Na Mwashungi Tahir-Maelezo -Zanzibar
Meneja wa
Biashara wa Kiwanda cha sukari Mahonda Bw Pronav Shah amekumbushia ombi
lao kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar la kukipatia Kiwanda maeneo
zaidi ya ardhi ili kuimarisha uzalishaji wa sukari katika kiwanda hicho.
Amesema
kiwanda hulazimika kusitisha uzalishaji wa sukari kutokana na upungufu
wa miwa na huku ikwalipa mishahara wafanyakazi bila ya kuzalisha na
kukipelekea kiwanda kuingia katika hasara.
Ameeleza
hayo Ofisini kwake Mahonda wakati Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo ya
Baraza la Wawakilishi ilipofanya ziara ya kutembelea kiwanda hicho
kuangalia mafanikio na changamoto zinazowakabili .
Bw Pronav
Shah ameieleza Kamati hiyo ya Baraza la Wawakilishi kuwa sehemu kubwa
ya mashamba ya kiwanda imevamiwa na wananchi wa kawaida kwa shughuli zao
ikiwemo ujenzi wa nyumba huku wakijua kuwa ni sehemu ya kiwanda na
kupunguza ukubwa wa shamba hilo.
“Sehemu
kubwa ya shamba la miwa hivi sasa limevamiwa na watu wa kawaida na
inasemekana wanaungwa mkono na baadhi ya viongozi wa shehia,”
amelalamika Meneja huyo.
Katika
hatua nyengine Meneja huyo wa Biashara ameiomba serikali kuwapatia bima
ili inapotokea ajali waweze kufidiwa gharama za ajali hiyo.
Amesema
iwapo serikali itawapatia bima itawasaidia hasa kwa vile mara kwa mara
mashamba ya miwa hushambuliwa na moto ambao haujulikani chanzo chake
licha ya juhudi za uchunguzi zinazofanwa na jeshi la Polisi.
Bw.
Pronav Shah ameshauri kuruhusiwa kupanua soko la kuuza sukari katika
soko la Tanzania Bara ambalo hivi sasa bei ni tafauti na Zanzibar ama
kuuza sukari yao Zanzibar kwa bei ya soko la Tanzania Bara.
Nae
mwenyekiti wa Kamati ya Fedha , Biashara na Kilimo Yussuf Hassan
ameutaka uongozi wa Kiwanda hicho kuendeleza uzalishaji wa sukari ili
kuwasaidia vijana kupata ajira na kufikia lengo la kujitosheleza kwa
bidhaa hiyo.
Ameuhakikishia
uongozi wa kiwanda hicho kuwa ombi lao la kupata ardhi zaidi kwa ajili
ya kuongeza mashamba ya miwa watalifikisha katika ngazi za juu ili
liweze kupatiwa ufumbuzi.
Amesema
Serikali inafahamu kuwa kufanikiwa kwa Kiwanda cha sukari cha Mahonda
itakuwa ni kivutio kwa wawekezaji wengine kuja kuwekeza Zanzibar. (P.T)
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269