Breaking News

Your Ad Spot

Apr 5, 2018

URAFIKI WA TANZANIA,CHINA NI WA DAMU,LAZIMA UDUMISHWE NA KULINDWA-BALOZI MAHIGA

*Balozi wa Wang Ke aongoza Jumuiya ya marafiki wa China ,Tanzania kuwakumbuka waliopoteza maisha wakati wa ujenzi wa reli ya Tazara


Na Said Mwishehe,Globu ya jamii


 SERIKALI ya Tanzania imeungana na Jamhuri ya Watu wa China katika kumbukumbu ya vifo vya Wachina 70 waliofariki wakati wa ujenzi wa reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA).

Watanzania waliongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Kikanda na Afrika Mashariki, Balozi Dk. Augustino Mahiga huku ikiwakilishwa na Balozi wao nchini, Wang Ke. Kumbukumbu hiyo, imeandaliwa na Jumuia ya Marafiki wa Tanzania na China ambayo Mwenyekiti wake Dk. Salim Salim na Katibu wake ni Joseph Kahama.

Kabla ya kuweka mashada kwenye makaburi kwenye makaburi ya wachina hao ambao wengi wao ni wataalamu na wahandisi katika ujenzi wa reli, ilitolewa historia fupi ya vifo vyao.

Akizungumza baada ya kuweka mashada, Balozi Mahiga alisema ujenzi wa reli hiyo ulithibitisha urafiki wa kutoka moyoni kati ya nchi hizo mbili na kufafanua ujenzi wake ulifungua milango kwa China kujenga viwanda vingine kama UFI na Kiwanda cha Nguo cha Urafiki.

"Wakati wa ujenzi huu damu zilimwagika, wachina wamepoteza maisha na wengine wamebaki na ulemavu wa kudumu...hivyo urafiki wetu sisi na China ni wa damu," amesema.


Naye, Balozi Wang amesema nusu ya karne iliyopita, kupitia ombi la Rais wa Tanzania, Julius Nyerere na Rais wa Zambia, Kenneth Kaunda, viongozi wa kizazi cha China, Mwenyekiti Mao Zedong na Waziri Mkuu, Zhou Enlai walifanya maamuzi ya kimkakati na kihistoria kusaidia ujenzi wa TAZARA.

"Wafanyakazi na mafundi Wachina 50,000 waliitikia wito wa taifa na waliungwa mkono na wenzao kutoka Tanzania na Zambia, walishinda vigumu na vikwazo vingine kumalizia ujenzi wa TAZARA yenye urefu wa kilomita 1,860 ndani ya miaka sita na kuufanya kuwa  mradi wa kihistoria wenye umaarufu duniani,"alisema.

Amesema wafanyakazi na mafundi 65  Wakichina walipoteza maisha na walizikwa katika ardhi ya Afrika mbali na nyumbani kwao.

"TAZARA imekuwa ikifahamika kwa dunia kama reli ya ukombozi iliyowasaidia watu wa Afrika kupata Uhuru na Ukombozi...na pia reli ya urafiki ikiwakilisha urafiki wa ndani kati ya Wachina na Waafrika,"amesema.

Kwa upande wa Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Mfuko wa Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku amesema ipo haja kwa Tanzania na China kuendelea kudumisha urafiki wao.

"Wakati ule Mwalimu Nyerere kabla ya kwenda kuomba China watujengee reli alianza kuomba kwa nchi moja ya Magharibi sihitaji, anaetaka kuijua aje nitamnong'oneza. Nchi hiyo ilimjibu Nyerere hivi; ujenzi wa reli ya Tanzania na Zambia upitie Zanzibar. Nyerere akaondoka tukaenda China na baada ya kufika huko Mwalimu ikabidi aongee na waziri mkuu wa nchi hiyo, Zhou Enlai.

"Tena wakati anaomba hakwenda moja kwa moja alizunguka lakini hakujibiwa chochote ila wakati tunataka kuondoka tulienda kuaga kwa Rais wa China ambaye alikubali ombi letu. Kwa hiyo huu ni urafiki wa damu,"amesema.
 Mnara wa Makaburi ya Wachina waliokuwa wakijenga Reli ya Tazara  ambao walifariki wakati wa ujenzi wa reli hiyo miaka zaidi ya 40 iliyopita.
 Waziri wa Mambo ya Nje Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Balozi  Agustine Mahiga akitoa heshima  na Balozi wa China Nchini Tanzania, Wang Ke, kwenye Mnara wa makaburi ya Wachina waliofkuja kutengeneza Reli ya Tazara
 Waziri wa Mambo ya Nje Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Balozi  Agustine Mahiga akiwa na Balozi wa China Nchini Tanzania, Wang Ke, wakiweka mashada kwenye moja ya kaburi la wakandarasi waliofika nchini kujenga reli ya Tazara
 Waziri wa Mambo ya Nje Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Balozi  Agustine Mahiga  akihutubia Viongozi na wakazi wa Jiji la Dar es Salaam waliofikakatika sherehe ya kitamaduni ya watu wa china ya kuwakumbuka mafundi waliojenga reli ya Tazara.
  Balozi wa China Nchini Tanzania, Wang Ke, akihutubia na kutoa historia fupi ya ushirikiano wa Tanzania na China ulivyoasisiwa na Mwalimu Nyerere.
 Waziri wa Katiba na Sheria , Profesa Paramagamba Kabudi akiweka maua kwenye kaburi la wataalamu wa kichina waliokuwa wanajenga reli ya Tazara.
 Kibao kinacho elezea utambulisho wa Makaburi ya Wataalam wa Kichina Gongolamboto
 Katibu  wa Mfuko wa Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku akieleza namana Mwalimuj Nyerere alivyoweza kuomba reli kwa kiongozi wa China Mau Sentum
  Waziri wa Mambo ya Nje Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Balozi  Agustine Mahiga  na  Balozi wa China Nchini Tanzania, Wang Ke, pamoja na Viongozi wengine wakiwa wamesimama nyimbo za Taifa za mataifa yote mawili zilivyokuwa zikiimbwa.
 watu waliofika katika Sherehe za utamaduni za kuwakumbuka Wataalamu na Wakandarasi walikuwa wanjenga reli ya Tazara  kutoka china  wakitoa heshima zao kwenye mnara wa kaburi hilo
Baadhi ya Wazee walioshiriki kujenga Reli ya Tazara kwa kushirikiana na Wachina miaka 40 iliyopita.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages