Breaking News

Your Ad Spot

Mar 1, 2016

KUGHAFILIKA BARAZA LA HAKI ZA BINADAMU LA UMOJA WA MATAIFA KATIKA UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YAKE

Kughafilika Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa katika utekelezaji wa majukumu yake
Kikao cha kila mwaka cha Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa kimeanza leo Jumatatu mjini Geneva, Uswisi na hafla ya ufunguzi imehudhuriwa na Katibu Mkuu wa UN, Ban Ki moon.
Mkutano huo wa kila mwaka unafanyika katika hali ambayo dunia inazidi kushuhudia ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu katika maeneo na mataifa mbalimbali. Mfano hai wa hilo ni kuendelea uvamizi na mauaji yanayoendeshwa na Saudi Arabia na nchi waitifaki wa Kiarabu pamoja na utawala haramu wa Israel dhidi ya wananchi wasio na hatia wa Yemen. Jinai ya hivi karibuni kabisa ya Saudia Arabia na waitifaki wao dhidi ya Yemen ni lile shambulizi la anga la wavamizi hao dhidi ya soko moja la umma karibu na mji mkuu, Sana'a ambapo watu kadhaa wakiwemo wanawake na watoto waliuawa.
Kituo cha haki za binadamu nchini Yemen hivi majuzi kilichapisha ripoti inayoweka wazi takwimu za kusikitisha kuhusiana na hasara, maafa na uharibifu uliosababishwa na hujuma za Saudi Arabia ndani ya muda wa takriban mwaka mmoja uliopita. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, tangu mwezi Machi mwaka jana hadi mwezi Januari mwaka huu, watu zaidi ya 8 000 wameuawa huko Yemen ambapo 236 kati yao ni watoto wadogo na 752 ni wanawake. Ni kutokana na maafa na uharibifu huo wa Saudia dhidi ya Yemen ndio maana shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International likataka jamii ya kimataifa isitishe uuzaji silaha kwa serikali ya Riyadh.
Mbali na vita vya Saudia dhidi ya Yemen, dunia pia inashuhudia ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu barani Ulaya hususan katika kadhia ya wakimbizi. Idadi kubwa ya wahajiri wamepoteza maisha kutokana na kuzuiwa kuingia katika baadhi ya nchi za Ulaya na wengine wamefariki dunia kutokana na kuwekwa katika mazingira ya kusikitisha barani humo. Hili linafanyika katika hali ambayo wakimbizi hao wanakimbia vita na machafuko ambayo yameanzishwa na nchi hizo hizo za Magharibi katika mataifa yao ya asili. Huku mkutano wa kila mwaka wa Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa ukifanyika, kadhia hiyo ya wahajiri inatarajiwa kutawala mijadala ya washiriki katika siku kadhaa zijazo.
Washiriki kwenye mkutano wa haki za binadamu mjini Geneva pia wanatarajiwa kuzamia kadhia ya Palestina na jinai zinazotendwa kila uchao na utawala haramu wa Israel dhidi ya Wapalestina. kiburi cha utawala huo kimekuwa kikitokana na ukimya wa jamii ya kimataifa hususan taasisi za haki za binadamu za Wamagharibi pamoja na Baraza la Haki za Binadamu la UN mbele ya jinai za Wazayuni.
Kwa maneno machache tunaweza kusema kuwa, utepetevu na mughafala wa Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa katika kutekeleza majukumu yake vimepelekea kuongezeka matukio ya ukiukaji wa haki za binadamu katika maeneo mbalimbali duniani.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages