Breaking News

Your Ad Spot

Aug 7, 2014

UKAWA WAHUDHURIA BUNGENI.....

  • Hotuba ya Sitta gumzo, zaidi watarajiwa
  • Kamati zaanza kujadili Sura ya 12 ya Rasimu 
NA WAANDISHI WETU, DODOMA
MPASUKO miongoni mwa wajumbe wa kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), umezidi kushika kasi huku baadhi wakiamua kuasi na kuhudhuria vikao vya Bunge Maalumu la Katiba.

Kundi la UKAWA, ambalo limesusia kushiriki vikao vya bunge hilo, linaundwa na wajumbe kutoka vyama vya CHADEMA, NCCR-Mageuzi na CUF, ambapo jitihada za makundi mbalimbali nchini, wakiwemo viongozi wa dini kuwataka kurejea bungeni na kushindana kwa hoja, zimeonekana kugonga mwamba.
 
Hata hivyo, kuna madai ambayo mpaka sasa yameshindwa kuthibitishwa ama kukanushwa na kundi hilo kuwa, wamekuwa wakiwezeshwa na taasisi fulani za nje kwa lengo la kukwamisha mchakato wa kuwapatia Watanzania Katiba Mpya.

Imebainika kuwa baadhi ya wajumbe wanaounda kundi hilo, wameanza kujisajili mmoja baada ya mwingine kurejea bungeni, huku usiri mkubwa ukitawala. Hatua hiyo imetokana na tishio lililowekwa na viongozi wa UKAWA kuwa wajumbe watakaosaliti watakiona cha moto.

Miongoni wa wajumbe hao ni Leticia Nyerere (Viti Maalumu-CHADEMA), ambaye jana alifika ofisi za Bunge mjini hapa kujisajili tayari kwa kushiriki vikao hivyo.

Mapema wiki hii, Leticia alikaririwa akisema kuwa, anajali maslahi ya taifa kwanza na kwamba, kushiriki ama kutoshiriki kwenye bunge hilo kutategemea maamuzi ya viongozi wake.

Jana, mbunge huyo alionekana katika viunga vya viwanja vya Bunge akienda kujisajili, lakini aligoma kuzungumza baada ya kutakiwa kueleza sababu za kupuuza agizo la viongozi wake wa UKAWA.
 
Jitihada za waandishi wa habari kumbana mbunge huyo hazikuzaa matunda, kutokana na muda wote kuzungumza na simu yake ya mkononi huku akitokomea.

Mbali na Leticia, mwingine ambaye anadaiwa kuwa tayari amejisajili kuhudhuria vikao hivyo ni Mbunge wa Maswa Magharibi (CHADEMA), John  Shibuda.

Habari zaidi zimedai kuwa, Shibuda ambaye siku zote amekuwa mstari wa mbele kutetea maslahi ya taifa, alijisajili juzi asubuhi licha ya kuwa hajaonekana kwenye vikao vinavyoendelea.

Hata hivyo, jitihada za kumpata Shibuda kuzungumzia suala hilo hazikuweza kufanikiwa kwani hata alipotafutwa kupitia simu yake ya kiganjani, ilikuwa ikiita bila kupokewa kabla ya muda mfupi kuzimwa kabisa.

Kamati zaanza kazi
Wajumbe wa bunge hilo jana walianza vikao vya kamati kujadili sura 12 za Rasimu ya Mabadiliko ya Katiba huku hali ya utulivu na maelewano ikitawala.

Baadhi ya wajumbe wamesema hali hiyo inaongeza matumaini kuwa, kazi ya kuandaa Katiba Mpya ya Watanzania iliyo bora itafanyika kwa umakini mkubwa.

Abdalah Bulembo, alisema vikao vimeanza katika hali ya utulivu na Watanzania wategemee Katiba Mpya bora na yenye kujali maslahi ya wanyonge.

Alisema wajumbe wamekuwa na ari kubwa na hotuba ya Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta aliyoitoa juzi wakati wa ufunguzi wa mkutano huo, imewaweka sawa kimawazo na kuwafumbua macho walio wengi, hasa kutokana na kauli za uchochezi na ghiliba zinazofanywa na UKAWA.

‘’Katiba bora na yenye kujali maslahi ya wanyonge itapatikana bila wachache wenye malengo na mitizamo binafsi. Hotuba ya Sitta imezidi kuwafumbua watu macho na sasa utulivu na umakini kwa wajumbe wote ni mkubwa,” alisema.

Kuhusu upigaji kura ili kupata theluthi mbili kila upande wa Jamhuri katika maamuzi ya kupitisha Sura za Rasimu, Bulembo alisema hilo si tatizo na kwamba theluthi mbili itapatikana.

Hata hivyo, alisema iwapo hilo litashindikana kutoka kila upande, wajumbe wamekamilisha kazi ya kufanya marekebisho na wananchi ndio watakuwa waamuzi wa mwisho.

‘’Tusitumie unajimu katika upatikanaji wa hizo theluthi mbili, wacha tumalize kazi tuliyotumwa na kama kuna lolote, wananchi wapo wataamua nini cha kufanya wakati wa kupiga kura,” alisema na kuongeza: 

“Watanzania wengi wanatambua nani anafanya nini katika kulinda na kudumisha taifa. Hawa wenzetu wamekuwa na ugomvi na CCM, lakini hii Katiba si ya CCM, ni ya wananchi, hivyo wanapaswa kuweka pembeni tofauti hiyo na kuweka mbele maslahi ya wananchi.’’

Naye Mansour Sharif, alisema upigaji wa kura si suluhisho katika kupata katiba iliyo bora kwani, bado wananchi wana nafasi katika kuangalia utungaji huo.

Alisema siku 60 walizopewa na Rais ni siku muhimu katika kufanya kazi hiyo ya wananchi na kamwe wananchi wasipotoshwe kuwa kazi hiyo haitawezekana.

Stephen Ngonyani, alisema kuna umuhimu wa kuanzisha utaratibu wa kutoa Katiba kwa wananchi mara inapopatikana ili waweze kuisoma na kuelewa kabla ya kufanyiwa marekebisho.

Alisema kwa sasa hali hiyo imejitokeza kwa wananchi walio wengi kutoijua Katiba Katiba ya sasa kikamilifu hivyo kuwa rahisi kupotoshwa.
WAJUMBE  wa Bunge Maalumu la Katika ambao pia ni Wabunge wa Bunge la Tanzania, Letcia Nyerere (Viti Maalumu -CHADEMA) na Mbunge wa Korogwe Vijijini, Stephen Ngonyani 'Profesa Majimarefu', wakiwasili Viwanja vya Bunge, Dodoma, jana.
----------------------------------
Na Happiness Mtweve, Dodoma
WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda, ameagiza watendaji kuhakikisha wanabadili fikra za wafugaji ili kuwawezesha kuendesha ufugaji wa kisasa na wa kibiashara, badala ya kuendelea na ule uliozoeleka, ambao hauna tija kubwa katika kukabiliana na umasikini.

Alitoa agizo hilo jana wakati akizindua mashindano ya Maonyesho ya Mifugo, ambayo kitaifa yanafanyika Dodoma katika viwanja vya Maonyesho ya Nanenane vilivyopo Nzuguni mjini hapa.

Pinda alisema ni lazima wizara ibadili fikra za wafugaji kwa maendeleo ya taifa.

Alisema iwapo agizo hilo litasimamiwa kwa umakini kwa kutoa elimu ya ufugaji bora na wa kisasa kwa wafugaji nchini, itawawezesha wafugaji kujikwamua na umasikini na kuchangia kwa kiasi kikubwa pato la Taifa.

Alifafanua kuwa bado hitaji la mifugo bora hapa nchini ni changamoto kubwa licha ya Tanzania kuwa na idadi nyingi ya mifugo, lakini pia mchango wake kwa pato la Taifa ni mdogo.

Waziri wa Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, Dk. Titus  Kamani, alisema kwa sasa wamekamilisha ujenzi wa maabara ya uhamilishaji katika wilaya ya Mpwapwa.
Alisema lengo la kujenga maabara hiyo ni kupata mbegu bora ya mifugo na kuongeza wigo wa huduma hiyo.

“Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunakuomba utusaidie kuongea na taaisis za fedha ili ziwe na sera moja ya fedha na kuwawezesha wafugaji kukopesheka,” alisema.
----------------------------------------
NA WAANDISHI WETU, DODOMA
KATIBU Mkuu wa CCM, Abrahaman Kinana, amesema Chama kitaendelea kuwa karibu na wafanyakazi katika kuhakikisha maslahi yao yanapatikana.
 
Kinana alisema hayo jana alipokuwa akipokea kadi ya uanachama kutoka Chama cha Wafanyakazi wa Hifadhi, Hotelini, Nyumbani, Huduma za Jamii na Ushauri (CHODAWU) katika ukumbi wa CCM Makao Makuu, mjini hapa.

Alisema mara nyingi wafanyakazi wamekuwa wakijitetea wenyewe lakini kwa sasa kutokana na kupokea kadi hiyo kunakifanya chama kuwa karibu zaidi na wafanyakazi.

Kinana alisema CCM ni chama cha  wakulima na wafanyakazi lakini kimekuwa hakipo karibu sana na wafanyakazi ila kimekuwa karibu na serikali.

“Nadhani Chama kina wajibu wa kuwa karibu na wafanyakazi kuangalia maslahi yao, haki mazingira na kuwasemea,‘’ alisema.

Alisema wakati mwingine Chama kimetakiwa kuwa kipaza sauti cha wafanyakazi na haiwezekani kufanya vyote hivyo bila ya kuwa sehemu ya wafanyakazi.

Kinana alisema Chama pamoja na yeye binafsi atahakikisha anakuwa karibu na CHODAWU na Shirikisho la Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) ili kuwa karibu na wafanyakazi  katika maeneo yao kwa kuwa wamekuwa na malalamiko mengi.

Kwa mujibu wa Kinana alisema tangu kuchaguliwa kuwa Katibu mkuu amekuwa  karibu sana na Chama cha Walimu Tanzania (CWT) kwa sababu walimwandikia  barua kumwalika.
Alisema alishawahi kufanya vikao vingi nao na kila akienda  katika ziara zake anakutana na makundi mbalimbali kuzungumza nao wakiwemo walimu.

Alisema ni wajibu wa CCM sasa kama watendaji kuwa wanachama wa chama cha wafanyakazi kupitia sehemu inayowahusu na miezi michache ijayo ataanzisha tawi la chama hicho katika ofisi za CCM Makao Makuu ili wafanyakazi wapate chombo husika cha kupigania haki zao.

“Dhamira yangu ni kumfanya kila mtumishi wa Chama ambaye ataridhia kwa hiyari yake kuwa mwanachama wa CHODAWU na nina hakika watapenda,’’ alisema

Alisema kwa kuanzia ni vyema  kuanzishwa kwa tawi la Chama hicho katika Ofisi Kuu ya CCM na kuhaidi kuwa mmoja wa waanzilishi mpaka watakapopatikana viongozi watakaochaguliwa kwa njia ya  demokrasia.
 
“Tutaangalia muundo wa matawi yetu maana yametapakaa nchi nzima maana wanachama wana malalamiko yao lakini sina uhakika kama wanamahali pazuri pa kusemea,nimekuwa nikipokea barua watu wanalalamika kupitia chombo fulani sasa mdomo wa wengi ni bora kuliko wa mmoja mmoja,” aliongeza Kinana.

Aidha alisema anajivunia kuwa mwanachama wa CHODAWU kwa kuwa hajawahi kuwa mwanachama wa chama chochote cha wafanyakazi.

“Mimi  kwa kipindi kirefu nimekuwa jeshini, na jeshini kama mnavyojua ni amri tu na hutakiwi kuwa na mwanachama wa chama chochote,” alisema Kinana.

Kinana alitumia nafasi hiyo kumpongeza rais mpya wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi, Gratian Mukoba na kuahidi kutoa ushirikiano.
------------------------------------------------------------------
KIBANO BUNGENI
  • Posho sasa kudhibitiwa, Kiti chapewa rungu
  • Kanuni kali kuwabana wajumbe watoro
  • Vinara wa zomea zomea, matusi kukiona
WAJUMBE wa Bunge Maalumu la Katiba, wamependekeza kuwepo kwa kanuni kali za kuwadhibiti wanaozomea na kutoa lugha chafu ili kurejesha heshima ya bunge hilo.
Pia wamependekeza wajumbe wote wanaotoroka kuhudhuria vikao vya Bunge, kutolipwa posho za vikao pamoja na kumpa rungu mwenyekiti la kuwaadhibu wote watakaokwenda kinyume.

Mapendekezo ya mabadiliko ya kanuni hizo, yanatokana na kilio cha wananchi wengi baada ya wajumbe wa bunge hilo kufanya vitendo vya kitoto na visivyoendana na hadhi waliyonayo.

Tangu kuanza kwa bunge hilo Februari, mwaka huu, vitendo vya utovu wa nidhamu, ikiwemo matusi na lugha za kejeli, vimekuwa kitu cha kawaida miongoni mwa wajumbe wa bunge hilo, ambalo limepewa jukumu zito la kuwapatia Watanzania Katiba Mpya.

Akiwasilisha mapendekezo ya kanuni hizo bungeni jana, Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni, Pandu Ameir Kificho, alisema hatua hiyo imelenga kujenga na kuimarisha nidhamu ndani ya bunge.

Alisema mjumbe aliyepewa adhabu kwa mujibu wa kanuni, hatalipwa posho ya vikao ama kujikimu kwa muda wote atakaokuwa akitumikia adhabu.

Hata hivyo, alisema mjumbe ambaye atakuwa amepewa adhabu na tayari amechukua posho, hatalipwa katika vikao vinavyofuata na utaratibu husika utatumika kufidia fedha hizo.

“Mjumbe aliyepewa adhabu kwa mujibu wa kanuni, hatalipwa posho yoyote ya vikao au ya kujikimu kwa kipindi chote, na iwapo posho ilishatolewa, basi itakatwa kutoka katika malipo mengine ya mjumbe husika,” alisema Kificho.

Aidha alisema mapendekezo hayo yatakapopitishwa, kila mjumbe atapaswa kutia saini karatasi ya mahudhurio iliyoandaliwa na kwamba baadaye itawasilishwa kwa Katibu wa Bunge Maalumu.

Kanuni nyingine inayopendekezwa kufanyiwa marekebisho ni ya 36, ambayo inahusu upigaji wa kura wa ibara za Rasimu ya Katiba.

Kwa mujibu wa Kificho, bila kuathiri masharti ya Sheria na Kanuni, ibara za Sura za Rasimu ya Katiba zilizoandikwa upya, zitapigiwa kura katika muda wa siku saba.

Alisema kanuni zingine zilizopendekezwa kufanyiwa mabadiliko ni pamoja na  namba 14, 15, 32, 32b, 33,35,46,47,54,60,62 na 65.

Alisema kamati yake imeshamaliza kazi ya kujadili kanuni hizo kwa mujibu wa maelekezo ya Mwenyekiti wa Bunge.

Wakichangia mapendekezo hayo, wajumbe waliomba kuwepo kwa kanuni kali zitakazoweza kuwabana wajumbe wa Tume ya Marekebisho ya Katiba kuendelea kujadili na kutoa kauli dhidi ya Bunge.

Zainab Gama, alisema ni vyema kukawa na kanuni maalumu ambazo zitamtaka mjumbe yeyote ambaye hajahudhuria kikao kwa muda wa siku 15, afutwe nafasi hiyo.

Alisema kugomea vikao hivyo vya Bunge ni kutumia vibaya nafasi ya uwakilishi katika bunge hilo maalumu.

Kwa upande wake, Dk Ave-Maria Semakafu, alisema ni muhimu kwa bunge hilo kuhakikisha kuwa masuala ya elimu, afya na usawa wa kijinsia vinapata nafasi katika majadiliano ya rasimu hiyo.

Alisema masuala ya muundo wa uongozi si kipaumbele cha wananchi kwani nia ya wananchi ni kupata katiba inayowagusa wananchi katika mambo yao.
SITTA ALALAMA
Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta, amelalamikia baadhi ya vyombo vya habari ambavyo vimekuwa vikitumika kuendesha midahalo inayowadhalilisha wajumbe wa bunge hilo.

Alisema vyombo hivyo vimekuwa vikirusha vipindi hivyo moja kwa moja, ambapo washiriki wamekuwa wakiegemea upande mmoja huku wengine wakitoa lugha chafu zenye kuudhi pamoja na kuwazomea wengine wanaoonekana kuwa upande tofauti.

ìInashangaza kuona watu hawa wanapewa nafasi na ni wale wale kila siku. Hebu Mama Mukangara (Dk. Fenella-Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo), angalia kuna nini huko, lakini pia nadhani serikali inasikia hili,” alisema.

Hivi karibuni, vituo kadhaa vya luninga vimekuwa vikirusha midahalo kuzungumzia Katiba Mpya, ambapo baadhi ya washiriki wamekuwa wakitumia lugha za kuudhi.
 
Mjumbe Thomas Mgoyi, alisema tume imeshafanya kazi yake na imemaliza, hivyo inabidi waachane na kulishambulia Bunge  Maalumu la Katiba.

"Watuache tufanye kazi za wananchi kuliko kutusema na kututukana maana tutashindwa kuvumilia,î alieleza.

MMANDA AZUNGUMIA RASIMU
Mmoja wa wajumbe wa Kamati ya Kanuni, Evod Mmanda, alisema bunge hilo lina uwezo wa kujadili Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume ya Jaji Warioba.

Alisema bunge hilo lina nguvu na mamlaka ya kujadili na hata kuboresha kilichowasilishwa kabla ya kwenda kupigiwa kura na wananchi.

Hata hivyo, alisema hakuna kanuni za kuwabana wanaoandaa midahalo nje ya bunge kwa kuwa, kanuni zinahusu kungíata wajumbe ndani ya bunge.

Pia alisema kanuni wala sheria hazisemi iwapo wajumbe wa kundi la 201, wanaweza kuadhibiwa iwapo watatoka ndani ya bunge kwa kuwa sheria haisemi kama wanaweza kufukuzwa.

Mmanda alisema sheria ipo wazi kuwa, iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ilishamaliza kazi yake na waliokuwa wajumbe wake wanazungumza kwa utashi wao.

No comments:

Post a Comment

Toa Maoni kistaarab kwa Hoja kwa faida ya wenzako. au tundikie kupitia nkoromo@gmail.com, simu 0672223269

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages