Breaking News

Your Ad Spot

Mar 1, 2016

SISITIZO LA JAMII YA KIMATAIFA LA KUWEKEWA SAUDI ARABIA VIKWAZO VYA SILAHA

Sisitizo la jamii ya kimataifa la kuwekewa Saudi Arabia vikwazo vya silaha
Kutokana na kushtadi ukatili na unyama wa Saudi Arabia dhidi ya wananchi wa Yemen taasisi mbalimbali za kimataifa na shaksia wakubwa wametaka vikwazo vya silaha vipitishwe mara moja dhidi ya utawala wenye kupenda vita wa familia ya Aal Saud.
Katika kile kinachonekana kama ushaidi wa wazi kwamba Riyadh ni miongoni mwa nchi zenye kupenda vita Mashariki ya Kati, utawala huo umekithirisha manunuzi yake ya silaha kwa asilimia 279. William Hartung, mtaalamu wa masuala ya silaha katika kituo kinachofuatilia sera za kimataifa (CIP) ameandika makala ndefu akizungumzia mwenendo wa manunuzi ya silaha ya Saudia Araba. Anasema kati ya mwaka 2011 hadi 2015, Riyadh imeongeza mrundikano wake wa silaha mbalimbali kwa zaidi ya asilimia 275. Hartung anasema asilimia kubwa ya silaha hizo zinatoka Marekani na Uingereza.
Taasisi nyingine ya kimataifa iliyozungumzia kuongezeka bajeti ya silaha ya Saudi Arabia katika miaka ya hivi karibuni ni ile inayofuatilia misaada ya kiusalama maarufu kama SAMM. Taasisi hiyo imesema uagizaji silaha wa Saudi Arabia kutoka Marekani umeongezeka kwa asilimia 96 katika kipindi cha uongozi wa Rais Barack Obama ikilinganishwa na kipindi cha George W. Bush. Pia taasisi hiyo ya kimataifa imesema Wasaudi wasiopungua 2 500 wamepata mafunzo ya kijeshi nchini Marekani katika kipindi hicho.
Umoja wa Ulaya kupitia bunge lake umezitaka nchi wanachama kusimamisha uuzaji wa silaha kwa serikali ya Riyadh kutokana na silaha hizo kutumika kuwaua kinyama wananchi wasio na hatia wa Yemen. Takwa la kusimamishwa uuzaji wa silaha kwa Saudia pia limetolewa na Muungano wa mashirika na taasisi za kutoa misaada ya kibinadamu (Oxfam) ambao umesema Riyadh imepelekea hali ya kibinadamu nchini Yemen kuwa mbaya kupindukia. Oxfam imesema kwenye ripoti yake ya hivi karibuni kwamba viongozi wa dunia wanaokutana mwezi Aprili nchini Uswisi kujadili biashara ya silaha wanapaswa kupitisha kwa kauli moja vikwazo vya silaha dhidi ya Saudia na waitifake wake ambao wanaendeleza uvamizi na mauaji dhidi ya raia wa Yemen.
Saudi Arabia imeongeza bajeti yake ya silaha katika miaka ya hivi karibuni sambamba na kukithirisha vitendo vya uvamizi na uingiliaji wa mambo ya ndani wa baadhi ya nchi za Mashariki ya Kati kama vile Bahrain na Yemen.
Amnesty international ni taasisi nyingine ya kimataifa ambayo imetoa ripoti maalumu inayoonyesha uhalifu wa kivita na jinai dhidi ya binadamu inayofanywa na Saudi Arabia na waitifaki wake dhidi ya Yemen. Kwa mantiki hiyo, taasisi hiyo ya kutetea haki za binadamu imetoa wito wa kuchukuliwa hatua za haraka na kivitendo za kusimamisha uuzaji wa silaha kwa watawala wa Riyadh.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages