Breaking News

Your Ad Spot

Dec 29, 2016

WAZIRI MKUU AHIMIZA KILIMO CHA MIHOGO NA ALIZETI

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa
Asema wanaotaka fedha wataipata shambani
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wakazi wa Ruangwa na mkoa mzima wa Lindi wachangamkie fursa ya kulima mihogo na alizeti kwa sababu mazao hayo yana uhakika wa soko.
Alitoa wito huo wakati akizungumza na wananchi wa vijiji mbalimbali vya wilaya ya Ruangwa, mkoani Lindi ambako anapita kuwasalimia wananchi wa jimbo lake na kuhimiza kazi za maendeleo. Waziri Mkuu yuko Ruangwa kwa siku nne kwa mapumziko ya mwisho wa mwaka.
“Nimekuja na fedha, wangapi wanataka kupata fedha?” alihoji Waziri Mkuu katika mikutano yake na kuitikiwa “Sisi” na umati wa watu walionyoosha mikono juu kuonesha kuwa wako tayari kupokea fedha hizo. Mikutano hiyo ilifanyika kwenye vijiji vya Namilema, Mbuyuni, Nandandara, Namkonjera, Muhuru, Chikundi, Chibula na Matumbu.
“Mnataka fedha siyo? Fedha iko shambani! Nimewaletea fursa ya mwekezaji anayetaka kununua mihogo yote katika mkoa huu,” alisema Waziri Mkuu na kusababisha kicheko kwa watu waliokuwa wakinyoosha mikono yao.
“Limeni mtu mmoja mmoja au jiungeni kwenye vikundi ili mpate ekari tatu hadi nne kwa sababu mna uhakika wa soko. Mwekezaji huyu anataka kununua mihogo yote na ya wilaya hii peke yake haitoshi kiasi ambacho anataka. Kwa hiyo tumekubaliana na wabunge wenzangu kwamba kiwanda hiki kitajengwa Nanjilinji ambako ni katikati ya mkoa ili iwe rahisi kusomba na kupeleka mazao hayo,” alisema.
Waziri Mkuu alisema eneo la Nanjilinji lililoko wilayani Kilwa, linafikiwa kwa urahisi na wakazi wote kutoka Kilwa, Nachingwea, Ruangwa, Lindi Vijijini na Liwale.
Akifafanua zaidi, alisema mwekezaji aliyepatikana (bado ni mapema kumtaja) yuko tayari kufuata mazao waliko wakulima na atakuwa akiwalipa hukohuko. “Yeye anachotaka ni mihogo ya kutosha, ndiyo maana nawasisitizia muanze kulima zao hili kwa wingi cha msingi mfuate kanuni bora za kilimo,” aliongeza.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu amewataka wakazi hao walime zao la alizeti kwa wingi kwa sababu amekwishapatikana mwekezaji wa kununua zao hilo na kwa bei nzuri.
“Nilipokwenda Singida nilikutana na mmiliki mmoja wa kiwanda cha kusindika mafuta ya alizeti akasema anahitaji kununua zao hilo kwa wingi kwa sababu inayozalishwa kule haitoshi. Ameshakuja hapa na kuangalia ardhi ya hapa amesema inafaa kwa zao hilo,” alisema.
“Yeye atawaletea mbegu na kila ekari moja inahitaji kilo tano. Ukivuna kila ekari unapata magunia 20 na kila gunia lina uwezo wa kutoa lita 20. Bei ya dumu mojala lita 20 ni sh. 60,000 kwa hiyo katika ekari yako moja una uhakika wa kupata sh. milioni 1.2. Hata ukitoa gharama ya kulima na palizi, bado huwezi kukosa walau sh. milioni moja kwa kila ekari.”
Alimwagiza Mkuu wa Idara ya Kilimo (Umwagiliaji na Ushirika) wa wilaya hiyo, Bi. Violeth Byanjweli afanye kazi ya kuratibu ni wakazi wangapi wana mashamba ya alizeti na wangapi wako tayari kuanzisha kilimo hicho ili mbegu zitakapoletwa iwe ni rahisi kuwasambazia huko waliko.
“Hiki kilimo ni cha miezi mitatu tu na palizi yake ni mara moja tu. Kwa hiyo mvua za Januari zikianza, changamkieni hiyo fursa na baada ya miezi mitatu kila mtu atakuwa na hela yake badala ya kusubiria korosho ambazo mnavuna mara moja kwa mwaka,” alisisitiza.



IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
ALHAMISI, DESEMBA 29, 2016.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages