalounganisha Agha Khan na Coco Beach kupitia baharini.

Amewataka wakandarasi watakaojenga barabara za juu katika makutano ya Ubungo kuharakisha ujenzi huo, ikibidi kumaliza kabla ya miezi 30 na pia amewasihi wananchi watakaopata kazi katika mradi huo kuwa waaminifu na waadilifu wakati wote wa ujenzi.

“Tujielekeze katika masuala ya msingi na ya maendeleo, tuache kujielekeza katika udaku, tunapoteza muda mwingi katika masuala ambayo yanatupotezea muda” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.

Pamoja na kuweka jiwe la msingi Dk. Magufuli na Dk. Jim Yong Kim wameshuhudia utiaji saini wa miradi mitatu itakayopatiwa mkopo nafuu kutoka Benki ya Dunia ambayo ni mradi wa ujenzi wa miundombinu ya usafiri katika Jiji la Dar es Salaam, mradi wa kusambaza maji safi, mazingira na ukusanyaji wa maji taka, na mradi wa uendelezaji wa miji ya Arusha, Dodoma, Kigoma, Mbeya, Tanga, Mwanza na Mtwara, yote ikiwa na thamani ya Jumla ya Sh. Trilioni 1.74.

Rais Magufuli amesema pamoja na mkopo wa Shilingi Trilioni 1.74 Tanzania inatarajia kunufaika na mkopo mwingine wa Shilingi Trilioni 2.79 zitakazotumika katika miradi ya endelezaji bandari ya Dar es Salaam, umeme, gesi, kilimo, afya na elimu kwa Tanzania Bara na Zanzibar.

------->HABARI KATIKA PICHA<------
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Dk. John Pombe Magufuli na Rais wa Benki ya Dunia Dkt. Jim Yong Kim wakiwa wamepanda basi la mwendokasi huku wakibadilishana mawazo wakielekea Ubungo kuweka jiwe la Msing la ujenzi wa barabara za juu (Interchange) kwenye makutano ya Ubungo na Samu Nujoma, , Dar es Salaam, March 20,2017
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Dkt. John Pombe Magufuli akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda, kabla ya kuweka jiwe la Msingi la ujenzi wa barabara za juu (Interchange) kwenye makutano ya Ubungo na Samu Nujoma, jijini Dar es Salaam, March 20,2017
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Dkt. John Pombe Magufuli akimtambulisa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasilia Prof. Makame Mbarawa kwa Rais wa Benki ya Dunia Dkt. Jim Yong Kim walipokwenda kuweka jiwe la Msingi la ujenzi wa barabara za juu (Interchange) kwenye makutano ya Ubungo March 20,2017
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Dkt. John Pombe Magufuli akihutubia wananchi alipokwenda kuweka jiwe la Msing la ujenzi wa barabara za juu (Interchange) kwenye makutano ya Ubungo March 20,2017
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa Benki ya Dunia Dkt. Jim Yong Kim wakipata maelezo jinsi barabara za juu (Interchange) kwenye makutano ya Ubungo zitakavyokuwa baada ya kujengwa March 20,2017
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa Benki ya Dunia Dkt. Jim Yong Kim katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wa serikali baada ya kuweka jiwe la Msingi ujenzi wa barabara za juu (Interchange) kwenye Makutano ya Ubungo March 20,2017. PICHA ZOTE NA IKULU

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages