Breaking News

Your Ad Spot

Dec 29, 2016

KUENDELEA JUHUDI ZA KUMSHAWISHI JAMMEH AKABIDHI MADARAKA KWA AMANI GAMBIA

Mivutano ya kisiasa ya baada ya uchaguzi wa rais nchini Gambia ingali inaendelea huku Mahakama Kuu ya nchi hiyo ikisubiriwa kutangaza uamuzi wake kuhusiana na malalamiko yaliyowasilishwa na Rais Yahya Jammeh ya kupinga matokeo ya uchaguzi huo.
Jammeh ametangaza kuwa hatokabidhi madaraka; lakini rais mteule wa nchi hiyo Adama Barrow ametoa wito tena kwa kiongozi huyo kumtaka angátuke madarakani na kueleza kwamba hata dola la kikoloni la Uingereza nalo lilikubali kukabidhi mamlaka ya nchi hiyo kwa njia ya amani.
Rais mteule wa Gambia ameongeza kuwa: "Wakati muda wa urais wa Jammeh utakapomalizika, mimi nitapaswa kula kiapo. Sitaki kushika hatamu za uongozi wa nchi kukiwa hakuna amani. Ninatoa wote kwa wananchi wote wapenda amani wa Gambia kufanya jitihada za kuhakikisha makabidhiano ya madaraka yanafanyika kwa njia ya amani.
Sambamba na hayo, Adama Barrow amesema kuna timu ya wataalamu ambayo ameipa kazi ya kufuatilia suala hilo na kwamba tayari ameunda tume maalumu ya kufanya maandalizi ya makabidhiano ya madaraka.
Rais mteule wa Gambia, Adama Barrow
Japokuwa kabla ya kufanyika uchaguzi wa rais nchini Gambia, wachambuzi walikuwa tayari wameshatabiri kwamba mivutano ya kisiasa itaibuka katika kipindi cha baada ya uchaguzi huo, lakini hatua Rais Yahaya Jammeh ya kutangaza kuwa amekubali kushindwa hata kabla ya kutangazwa matokeo rasmi ya uchaguzi iliwashangaza watu wote hususan waangalizi wa kimataifa.
Baada ya kupita siku chache tangu kiongozi wa upinzani kutangazwa mshindi, huku kila mtu akiutathmini uamuzi wa rais Jammeh kama hatua ya kufanikisha demokrasia nchini Gambia na kuhakikisha amani na uthabiti unatawala, katika hali isiyotarajiwa, kiongozi huyo alibadilisha ghafla msimamo wake na kutangaza kuwa hakubaliani na matokeo ya uchaguzi na hatokabidhi madaraka kwa rais mteule aliyechaguliwa na wananchi. Msimamo huo mpya wa Rais Jammeh uliwashangaza tena Wagambia na jamii ya kimataifa. Alingángánia msimamo wake huo na kutaka kuitishwa tena uchaguzi wa rais.
Nchi nyingi za eneo la magharibi mwa Afrika pamoja na taasisi za kimataifa zimechukua msimamo juu ya suala hilo kwa kumtaka Jammeh aheshimu matokeo ya uchaguzi na kukabidhi madaraka, lakini hatua zote za mashauriano zilizochukuliwa hadi sasa zimeshindwa kuwa na tija.
Viongozi wa Jumuiya ya ECOWAS katika kikao na Rais Yahya Jammeh
Hii ni katika hali ambayo hapo kabla pia Rais wa Gambia alikuwa akikabiliwa na lawama mbalimbali kwa sababu ya kutoheshimu haki za binadamu, kubinya uhuru wa kisiasa, kujenga mazingira ya vitisho na hofu na kutumia mabavu na mkono wa chuma dhidi ya wapinzani.
Hivi sasa wasiwasi umezidi kuongezeka wa kushtadi hali hiyo na kutumika tena mkono wa chuma na ukandamizaji dhidi ya wapinzani na hatimaye kuitumbukiza Gambia kwenye lindi la vita vya wenyewe kwa wenyewe. Na hii ni katika hali ambayo nchi za magharibi mwa Afrika zinapigania kurejesha amani na uthabiti katika kwa kupambana na makundi ya kigaidi yanayotishia amani na usalama wa eneo hilo. Hivi sasa juhudi za kidiplomasia na mashauriano ya jumuiya na taasisi za kisiasa za eneo zimeongezeka ili kumshawishi Jammeh abadilishe tena msimamo wake lakini jibu analotoa ni kwamba atakabidhi madaraka endapo tu Mahakama Kuu itamwamuru kufanya hivyo. Mahakama hiyo inatazamiwa kutangaza uamuzi wake mnamo siku kadhaa zijazo; lakini wapinzani wengi wanasema uamuzi utakaotolewa utakidhi matakwa ya Jammeh.
Rais Yahya Jammeh na Jaji wa Mahakama Kuu
Pamoja na yote hayo, juhudi za kisiasa na kidiplomasia zinaendelea kufanywa ili kumaliza mgogoro wa kisiasa nchini Gambia na kuhakikisha Rais Yahya jammeh anakabidhi madaraka kwa rais mteule Adama Barrow. Hii ni kwa sababu kuzuka vita vingine vya ndani katika eneo la magharibi mwa Afrika kunaweza kusababisha madhara mengi kwa nchi jirani na eneo zima kwa jumla…/

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages