Breaking News

Your Ad Spot

Mar 1, 2016

CHANZO CHA UTAKFIRI KATIKA ULIMWENGU WA KIISLAMU SEHEMU YA (24) NA SAUTI

Picha ya kihistoria ya waasisi wa Uwahabi karne kadhaa zilizopita Picha ya kihistoria ya waasisi wa Uwahabi karne kadhaa zilizopita
Ni yangu matumaini kuwa hamjambo wapenzi wasikilizaji na karibuni kutegea sikio kipindi cha 24 cha makala yanayozungumzia chanzo cha utakfiri katika ulimwengu wa Kiislamu.
Katika kipindi kilichopita tuliangazia macho namna ambavyo Ibn Taymiyyah ambaye jina lake halisi ni Taqiyyud-Din Abul-Abbas Ahmad Ibn Taymiyyah, alijikita katika kuwatusi Ahlul-Bayti wa Mtume hususan Imam Ali (as) na kubuni hadithi bandia dhidi ya watukufu hao, huku akiwasafisha watu wa ukoo wa Abu Sufiyan sanjari na kudhoofisha hadithi sahihi na kinyume chake kuzifanya sahihi hadithi dhaifu katika kukabiliana na ubora wa familia ya Mtume (as). Kwa hakika kile kilichotawala katika Usalafi wa Ibn Taymiyyah ulikuwa ni Uislamu wa Bani Umayyah tu. Ni Uislamu ule ambao Bani Umayyah walikuwa wakiulingania, katika kuwachukia watu wa familia ya Mtume Muhammad (saw). Ni katika fremu hiyo ndio maana naye Ibn Taymiyyah akajikita tu katika kuunga mkono Uislamu huo sanjari na kuwapigia debe kwa kiasi kikubwa watu wa ukoo wa Abu Sufiyan, huku akiyasafisha maovu yao na kupambana wazi wazi na watu wa familia ya Mtume (saw) hususan Imam Ali (as) na watoto wake wema. Hii ni katika hali ambayo, Imam Ahmad Ibun Hanbali si tu kwamba alikuwa akiwapenda Ahlul-Bayti wa Mtume (saw), bali alijikita katika kueneza mitazamo na mafundisho yao matukufu baina ya Waislamu. Ndugu wasikilizaji mnapaswa kufahamu kwamba, Ibn Taymiyyah alisimama na kupambana na madhehebu zote za Kiislamu kwa kuwatuhumu Waislamu kuwa watu wa bidaa, ambapo aliwataja pia kuwa ni makafiri, na hivyo akawa amepandikiza mbegu ya unafiki na mfarakano baina yao. Hii ni katika hali ambayo katika maisha yake Imam Ahmad Ibn Hanbali, alijitahidi sana kuweka misingi ya pamoja katika kuiunganisha mirengo tofauti ya watu wa hadithi licha ya tofauti kubwa zilizokuwepo baina yao. Kiujumla ni kwamba, Ibn Taymiyyah aliasisi mrengo wa kufurutu ada katika uga wa itikadi ambapo athari yake hasi ilidhihiri katika karne ya 11 kupitia linganio la Muhammad Ibn Abdul-Wahhab, mwasisi mkuu wa Uwahabi. Mrengo huo wa kizushi wa Ibn Taymiyyah sanjari na kuimarishwa zaidi na wafuasi wa Uwahabi karne kadhaa baadaye, uliwekewa rasmi jiwe la msingi la kufurutu ada na ukufurishaji katika kipindi cha mwasisi wake Ibn Abdul-Wahhab, mambo ambayo yalienda sambamba na utekelezaji wa umwagaji mkubwa wa damu za Waislamu wa enzi hizo. Pamoja na kwamba Ibn Taymiyyah katika zama zake hakufanikiwa kuibua kivitendo tofauti na mpasuko baina ya Waislamu, lakini kwa upande wake Muhammad Ibn Abdul-Wahhab, aliweza kutumia mafundisho na fikra ghalati za kuibua farqa na fitina za shakhsia huyo (yaani Ibn Taymiyyah) na kwa uungaji mkono wa dola la Aal-Saud lililosimama kwa upanga chini ya himaya kamili ya Uingereza, kupandikiza mbegu hiyo chafu ya fitina baina ya umma wa Kiislamu na hivyo kuusababishia hasara na maafa makubwa katika ulimwengu wa Kiislamu. Mitazamo ya genge la Kisalafi ambalo liliwekewa jiwe la msingi katika karne ya 11 na Ibn Taymiyyah, ilisambaratika baada ya kufariki kwake dunia, licha ya juhudi kubwa zilizofanywa na wanafunzi wake pinde baada ya kufariki kwake dunia. Hata hivyo mitazamo hiyo iliibuka rasmi katika karne ya 12 kwa aina na utaratibu mpya kwa jina la Uwahabi. Jina la Uwahabi linatokana na mwasisi wa kundi hilo, Muhammad Ibn Abdul-Wahhab. Kinyume kabisa na watu waliomtangulia, Ibn Abdul-Wahhab aliweza kueneza mafundisho na fikra zake potofu katika maeneo ya Najdi na Hijazi (Saudia) kupitia nguvu ya kisiasa na uungaji mkono kamili wa Uingereza kwa upande mmoja na nguvu ya upanga kwa upande wa pili. Ni katika kipindi hicho ndipo itikadi za Usalafi wa kitakfiri zilishika kasi sanjari na kushuhudiwa mauaji ya kutisha dhidi ya Waislamu wa Kisuni na Kishia wa maeneo hayo.
*************************************
Muhammad Ibn Abdul-Wahhab, alizaliwa mwaka 1115 Hijiria, katika mji wa ‘Uyainah’ huku baba yake Sheikh Abdul-Wahhab, akiwa ni mmoja wa masheikh maarufu wa dhehebu la Uhanbali na pia kadhi wa mji huo. Uyainah ni eneo katika mji wa Najd ambao uko umbali wa kilometa 70 kutoka mji mkuu wa Saudi Arabia, Riyadh. Allamah Aaluusi, ambaye ni mmoja wa watu waliokuwa na misimamo ya kufurutu ada na mfuasi wa Muhammad Ibn Abdul-Wahhab anaeleza kuwa, katika mwaka ambao Sheikh Muhammad, alitangaza wazi itikadi zake, alikabiliwa na upinzani mkubwa kutoka kwa watu na maulama wa enzi hizo. Anaendelea kusema kuwa, muda fulani Sheikh Muhammad Ibn Abdul-Wahhab alielekea mjini Makkah kwa ajili ya kutekeleza ibada ya Hija, na baada ya hapo, akaelekea mjini Madina kwa ajili ya kujiendeleza kielimu. Akiwa mjini hapo, na bila ya kuwa na elimu ya kutosha, alianza kuwakataza Waislamu kwenda kuzuru kaburi la mtukufu Mtume Muhammad (saw) na kudai kuwa eti jambo hilo ni ushirikina. Baada ya kutoka mjini Madina, Ibn Abdul-Wahhab alielekea Najdi na kisha mjini Basra, Iraq. Watu wa mji wa Basra ambao tayari walikuwa wamepata habari juu ya itikadi potofu za shakhsia huyo yaani Ibn Abdul-Wahhab, walimfukuza mjini humo. Kwa hakika maisha ya Muhammad Ibn Abdul-Wahhab yaliyojaa matatizo mengi, yalienda sambamba na kuibua fikra za utakfiri ambazo zilisababisha mauaji ya watu wengi.
****************************************
Karne ya 12 Hijiria ambayo ni sawa na karne ya 18 na 19 Miladia, ilikuwa karne maalumu ambapo Waislamu walishuhudia matatizo chungu nzima. Hii ni kwa kuwa katika kipindi hicho kulishuhudiwa wimbi la ukoloni wa madola ya kibeberu dhidi ya nchi za Kiislamu. Uingereza ambayo kwa miaka mingi ilikuwa ikiikalia bara Hindi, ilitaka kuendeleza ukoloni na kujizatiti kwake katika eneo hilo kwa kutumia mabadiliko ya mitaala ya masomo. Kwa kutumia mbinu hiyo, Uingereza iliweza kujitanua na kuidhibiti jamii ya Kiislamu ya India na vizazi vya baadaye nchini humo. Huku hali ikiwa ni hivyo huko India, Ufaransa nayo chini ya uongozi wa Napoleon, ilizikalia kwa mabavu nchi za Misri, Syria na Palestina, nayo Urusi ya zamani sanjari na kutekeleza hujuma mtawalia dhidi ya Iran na dola la Othmania, ikafanya njama za kutanua wigo wake wa kisiasa na kijografia kupitia mikataba yake ya kikoloni katika nchi hizo.
Mfalme wa Othmania ambaye alikuwa amevaa vazi la Kisuni, alikuwa akipitia kipindi kigumu kufuatia kudhoofika utawala wake huku akikabiliwa na hatari kuporomoka kabisa utawala huo. Katika mazingira hayo, ulimwengu wa Kiislamu uliokuwa unakabiliwa kwa kiasi kikubwa na hatari ya kuporomoka, ulikuwa unahitajia sana umoja na mshikamano kwa ajili ya kukabiliana na changamoto hizo za mabeberu. Uislamu ulikuwa unahitajia nguvu ya pamoja ya Waislamu kwa ajili ya kuwaandalia uwezo wa kukabiliana na adui wao wa pamoja. Hata hivyo katika mazingira hayo hatari, Mawahabi si tu kwamba hawakusaidia kwa aina yoyote katika kuunda umoja wa Waislamu, bali ndio kwanza walipandikiza mbegu ya unafiki, farqa na uadui baina ya Waislamu, sanjari na kushirikiana bega kwa bega na wakoloni na hivyo kuwafungulia mlango wa kupenya zaidi katika nchi za Kiislamu, suala ambalo lilitoa pigo kubwa kwa Waislamu. Ni katika kipindi hicho hicho ndipo Muhammad Ibn Abdul-Wahhab, kwa kutumia misaada ya mtawala wa ukoo wa Aal-Saud kwa upande mmoja na msaada wa Uingereza kwa upande wa pili, akafanikiwa kueneza mafundisho na fikraza zake potofu katika ardhi ya Hijaz (Saudi aya leo).
Wapenzi wasikilizaji kitu kinachomtambulisha mtu msomi, ni athari zake za kielimu, au walimu na wanafunzi wanaojinasibisha na msomi huyo. Hata hivyo kwa upande wake Muhammad Ibn Abdul-Wahhab, kinyume na alivyokuwa mtangulizi wake, (yaani Ibn Taymiyyah), alipitia hali ngumu ya umasikini wa elimu na mali. Hii ikiwa na maana kwamba, Ibn Taymiyyah alikuwa mwandishi mkubwa huku akiwa na wanafunzi kama vile, Ibn Qayyim na Ibn Kathir, ambao walikuwa mashuhuri katika zama hizo. Hata hivyo Muhammad Ibn Abdul-Wahhab, si tu kwamba hakuwa mwandishi, bali pia hata vitabu na athari zinazonasibishwa kwake, zimeendelea kutiliwa shaka na maulama wa Kiislamu juu ya usahihi wake. Kwa hakika kitu ambacho kilifanikisha kuenea kwa fikra potofu za Ibn Abdul-Wahhab, haikuwa hoja zake za kielimu, hekima, wala busara, bali ilikuwa ni upanga, na nguvu ya kisiasa ya Aal-Saud na kadhalika Waingereza.
******************************************
Wapenzi wasikilizaji muda uliotengewa kipindi hiki umefika ukingoni. Msikose kuungana nami katika sehemu ya 25 ya mfululizo wa vipindi hivi. Mimi ni Sudi Jafar Shaban, hadi wiki ijayo ninakuageni kwa kusema: Kwaherini.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages