Vyombo vya usalama nchini Misri vimewasweka
mbaroni mamia ya wafuasi wa harakati ya Ikhwanul Muslimin, kwa tuhuma za
kuitisha maandamano dhidi ya serikali.
Duru za habari zinaarifu kuwa, watu 229 wamekamatwa na polisi
ya Misri tangu Ijumaa iliyopita, kwa 'kuitisha na kuonyesha kuwa tayari'
kutekeleza wito wa maandamano uliotolewa na wanaharakati wa Ikhwan.
Habari zaidi zinasema kuwa, 78 miongoni mwao walikamatwa katika mji
mkuu Cairo, 104 kutoka mkoa wa Beheira Kaskazini na 21 kutoka eneo la
Minya, kusini mwa mji mkuu Cairo.
Alkhamisi iliyopita, idadi kubwa ya askari usalama na wajeshi wa
Misri walionekana katika miji mbalimbali ya nchi hiyo kwa shabaha ya
kukabiliana na maandamano ya wananchi dhidi ya serikali ya Rais Abdul
Fattah al-Sisi.
Tangu siku kadhaa zilizopita wanaharakati wa Misri walianzisha
kampeni kubwa katika mitandao ya kijamii wakitoa wito wa kushiriki kwa
wingi wananchi katika maandamano yaliyokuwa yamepangwa kufanyika Ijumaa
kwa jina la 'Mapinduzi ya Watu Maskini'. Sababu kuu ya wito huo ni
kulalamikia hali mbaya ya kiuchumi na kijamii nchini Misri.
Aidha misikiti ya mikoa yote 27 ya nchi hiyo ilifungwa mara tu baada
ya kumalizika swala ya Ijumaa kwa amri ya Waziri wa Wakfu wa nchi hiyo
ya kaskazini mwa Afrika.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269