Breaking News

Your Ad Spot

May 26, 2014

COMPASSION KUTUMIA BILIONI 41.8 KWA MIRADI

Mkurugenzi wa shirika la Compassion Tanzania,Mchungaji Joseph Mayala alipokuwa akizindua miradi mbalimbali Iringa. (picha na Denis Mlowe)
======  ======  =======

Na Denis Mlowe,Iringa.

SHIRIKA la kimataifa la Compassion linalofanya kazi na madhehebu ya Kikristo nchini linatarajia kutumia zaidi ya sh. Bilioni 41.8 hadi Juni mwaka huu katika kutekeleza miradi yake ikiwemo kuwasomesha  wanafunzi 70,087 wanaosoma shule na vyuo mbalimbali ndani na nje ya nchi.
 
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa shirika hilo Joseph Mayala, wakati akizungumza katika ufunguzi wa nyumba ya mtoto Chris Kadege(3) iliyofadhiliwa kwa msaada wa shirika hilo kwa kushirikiana na Kanisa la Kianglikana Dayosisi ya Ipogoro mwishoni mwa wiki mjini hapa, alisema  kuwa miradi hiyo inalenga kutekeleza malengo ya maendeleo ya millennia (MDG) na dira ya taifa 2025.
 
Alisema kuwa mkazo mkubwa ukiwa ni kuwatoa na kuwakomboa watoto hao kutoka kwenye hali za umasikini wa Kiuchumi, kiroho, Kijamii, na Kimwili na hatimaye kuwawezesha kuwa watu wazima wanaoujua wajibu wao, na wanaojitosheleza.
 
 “Imekuwa kasumba ya watanzania waliowengi kulalamika bila kufanya kazi kwa bidii, maarifa na uadilifu hivyo ni lazima tuwe na mkakati na tunataka tuwe na kizazi sio cha wanung’unikaji na walalamikaji tunataka tuwe na kizazi chenye kutafuta suluhisho ufumbuzi wa matatizo na suala ya kuwasaidia watoto yatima ni jukumu letu sote kuanzia ngazi ya familia hadi taifa” alisema Mawala.

Aidha Mch.Mayala alisema kuwa malengo waliyonayo ni pamoja na kuendelea kutoa huduma kwa kushirikiana na makanisa yenye ushirika wenza katika misingi ya uadilifu,utu,na kuwa mawakili wema wa rasilimali za watoto na jamii na kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa katika vituo vyao vyote.
 
Alisema Watoto na vijana ni talanta na rasilimali kwa taifa ambayo Mwenyezi Mungu ametupa sisi Serikali, Makanisa na jamii kwa ujumla ili tuwekeze kwao kwa namna ambayo inafaa na inayotambua mpango mkamilifu wa Mwenyezi Mungu kwa kila mtoto mmoja mmoja ili afikie kule ambako Mungu alimkusudia. Watoto na vijana tulio nao leo ndio pekee wanaoweza kubadilisha chanya kesho ya Taifa letu kama tukiwaandaa na kuwasimamia kikamilifu.
 
Alisema shirika hilo linazidi kukua kwa kasi kutokana na kufanya kazi zake kwa uadilifu kwa kutekeleza miradi mbalimbali na taarifa zake kurudishwa makao makuu ya shirika hilo nchini Marekani hivyo kusababisha kuendelea kupata misaada zaidi. Aliongeza kuwa licha shirika hilo kumjengea nyumba mtoto Chris Kadege anayeishi katika mazingira magumu limewajengea watoto wanaolelewa na kanisa la Kianglikana dayosisi ya Ipogoron ukumbi  wa mkutano na madarasa mawili yenye thamani ya shilingi milioni 49 na nyumba iliyogharimu shilingi  milioni 7.8
                                                               
Alizitaja programu  mbalimbali zinazofanywa na shirika hilo ni kupamba na UKIMWI, Majanga, Afya , Watoto walio katika mazingira hatarishi na Miundombinu . Miradi mengine ni kutoa vifaa vya Mafunzo kwa watoto, Matibabu , Ujasiriamali , Elimu isiyokuwa rasmi, Elimu kwa Wazazi,  Maji na Usafi.    .
              
 “Kwa kuzingatia uadilifu huwa tunatoa taarifa kwa serikali kwenye ofisi mbalimbali zikiwemo ofisi za wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya sehemu ambazo huduma hii ipo kila robo mwaka na taarifa ya mwaka zikiwemo taarifa za wakaguzi wa hesabu wa nje (External Auditors) hivyo tunamshukuru Mungu kuwa mpaka sasa Shirika la Compassion International Tanzania limekuwa na mahusiano mazuri na kushirikiana na Serikali, makanisa na jamii ya watu wote wanaotuzunguka na kushirikiana nao katika malezi, makuzi na maendeleo ya kiujumla ya watoto na vijana” alisema Mayala.
 
Alisema katika Afrika Mashariki ukiondoa Tanzania shirika hilo lipo Rwanda, Kenya, Uganda na Ethiopia na tayari limezalisha wasomi wengi wakiwemo madaktari na wauguzi wahasibu, wanasheria na askari ambao kwa sasa wamekuwa tegemeo kubwa kutokana na ufadhili unaotolewa na shirika hilo.

Shirika hilo la compassion internation Tanzania lilianzishwa rasmi tarehe 30/4/1999 lengo ikiwa ni kuhudumia watoto wahitaji ili kuwatoa katika umasikini wa kiroho,kiuchumi,kijamii na kimwili na baadae lilianzisha ushirika wenza na baadhi ya makanisa ya kiinjili katika mikoa ya lindi ,mtwara,Iringa  na Arusha ambapo ndio makao makuu.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages