Rais Yahya Jammeh wa Gambia
Gazeti la Le Monde la nchini Ufaransa
limefichua kuwa, Rais Yahya Jammeh wa Gambia anatumia ndege yake binafsi
kufanya magendo ya silaha na vitui vingine katika kona mbalimbali za
dunia.
Gazeti hilo limeandika hayo katika
toleo lake la leo Jumapili na kuwanukuu maafisa wa uwanja wa ndege wa
Gambia wakisema kuwa, Jammeh ambaye ameitawala nchini hiyo ya magharibi
mwa Afrika kwa zaidi ya miaka 22 kabla ya kushindwa kwenye uchaguzi wa
hivi karibuni, anatumia ndege yake binafsi kufanya magendo kama vile ya
silaha, mihadarati na almasi.
Wafanyakazi wa Uwanja wa Ndege wa
Banjul, mji mkuu wa Gambia wamenukuliwa na gazeti la hilo la Ufaransa
wakisema kuwa, wameshuhudia ndege binafsi ya Yahya Jammeh ikisafirisha
bidhaa kwa siri nyakati za usiku na hakuna mtu yeyote aliyethubutu
kupekua mizigo au wasafiri wa ndege hiyo.
Mwaka 2001 pia, kundi moja la wachunguzi
wa Umoja wa Mataifa ambao walitumwa kufanya uchunguzi kuhusu matukio ya
Liberia walisema wana wasiwasi ndege binafsi ya Rais Yahya Jammeh wa
Gambia ilitumika kumtumia silaha Charles Taylor, rais wa zamani wa
Liberia.. Ikumbukwe kuwa mwaka 2012, Taylor alihukumiwa kifungo cha
miaka 50 jela baada ya kupatikana na hatia ya kufanya jinai dhidi ya
binadamu nchini Liberia.
Habari kuhusu magendo hayo yanayodaiwa
kufanywa na Rais wa Gambia zimesambazwa wakati huu ambapo Yahya Jammeh
amekataa matokeo ya uchaguzi yaliyompa ushindi mpinzani wake. Hadi hivi
sasa viongozi wa nchi za Afrika wameshindwa kumshawishi Yahya Jammeh
aachie madaraka kwa amani.
No comments:
Post a Comment
Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269