Na
Ally Daud-Maelezo
Serikali imefungia kituo cha tiba asilia cha
Foreplan kinachomilikiwa na Tabibu Juma Mwaka Juma kwa kudaiwa kukiuka masharti ya
kibali alichopewa kwa kujitangaza kuwa anatoa tiba za kisasa badala ya matibabu
ya asilia.
Akizungumza na Waandishi wa habari leo jijini Dar
es salaam Mwenyekiti Wa Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala Dk. Edmund
Kayombo amesema kuwa kituo hiko kimefutiwa usajili na hakiruhusu kutoa huduma
za tiba asilia na Tiba mbadala kwa jamii kwa kutokidhi masharti ya usajili na kufanya
kazi kinyume cha usajili wake.
“Kuanzia hivi sasa tumekifutia usajili kituo cha
tiba asili na tiba mbadala cha Foreplan kwa kukiuka masharti ya usajili na
hivyo hakiruhusiwi kutoa huduma kwa jamii
na watanzania kwa ujumla”, alisisitiza Dkt. Kayombo.
Aidha Dkt. Kayombo ameongeza kuwa vituo vingine
vilivyofungiwa kutoa huduma ni pamoja na Tabibu Abdallah Mandai wa Mandai
Herval Clinic na kituo cha Fadhaget Sanitarium Clinic kinachomilikiwa na tabibu
Fadhil Kabujanja.
Dkt. Kayombo aliendelea kwa kusema kuwa, ukiacha waliofungiwa
kutoa huduma pia vipo vituo vilivyofungiwa kwa miezi sita kila kimoja kama vile
tabibu Simon Rusigwa wa kituo cha Sigwa Herbal Clinic na Tabibu John Lupimo wa
kituo cha Lupimo Sanitarium Clinic.
Mbali na hayo Dkt. Kayombo amesema kuwa huduma za
tiba asili na tiba mbadala zinagusa zaidi maisha na afya za wananchi moja kwa
moja na hivyo sio vyema zikaachwa ziendeshwe kiholela bila utaratibu wa
kitaalamu na kimaadili.
“Kutokana na huduma hizo kutolewa kiholela, waratibu
wote mnatakiwa kufuatilia na kuchukua hatua za kisheria dhidi ya waganga wote
ambao hawajajisajili na kutoa taarifa katika Ofisi ya Msajili wa Baraza la tiba
asili na tiba mbadala kwa kila hatua iliyochukuliwa” aliongeza Dkt. Kayombo.
Aidha Dkt. Kayombo amesisitiza kwamba kila mtoa
huduma lazima asajiliwe yeye mwenyewe, wasaidizi wake pamoja na kituo chake cha
kutolea huduma kupitia ofisi za Mganga Mkuu wa Halmashauri husika.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269