Breaking News

Your Ad Spot

Sep 18, 2017

PROF. MBARAWA: MNAOTUMIA MITANDAO VIBAYA JIANGALIENI, IPO SIKU MTALIA MTAKAPONASA KWENYE MKONO WA SHERIA

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa kwanza kushoto), akikagua jenereta linalowezesha mnara wa Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), katika eneo la eneo la Gairo Hill, wilayani Gairo, Mkoani Morogoro. Wa kwanza kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Siriel Mchembe.
-----------------------------------
NA MWANDISHI MAALUM, MOROGORO
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amewaonya wananchi kujiepusha na matumizi mabaya ya mitandao ya mawasiliano ili wasingie katika janga la kushughulikiwa na sheria kali inayodhibiti matumizi hayo mabaya ya mitandao.

Amesema, wakati jitihada zinaendelea kufanyika kuhakikisha huduma za mawasiliano ya simu kuwa bora zaidi na pia kuwafikia Watanzania wengi, baadhi wamekuwa wakitumia mitandao vibaya badala ya kuitumia kwa ajili ya kutafuta maendeleo.

"Wanaotumia mitandao hii vibaya, pamoja na kupata hasara, lakini ni vema wakaacha mara moja tabia hiyo vinginevyo watajikuta wameingia katika janga la kushughulikiwa na sheriaa kali ambazo tayari zipo kwa ajili ya kudhibiti matumizi hayo mabaya ya Mitandao", alisema prof. Mbarawa.

Pia amezita kampuni za simu nchini kuhakikisha mawasiliano ya simu yanapatikana wakati wote katika ubora unaotakiwa ili kuwawezesha wananchi kupata huduma inayowiana na thamani ya fedha wanayolipa.

Akikagua na kuzindua minara ya simu ya kampuni za TTCL, VODACOM, HALOTEL, na TIGO katika Wilaya ya Gairo mkoani Morogoro, Profesa Mbarawa amesema Serikali itaendelea kushirikiana na kampuni za simu kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa wote UCSAF ili katika kipindi cha miaka mitatu ijayo sehemu zote za Tanzania ziwe zimefikiwa na huduma ya mawasiliano ya simu ya uhakika.

"Tumieni mawasiliano ya simu kufanya biashara, kuboresha huduma za jamii kama elimu na habari ili kukuza ustawi wa maisha yenu", amesema Profesa Mbarawa.

Amezungumzia umuhimu wa kampuni za simu kujenga minara katika maeneo mapya na kukarabati minara ya zamani ili kuwezesha mawasiliano kuwa katika ubora maeneo yote ya nchi.

Amewataka wakazi wa vijiji vya Letugunya, Leshata na Chakwale kutumia fursa ya upatikanaji wa mawasiliano kuongeza uzalishaji wa mazao na kuyauza kwa bei nzuri na hivyo kukuza uchumi wao.

Kwa upande wake Mtendaji mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa wote Mhandisi Peter Ulanga amemhakikishia Waziri Profesa Mbarawa kuwa  mfuko huo umejipanga kukamilisha miradi yote kwa wakati na kufanya uhakiki wa takwimu za mawasiliano nchi nzima ili kubaini maeneo ambayo yana changamoto kubwa ya mawasiliano na kuyatatua.

Mkuu wa Wilaya ya Gairo Siriel Mchembe  amemshukuru Waziri Mbarawa kwa kuboresha huduma za mawasiliano katika Wilaya hiyo na kumhakikishia wananchi watailinda miundombinu hiyo ili idumu kwa muda mrefu.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages