Breaking News

Your Ad Spot

May 19, 2015

KABURI LAFUKULIWA NA KUVULIWA SUTI, SOKSI NA VIATU NA KUTOKOMEA NAVYO

Kaburi likiwa wazi baada ya kufukuliwa.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani linawasaka watu wanaosadikiwa kuwa ni wezi ambao wamebomoa kaburi la marehemu Napegwa Kishaluli (75), mkazi wa Mailimoja Kibaha na kuutoa mwili wake kisha kuiba suti, viatu na soksi alizokuwa amevalishwa.

Habari za kipolisi kutoka mkoani Pwani  zinasema kuwa, marehemu alizikwa Aprili 20, mwaka huu lakini siku saba baadaye watu wasiojulikana walikwenda kaburuni na kulivunja kisha kulitoa jeneza wakidhani kulikuwa na mali kaburini kisha kumvua nguo zote marehemu wakidhani alikuwa na dhahabu.

Tukio hilo lilitokea Aprili 24, mwaka huu katika Kata ya Tangini jirani na Soko la Loliondo, habari zinasema baada ya mazishi kaburi hilo liliwekewa mlinzi kwa muda wa wiki moja kutokana na uvumi kuenea kuwa marehemu alizikwa na vitu vya thamani ukiwemo mkufu wa dhahabu.

Watu wa karibu na familia ya marehemu wamethibitisha kutokea kwa tukio hilo na wakasema kuwa baada ya mazishi ulikuwepo uvumi kwamba marehemu alizikwa na vitu vya thamani kama vile pete na mkufu wa dhahabu, kitu ambacho siyo kweli.

Akizungumza na mwandishi wetu, ndugu wa marehemu ambaye hakutaka jina lake kuandikwa gazetini kwa kuwa siyo msemaji wa familia, alisema baada kuzika walilazimika kuajiri mtu wa kulinda kaburi hilo la ndugu yao kwa wiki moja lakini siku moja baada ya mkataba kumalizika kaburi hilo lilivunjwa.

“Tuliweka mlinzi alinde kaburi hilo kwa wiki moja tukiamini litakuwa limekauka kwa sababu lilitengenezwa kwa zege. Tuliamini watu wenye nia mbaya watashindwa kulivunja  jambo ambalo limekuwa kinyume kwa vile baada ya muda huo kumalizika kaburi lilibomolewa ‘ubavuni’ na watu wasiojulikana ambao waliamini ndani ya kaburi kulikuwa na mali nyingi,” alisema.

Aliongeza kuwa baada ya kuvunja kaburi hilo wahalifu hao walilitoa jeneza nje, wakalifungua kisha kupekua ndani kwa kuligeuza na kuliweka tofauti na lilivyokuwa awali.Baada ya kuona hakukuwa na mali zozote waliamua kumvua marehemu nguo zote,  viatu na soksi alizovalishwa wakaondoka nazo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, ACP Jafari Mohamedi juzi alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na akaongeza kwamba watu hao hawajakamatwa.“Bado tupo kwenye uchunguzi na watakaobainika watachukuliwa hatua za kisheria,” alisema.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages