Breaking News

Your Ad Spot

Feb 6, 2013

MAUAJI YA KIMBALI YANAWEZA KUTOKEA NCHI YOYOTE HATUA ZA KUDHIBITI ZISIPOCHUKULIWA

Washiriki wakiwa kwenye semina hiyo
 Na Mwandishi Maalum, NEW YORK
Kauli za uchochezi, chuki, ubinafsi,  ubaguzi kwa  misingi  ya rangi, dini, kabila,  na kutengana    ni  baadhi ya viashiaria ambavyo kama havitatambuliwa mapema na kudhibitiwa  ipasavyo vinaweza kuitumbikiza nchi yoyote ile katika hatari kubwa ya mauaji ya kimbari.
 “ Ni wajibu basi wa kila serikali   na kila raia kuwa macho na viashiria hivyo hasa ikizingatiwa kwamba mauaji  aina hii  huwa yazuki ghafla    la hasha, maandalizi yake ni ya muda mrefu, yanakuwa na viongozi wake na yanapangwa”.
Hayo yameelezwa na  Balozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Tuvako Manongi, wakati alipokuwa akifungua semina ya siku mbili kuhusu Uzuiaji wa Mauaji ya Kimbari  na   Wajibu wa kulinda Raia.
Semina hiyo  imeandaliwa na  Ofisi ya Mshauri Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu  Uzuiaji wa Mauaji ya Kimbari ( OSAPG) kwa kushirikiana na  Taasisi ya Mafunzo na Utafiti ya Umoja wa Mataifa ( UNITER) na imewahusisha wataalamu wa sheria, na haki za binadamu  kutoka Balozi mbalimbali na Asasi zisizo za Kiserikali.
Balozi Manongi, amewaeleza washiriki wa semina hiyo ambayo madhumuni yake   ni kujenga  uwezo na uelewa kuhusu  mauaji ya kimbari,  vyanzo vyake,  namna ya kubaini mapema viashiria  hatarishi na ukusanyaji wa  taarifa za awali na wajibu wa kulinda raia, kwamba mauaji ya kimbari yana mazingira yake.
Kwa hiyo, anasema Balozi  mahali pa kuanzia  daima ni kuielewa dhana nzima na mazingira ya mauaji  ya kimbari, “tunahitaji kuelewa kwa nini yanatokea na mahusiano yake na  vuguvugu za chini kwa chini,  kama  vile migogoro ya kugombania madaraka,  rasilimali,  hadhi ya uraia na haki zitokanazo na hadhi hiyo”.
“Kwa bahati nzuri, tunaweza kuzuia mauaji  haya na  mengine ya aina yake, kwa sababu kama nilivyosema mwanzo hayaibuki tu ghafla yana mazingira yake.  Masuala  kama vile misingi ya dhaifu wa kiutawala,  udhaifu wa utawala wa sheria  au kutokuwapo kabisa kwa utawala wa sheria ni  viashiria vingine vinavyoweza kuaanda mazingira ya mauaji ya kimbari na maujaji ya halaiki”.  Akasisiza Balozi.
Na kuongeza kuwa mauaji ya hayo hutanguliwa na uhalifu mwingine kama vile ubaguzi na kutengana. “Kama tunahitaji kuyashinda mauaji ya kimbari tunatakiwa kuwa macho na viashiria vya aina hii”.  
Aidha akaeleza kuwa  ,  kila serikali na kila raia anaowajibu mkubwa wa kuzibaini dalili za kuzuka kwa machafko,  chuki, na uchochezi dhidi ya aina yoyote ya ubaguzi wa rangi, kabila au dini na kutoa taarifa kwa taasisi  zinazohusika ili hatua ziweze kuchukuliwa mapema.
 “ Tunahitaji pia kuwa na misingi mizuri ya kuweza kuzigundua dalili hizo  mapema  hii ni pamoja na kuweza kutambua wapi au eneo gani la nchi pana dalili za  kutokea kwa machafuko”. 
Akasema  Afrika  imejifunza mengi kutokana na  mauaji  ya kimbari yaliyotokea Rwanda na kwamba   imejiweka mikakati mbalimbali  ikiwa ni pamoja na kuwa na chombo cha kubaini mapema kuwapo kwa dalili za machafuko  na kusisitiza  pia kwamba Jumuiya ya Kimataifa nayo inayowajibu mkubwa wa kukabiliana na mauaji hayo kwa kuyadhibiti mapema kabla hayajatokea.
Aidha Balozi Manongi ameeleza pia kwamba Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai ( ICC) na mahakama maalumu za kimataifa  kama  zile za ICTR na ICTY   ni vyombo ambavyo vinatakiwa kuwa sehemu ya mwisho kabisa   katika mchakato mzima wa uzuaji wa mauaji ya Kimbari.
Awali akimkaribisha Balozi kufungua Semina, hiyo, Mshauri Maalum wa Katibu Mkuu Bw. Adama Dieng ameeleza kwamba hakuna nchi inayoweza kujidai kwamba haitakuwa mhanga wa mauaji ya kimbari.
Akasema kwamba udhibiti wa uhalifu huo unachangamoto nyingi zikiwamo za rasimali na utashi wa kisiasa wa viongozi kukubali  au kukiri mapema  kwamba kuna tatizo katika nchi zao.
Akabainisha kwamba ni wajibu wa serikali kuzuia kutokea kwa mauaji ya kimbari kwa kujiwekea misingi bora ya utawala wa sheria, kuwa na mifumo ya sheria na mahakama zinazofanya kazi na kutimiza wajibu wake ipasavyo na kubwa zaidi wananchi wenye wawe na wajibu wa kuishi kama jamii moja  na kuvumiliana.
 Bwana Adama Dieng ambaye pia amewashi kufanya kazi katika Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya  Rwanda  iliyoko  jijini Arusha nchini Tanzania, amesema  anatiwa hofu na baadhi ya mambo yanayotokea katika baadhi ya nchi hivi sasa, akitolea mfano wa  Kundi la Boko Haramu , kundi ambalo limekuwa likiendesha mauaji ya raia wasiokuwa na hatia nchi  Nigeria.
Akaongeza kuwa  makundi ya aina hiyo ni  mengine yenye silaha ni viashiria vya kutoweka kwa amani na dalili za kutokea kwa mauaji ya kimbari au  halaiki, na kwamba  makundi ya aina hiyo na dalili nyingine za aina yoyote ile zinatakiwa kushughulikiwa na kudhibitiwa wa nguvu zote.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages